KURASA

Monday, February 8, 2010

DARAJA LINALOISHI



Huko nchini INDIA sehemu za CHERAPUNJEE ambako ni eneo tengefu lenye majimaji ambako wanapatikana watu jamii ya KHASIS huwa wanatumia mizizi ya miti jamii ya mipira kutengeneza madaraja kwa ajili ya matumizi ya kila siku.



Wanachofanya ni kuielekeza mimizi ya mti husika kukua kuelekea upende wa pili wa mto, kwa kawaida miti hii huwa na mizizi ya chini ya udongo na ile ambayo hutokea kwenye matawi na kuelea elea hewani, kwa hiyo mizizi hii inayoelea hewani huongozwa kukua kufuatana na matakwa ya watu hao mpaka upande wa pili na hapo huachiwa ikue kwa kuingia ardhini ili kupata uimara unaohitajika.



Ili kupata daraja kamili na lenye uimara unaohitajika zoezi hili huchukua kati ya miaka 10 hadi 15, na yapo madaraja yenye hadi refu wa futi 100 na huwa na uwezo wa kuhimili jumla ya watu 50 kwa pamoja kama wote watakaa juu ya daraja husika. Kati ya madaraja hayo lililo maarufu zaidi hujulikana kama UMSHIANG DOUBLE DECKER ROOT BRIDGE ambalo kama jina lake lilivyo lina njia mbili ya juu na chini

DARAJA LA UMSHIANG


Sunday, February 7, 2010

MBUZI WA MOROCCO

Mbuzi unaowaona pichani hupatikana nchini MOROCCO, inasemekana ni kawaida kuwaona mbuzi wakiwa wamepanda juu ya hivyo vichaka ni kwa sababu wanafuata matunda yajulikanayo kama ARGO, kutokana na kuyapenda sana matunda hayo basi mbuzi hao hudandia juu ya matawi ya vichaka ili kupata matunda hayo



Tuesday, January 26, 2010

SIMBA MWENYE FADHILA



Mwaka 1969 John Rendall na Ace berg walimuona mtoto wa simba (dume) aliyekuwa anauzwa huko Harrods alionekana mpweke ndani ya kibanda chake kidogo na wakaamua kumnunua na kwenda naye nyumbani kwao ambako ni ghorofani na wakampa jina la Christian. Paroko wa kanisa moja aliwaruhusu kucheza naye katika viwanja vya kanisa lakini ndani ya muda mfupi simba alikuwa haraka na kuwa mkubwa ambako kwenye nyumba yao asingeweza kuendelea kuishi zaidi ya hapo.

Wakaamua kumrudisha kwenye mazingira yake ya asili kwenye mbuga za Afrika na baada ya Mwaka walipotaka kumtembelea waliambiwa ya kwamba amekuwa mkubwa na kuwa na milki yake na sasa amegeuka mnyama pori kamili kwa hiyo ni hatari kama simba wengine kwa maana hiyo wasingeweza kumsogelea karibu tena, pamoja na hayo bado waliamua kwenda kumuangalia hivyo hivyo, baada ya kumtafuta kwa masaa kadhaa walifanikiwa kumuona…….. ukiangalia kwenye video hii utaona jinsi alivyo warukia kwa furaha akiruka ruka, kucheza nao huku nao wakimkumbatia na wala hakuwa mkali au hatari kwao kama walivyoambiwa, na mwisho alikuja simba mwingine jike ambaye alikuwa ni mke wake kwenye hiyo milki yake na huyo simba jike naye akabaki akiwaangalia tu na wala hakuwashambulia ( ni kama naye alitambulishwa)

Saturday, January 23, 2010

VODACOM NA WAATHIRIKA WA MAFURIKO



Katika kuthamini waliopatwa na maafa ya mafuriko pote nchini kampuni ya simu ya VODACOM imeanzisha kampeni inayojulikana kama RED ALERT itakayowawezesha wateja wake kuchangia kadri wawezavyo ili kuwasaidia waathirika wa mvua na mafuriko pote nchini

Kwa ufupi ni kwamba ukitaka kuchangia waliopatwa na maafa pote hapa nchini kama Kilosa, Same, Tanga na Dodoma basi tuma neno MAAFA kwenda namba 15599 na hapo utakatwa shilingi 250/= (PAMOJA NA KODI) kama mchango wako kwa waathirika wa mvua na mafuriko.

Serekali imefanya tathmini na kutangaza kwamba kiasi cha shilingi billioni 10 zinahitajika ili kuweza kuwasaidia wale walioathirika mpaka hali itakapo tengemaa, na kampeni hii ni kuanzia tarehe 24th January 2010 paka 30th January 2010 (wiki moja tu)

MTI MZEE ZAIDI DUNIANI

Mti mzee kuliko yote duniani ulio hai ni bristlecone pine (Pinus longaeva) unaoitwa Methuselah mti huu unapatikana marekani California katika mlima mweupe, mti huu ambao uko futi 11,000 juu ya usawa wa bahari una miaka 4838 na sio tu ni mti mzee zaidi bali ni kiumbe kizee zaidi duniani cha asili (non-cloned) kilicho hai
Kabla ya Methuselah haujagunduliwa kwamba ni mti mzee zaidi duniani Mwaka 1957 na Edmund Schulman iliaminika kwamba mti mkubwa aina ya Sequoias ndio mti wenye umri mkuwa zaidi ukiwa na miaka 2000

MITI AINA YA METHUSELAH HUKO CALIFORNIA KATIKA MLIMA MWEUPE


Mti mwingine aina ya Prometheus uligunduliaka baada ya mwanafunzi wa Mwaka wa mwisho chuoni 1964 ajulikanaye kama , Donald R. Currey alipokuwa akifanya majaribio ya kisayansi na kifaa chake cha kuchimbia viini vya miti miti kuvunjika ndani ya mti, aliomba ruhusa ya kuukata mti huo (iliauchunguze zaidi) kutoka idara ya misitu na alistaajabu alipokubaliwa (wenzetu hawakati miti hovyo hovyo bila sababu maalum) na baada ya kuukata mti huo ndipo walipogundua kwamba ni mti wenye umri mkubwa zaidi duniani ukiwa na zaidi ya miaka 5000.

MITI AINA YA METHUSELAH WENYE MIAKA 4838



Kwa hiyo Prometheus ndio mti mzee zaidi kugunduliwa lakini umekufa baada ya kukatwa na Methuselah ndio mti mzee zaidi duniani ulio hai mpaka sasa. Miti ya Methuselah iko mingi na yote ikiwa na umri zaidi ya miaka 4000 na ipo California katika mlima mweupe lakini mahali ulipo kutwa mti wa Prometheus pamefanywa siri kwani bado wanaendelea kulichunguza eneo hili wakiamini wataukuta mti mwingine wenye umri unaofanana na ule walioukata

KISIKI CHA MTI WA PROMETHEUS BAADA YA KUKATWA

Tuesday, January 19, 2010

MTI MPWEKE ZAIDI DUNIANI

Mti aina ya acacia ulioota kwenye jangwa la sahana nchini Niger ndio mti ulio mpweke zaidi baada ya kuwa umbali wa zaidi ya maili 250 pande zote bila kukutana na mti mwingine. Mti huu uligunduliwa Mwaka 1970 lakini uliota mahala hapo wakati jangwa halijawa kavu kama lilivyo sasa, kwa miaka hiyo ambako mti huu uliota haukuwa peke yake bali kulikuwa na miti mingine ila yenyewe ilikufa baada ya jangwa hili kuendelea kuwa kavu zaidi na kupata kiasi kidogo cha mvua

MTI MPWEKE PICHANI



Mtii huu Ulikufa baada ya dreva wa lori kutoka Libya alipougonga, inasemekana dreva huyo alikuwa akiendesha lori hilo huku akiwa amelewa pombe. Baada ya mti huu kufa wana sayansi walichimba pembeni yake na kugundua mizizi ilikwenda chini kiasi cha futi 120 (mita 36) mpaka kufikia maji ya chini ya ardhi (water table) Sasa hivi sehemu ulipoota mti huo imejengwa nguzo ya chuma kama kumbukumbu ya mti mpweke zaidi duniani

NGUZO MAHALI ULIPOKUWA MTI MPWEKE

Sunday, January 17, 2010

UGONJWA WA MIGUU NA MIDOMO - FOOT AND MOUTH DISEASE

KWATO ZA MNYAMA MWENYE FMD


Ugonjwa huu husababishwa na virusi jamii ya Aphtovirus vinavyoambukiza binadamu pia (Aphtae epizooticae) ambavyo vipo kwenye Makundi ya A, O, C, SAT1, SAT2, SAT3, Asia1, vinauwezo wa kuishi kwenye matezi na ndani ya mifupa (bone marrow) madhali PH isiwe chini ya 6 na vinauwezo wa kuendelea kuishi kwenye mwili wa mnyama aliyekufa au kwenye udongo kwa mwezi mzima madhali PH isizidi 6. Kama lilivyo jina lake ugonjwa huu hushambulia kwato na midomo (fizi)
Ugonjwa huua zaidi ndama kuliko wanyama wakubwa, hushambulia wanyama wenye kwato kama ng’ombe, mbuzi, kondoo, punda, farasi, nguruwe, nyati maji, na wanyama wengine wenye kwato wanyama jamii ya ngamia, llama na nyati pori, huwa hawasumbuliwi sana na ugonjwa huu

MIKONO YA MTU ALIYEAMBUKIZWA UGONJWA


KUSAMBAA
Ugonjwa hussambazwa kwa njia ya mate, machozi, kinyesi, viatu, vifaa vya kuhudumia wanyama, nyama, maziwa, magari na hata hewa hasa kwa ukanda wa pwani usizidi futi 300 kutoka usawa wa bahari, wanyama ambao wana vijidudu na hawaumwi (carriers) kama nyati pori pia husambaza ugonjwa huu.

DALILI KUU
Toka mnyama aambukizwe huchukua siku 2 -14 na dalili kuu ni uzalishaji wa maziwa kushuka, kusaga meno, joto hupanda, mnyama huchechemea na kurusha mateke, ukiangalia fizi na kati kati ya kwato utaona kama vipele ambavyo baadae hupasuka na kuwa vidonda, wanyama hutoa mimba na wanyama wadogo (ndama )hufa

DAWA
Ugonjwa huu hauna dawa, bali unaweza kutibu vidonda kwa kutumia dawa (antibiotic) kama ulipo hakuna dawa unaweza kutumia chumvi au magadi ukiyeyusha kwenye maji na kuosha kwenye fizi na kwato za mnyama

KINGA
Kuna chanjo za ugonjwa huu ambazo hupigwa , sindano ya pili hupigwa baada ya siku 30 na baada ya hapo ni kila baada ya miezi 6 ( waone maafisa ugani wa mifugo) unaweza kuwakinga wanyama wako kwa kuzuia mwingiliano na wanyama wengine na kabla ya kuleta mnyama mpya hakkisha amepata chanjo zote (sijui wangapi wanafanya hii) pia karantini zitumike mara mlipuko wa ugonjwa huu unapotokea, wanyama wenye ugonjwa wauwawe na kuchomwa moto (incineration)

MFANO WA KIBAO CHA KARANTINI


WANYAMA WENYE UGONJWA WAKICHOMWA MOTO

Tuesday, January 12, 2010

KAMBALE ANAYETEMBEA

Hii ni aina ya kambale inayopatikana sana bara la Asia na Africa, amepewa jina la kambale anayetembea sababu ya uwezo wake wa kujikongoja na kuhama toka sehemo moja hadi nyingine kupitia nchi kavu kwa dhumuni la kutafuta chakula au mazingira mazuri, sio kwamba anatembea bali hujinyanyua juu kwa kutumia mapezi yake na kujinyonga nyonga kama nyoka na ii humuwezesha kusogea mbele, ana uwezo wa kuka muda mrefu nje ya maji madhali ardhi isiwe kavu bali iwe na unyevu

Hupendelea kwenye maji yenye kina kifupi au yasiyotembea, kama kwenye vijito na mito, mabwawa, majaluba ya mpunga na sehemu yoyote ambayo maji hujikusanya. Hukua hadi sentimeta 30 (urefu wa rula ya mwanafunzi) hana magamba kama kambale wengine bali ngozi yake huwa na ulenda ulenda unaomsaidia atembeapo nchi kavu, ana rangi ya kijivu mpaka kahawia iliyokolea kabisa. Tofauti na yake na kambale wengine yeye hana mapezi ya kwanza juu ya mgongo bali pezi lake la pili huwa refu mpaka karibu na mwisho wa mkia, unapomvua kambale huyu usimshike akiwa hai au hata kama kafa mshike kwa umakini sababu ana miiba iliyojificha kwenye mapezi ya chini karibu na mkia



Hupendela halijoto kati ya 10c mpaka 28c, chakula chao kikuu ni samaki wadogo, wadudu, konokono wasio na magamba na mimea ya kwenye maji, kambale hawa wanatabia ya ulafi inayowafanya wawe hatari kwa viumbe wengine wa kweye maji

Saturday, January 9, 2010

ADHA YA MVUA JIJINI DAR ES SALAAM


Kuwasha taa ni muhimu maana madereva hawaoni vizuri mbele kwa sababu ya ukungu kwenye vioo vya mbele





Hapo hata dala dala hazitanui maana inaweza kudumbukia kwenye mtaro, njia haionekani




Ukiwa na mwamvuli hautaloana labda miguuni ndio kasheshe


Magari (hasa ya petroli) nayo hupata hitilafu na kuzimika, hii husababisha adha kwa wenye kuyamiliki na gharama za ziada kama kusukumwa na kuyatengeneza tena


Limebuma


Jamaa anashuka......


Jamaa hana la kufanya anatafakari.... nyuma foleni kama treni


Jamaa anafurahia mvua kwa sababu lazima atauza makoti na mabuti ya mvua hahahahhe!!!!! kufa kufaana


Vituo vya kuwekea mafuta navyo vimefurika maji, je yakiingia kwenye matanki ya mafuta si tutauziwa maji-balaa hili........



Hata zoezi la kuzoa taka hufanyika kwa tabu na jamaa hawana vifaa vya kujikinga angalau gum boot

Sunday, January 3, 2010

MVUA NA MIUNDO MBINU YETU

Jamani heri ya mwaka mpya kwenu nyote, namshukuru MUNGU niko buheri wa afya, Leo nitawaonyesha baadhi ya picha zinazoonyesha tabu tunayopata tukiwa field kutokana na madhara ya mvua kwenye barabara ambazo si za lami, kwa kweli kuna sehemu hata gari ikiwa na 4wheel drive inaweza isipite, pia kunatakiwa uzoefu wa kuendesha kwenye barabara hizo, kama wewe ni dereva wa mjini kwenye lami tu basi kazi utakuwa nayo

TANGA







MANYARA


RUKWA





RUVUMA


Hivi mnategemea kwa kutumia barabara hizi mkulima ataweza kweli kusafirisha mazao yake na kuyapeleka mjini kwenye masoko au mazao hasa yale yanayooza haraka kama matunda na mboga mboga si yataharibikia shambani.

Wednesday, December 30, 2009

MNYAUKO FUSARI - COFFEE FUSARIUM

Ugonjwa huu husababishwa na vimelea vya fusari. Hushambulia mashina, machipukizi na hata punje. Ugonjwa wa mnyauko fusari unashamiri kwenye mashamba ambayo hayatunzwi vizuri inavyopasa. Viini vya ugonjwa huu vinauwezo mdogo sana wa kushambulia
mkahawa wenye afya nzuri, ukiona shamba limeshambuliwa na uonjwa huu jua moja kwa moja kwamba shamba hilo halitunzwi vizuri kwa kufuata kanuni za kilimo bora.

DALILI KUU:

Machipukizi yaliyoshambuliwa na ugonjwa huu hunyauka, na majani hubadilika na kuwa na rangi ya kahawia. Matawi na mashina yakishambuliwa hunyauka na kufa. Ukitaka kuthibitisha dalili za fusari kata shina utaona miviringo ya kahawia. (Brown ring)

JINSI YA KUZUIA
• Palizi ni muhimu kwenye shamba.
• Ukataji sahihi wa matawi.
• Matumizi ya mbolea kwa kiwango kinachoshauriwa.
• Ng’oa na choma moto mikahawa iliyokufa.
• Iwapo ni matawi yanayoonyesha dalili za ugonjwa matawi hayo yakatwe na kuchomwa moto.

NB: Miche mingine ya kahawa isipandikizwe sehemu ilikong’olewa
mikahawa yenye ugonjwa kabla ya miezi sita.

SALAMU ZA MWAKA MPYA

Jamani kwa mwaka huu hii ni makala yangu ya mwisho, mwenyezi Mungu akinijaalia nitaendelea mwakani kuwaletea makala nyingine, mwaka huu Mungu aliniwezesha kutuma jumla ya makala 77 ambazo naamini kuna watu zimewasaidia na kuwanufaisha, kuna wengine wamekuwa wakiniuliza maswali kwa faragha na hawakupenda nichapishe majina yao nawashukuru sana, kuna wale walioanzisha mashamba mapya au walikuwa na mashamba na walihitaji ushauri wa kitaalam nao nilishirikiana nao vizuri, kuna ambao walitaka msaada wangu walipata lakini walishindwa gharama za mradi nawaombea kwa Mungu awawezeshe kupata pesa za kuanzisha miradi hiyo, Kuna nilio wakwanza kwa kushindwa kuwasaidia, inawezekena nilibanwa na ratiba au ushauri wangu haukuwa na manufaa kwao na wale walioshindwa gharama za ushauri (ingawa ni sawa na bure) NAOMBA WANISAMEHE

Monday, December 28, 2009

KUTU YA MAJANI - COFFEE LEAF RUST

Huu ni mwendelezo wa magonjwa makuu ya kahawa
Kutu ya Majani ni ugonjwa unaosababishwa na vimelea vya ukungu jamii ya Hemileia vastatrix; Ugonjwa huu ushambulia karibu aina zote za kahawa; hasa katika nyanda za chini ambako kuna joto zaidi. Ugonjwa wa kutu ya majani hujitokeza kabla ya mvua za masika kuanza.



MAZINGIRA MAZURI YA VIMELEA VYA KUTU YA MAJANI:
• Joto lililo ambatana na unyevu nyevu mwingi angani.
• Kivuli kinachosababishwa na miti mingi shambani au matawi
ya kahawa.
• Magugu jamii ya Oxalis.
• Kahawa zilizozeeka kupita kiasi nazo hushambuliwa kwa urahisi.

MASHAMBULIZI NA DALILI
• Kutu au rangi ya machungwa iliyochanganyika na manjano huonekana upande wa chini wa majani ya kahawa.
• Kudondoka kwa majani yangali bado machanga.
• Kudumaa kwa matawi.
• Kukauka kwa ncha za matawi.
• Hatimaye mavuno hupungua kwa kiasi kikubwa.

UGONJWA UNAVYOSAMBAZWA:
• Upepo huongeza kasi ya kusambaa kwa vimelea vya kutu ya majani.
• Wanyama (ndege) wadudu, husambaza vimelea vya kutu ya majani toka mmea mmoja hadi mwingine.
• Miezi michache kabla ya Vuli vimelea vya kutu ya majani huanza kukua;
- Vimelea hivi hujihifadhi kwenye magamba ya shina la kahawa na matawi makubwa (Primary branches) hasa kahawa zilizozeeka.
- Kipindi hiki huwa na joto.
• Vuli husaidia kuongeza kasi ya kukua kwa vimelea hivyo na kusambaza.
- Kutokana na unyevunyevu uliopo kwenye majani na kahawa kwa ujumla.
• Vimelea vya ukungu wa aina hii vinapoendelea kusambaa ndivyo na ashambulizi ya mmea yanavyoongezeka.
• Mashambulizi huendelea kipindi chote cha joto hadi masika, kipindi ambacho vimelea hukosa nguvu.
• Nguvu ya vimelea vya kutu ya majani huanza tena kidogo kidogo
baada ya masika kwisha.



KUPAMBANA NA KUTU YA MAJANI:
• Shamba liwe safi wakati wote.
- Punguza kivuli cha miti na migomba kwenye shamba la kahawa.
- Punguza matawi ya kahawa (pruning); wakati wa kukata matawi kata matawi yote yalivyozeeka; na yaliyo na ugonjwa.
- Lima ili kupunguza magugu hasa jamii ya oxalis.
• Hakikisha udongo una unyevunyevu wa kutosha, wakati wote: (weka matandazo, mbolea na kumwagilia maji)
• Ondoa magamba kwenye kahawa kwa kutumia brush / magunzi mbalimbali.
• Jaribu sumu za asili kama utupa (rejea makala zangu).
• Sumu za viwandani (mrututu) zitumike pale tu ambapo ni lazima kufanya hivyo kufuatana na hali ya hewa;
- mrututu (copper) utumike kama kinga mara baada ya mvua za masika kama joto liko juu likiambatana na unyevunyevu angani.
- Endapo kutu ya majani imeshamiri tumia Bayleton kama tiba (control) lakini si zaidi ya mara 2 kwa msimu.
NB: Wakati wa kunyunyuzia sumu elekeza bomba chini ya majani.

Saturday, December 26, 2009

MAGONJWA MAKUU YA KAHAWA

Magonjwa makuu ya kahawa ni haya yafuatayo
- Chule buni (CBD)
- Kutu ya majani (Coffee leaf rust)
- Mnyauko fuzari (Fusarium)
Leo nitaongelea ugonjwa wa chule buni

CHULE BUNI (CBD- Coffee Berry Disease)
Chule Buni (CBD) ni ugonjwa wa matunda ya kahawa ambao umeenea sehemu nyingi nchini hasa zile za miinuko ya juu. Ugonjwa huu husababishwa na fangas wajulikanao kama colletotrichum kahawae. Ushambuliaji huwa ni mkubwa zaidi wakati wa mvua za masika kwani wakati huu hali ya unyevu unyevu kwenye hewa ni mkubwa na hali ya hewa ni ya baridi.

MFANO WA TUNDA LILISHAMBULIWA


MADHARA
Ugonjwa huu ni mbaya sana na huenea kwa kasi. Mbuni ulioshambuliwa haufi bali mkulima anaweza kupoteza mpaka asilimia 90 ya mavuno kwa mwaka kama hatazingatia namna bora ya kuuzuia.

Ugonjwa huu hushambulia mibuni katika hatua tatu muhimu nazo ni:
• Maua yanapochanua.
• Punje zikiwa changa na laini.
• Punje zinazoiva.

Madhara makubwa hutokea wakati punje zikiwa changa na laini.
Mara nyingi mibuni iliyoshambuliwa na Chule Buni matunda yake huwa na vidonda vyeusi na vilivyobonyea na hudondoka na mengine hubakia kwenye mibuni. Yale matunda yanayobakia yanakauka na kuwa chanzo cha uambukizaji kwenye mavuno ya msimu unaofuata. Picha ya mbuni ulioshambuliwa na Chule Buni

JINSI YA KUZUIA
Ili mkulima aweze kudhibiti vizuri ugonjwa huu anashauriwa:
• Kupunguza matawi yasiyotakiwa ili sumu iweze kupenya vizuri
na kufikia matunda yote.
• Kutumia sumu sahihi zilizopendekezwa kutumika kwenye kahawa.
• Kutumia kiasi na kipimo sahihi kilichopendekezwa.
• Kunyunyizia sumu wakati sahihi yaani:

1. Kabla ya ugonjwa haujatokeza.
2. Unyunyuziaji dawa uanze wiki tatu kabla ya mvua za vuli kuanza (Oktoba - Novemba) na kurudiwa tena mwezi mmoja baadae (Disemba).
3. Unyunyiziaji unaofuata ufanyike tena wiki tatu kabla ya mvua za masika (Machi) na kurudiwa kila mwezi hadi matunda yakomae (Julai)
• Aelekeze dawa kwenye matunda.



Mkulima anashauriwa kunyunyizia sumu mojawapo ya hizi zifuatazo:
1. Jamii ya mrututu - hasa zile nyekundu na za bluu zilizopendekezwa kudhibiti Chule buni. Mfano: Nordox, Cobox, Funguran-OH.
2. Jamii isiyo ya mrututu - hizi mara nyingi ni zile za maji maji zilizopendekezwa kutumika kwenye kahawa mfano: Bravo, Daconil na Dyrene.

FAIDA YA KUDHIBITI
Mkulima akidhibiti vizuri Chule Buni anapata faida zifuatazo:
1. Atakuwa amepunguza uwezekano wa kuendelea kuongeza kasi ya huu ugonjwa mwaka hadi mwaka.
2. Atakuwa ameongeza wingi na ubora wa kahawa.
3. Atakuwa amejiongezea kipato chake na kuwa na maisha bora zaidi.
4. Atakuwa ameongeza pato la taifa kwa ujumla.

MAMBO YA KUZINGATIA
• Mwisho wa msimu hakikisha unaondoa matunda yote haswa yale yaliyoshambuliwa na chule buni.
• Tambua wakati sahihi wa kuzuia huu ugonjwa.
• Nunua sumu sahihi zilizopendekezwa.
• Hakikisha matunda yote yanapata sumu vizuri.
• Epuka ununuzi holela wa sumu kwani unaweza kununua hata zile zilizokwisha muda wake.
• Mara upatapo tatizo onana na mtaalamu wa kilimo/afisa ugani aliyekaribu nawe.

Saturday, December 19, 2009

LEHEMU - CHOLESTEROL

Dada Mary Chuwa alipenda kujua kuhusu lehemu kwenye mafuta, kwa lugha ya kiingereza lehemu ni cholesterol, kwa kawaida kuna aina mbili za cholestrol low density lipoprotein na high density lipoprotein aina zote mbili zinatokana na balance ya kemikali mbili za mafuta zijulikanazo kama polyunsaturated fats na monounsaturated fats. kama hizi kemikali mbili zitabalance zitatengeneza low saturated fats ambazo ni high density lipoprotein, hii ni cholestrol nzuri kwa mwili wa binadamu kwa sababu haina madhara, ila kama polyunsaturated fats na monounsaturated fats hazita balance zitaengeneza low density lipoprotein ambayo ni cholestrol mbaya na inamadhara katika mwili wa binadamu.

Lehemu mbaya (low density lipoprotein) ikiingia mwilini huganda kwenye kuta za mishipa ya damu na kwenye moyo hivyo kufanya njia za damu kuwa nyembamba na kusababisha magonjwa ya moyo au kiharusi (stroke)

Mafuta yatokanayo na Alizeti, karanga na mahindi kwa asili huwa hayana lehemu mbaya an hivyo kuwa salama kwa matumizi ya binadamu. Mafuta ya mawese, nazi, na yale yatokanayo na wanyama pamoja na mazao ya maziwa huwa na lehemu mbaya

Mikoa ya Singida na Manyara imekuwa ikizalisha kwa wingi sana alizeti na kuna viwanda vya kukamua mafuta sehemu hizo, kwa hiyo nashauri kama unaweza agizia mafuta halisi ya alizeti toka sehemu hizo, mbegu za alizeti hukamuliwa ilikupata mafuta na baada ya hapo mafuta huchemshwa na kuchujwa kisha kuwekwa kwenye madumu tayari kwa kuuzwa.

Ili kupunguza lehemu mwilini mwako inashauriwa kutumia asali kijiko kimoja na mdalasini nusu kijiko kila asubuhi kabla hujala chochote, unaweza kutia kwenye chai au maji ya moto mchanganyiko huu.
nakaribisha maoni kwa wenye ufahamu zaidi

Monday, December 14, 2009

NDIGANA KALI - EAST COAST FEVER (ECF)

Huu ni ugonjwa wa ng’ombe, nyati na nyati wa India wakaao kwenye maji (water buffalo) ambao umeenea sana hapa nchini kwetu, msambazaji mkuu ni kupe (rephicephalus appendiculatus) na ng’ombe huanza kuugua siku 10 – 25 (wastani siku 14) toka kuambukizwa ugonjwa huu, protozoa aina ya theileria parva ndiye husababisha ugonjwa huu



DALILI KUU ZA NDIGANA KALI
-Joto kali hadi kufikia 42c kwa kawaida ng’ombe huwa na joto 38c
-Manyoya ya mgongoni husimama muda wote na huwa na rangi ya udongo (brown) kwa mbali
-Kuharisha
-Kutoa makamasi laini
-Matezi ya shingo kuvimba
-Kupe aina ya rephicephalus appendiculatus utawaona kwenye masikio ya mnyama (sio lazima)
-Mnyama hushindwa kula vizuri
-Pua (muzzle) huwa kavu bila unyevu unyevu



TIBA
Dawa aina ya BUTALEX ni maarufu sana hapa nchini kwa ajili ya kukabiliana na ugonjwa huu, ni muhimu dalili za mwanzo zinapoonekana kumtaarifu mtaalam wa mifugo na ikithibitika ni Ndigana kali tiba ianze mara moja ikiambatana na OTC 20% ili kushusha homa.

KINGA
Kinga kubwa ni kuogesha mifugo yako mara kwa mara, dawa ya ruzuku ijulikana yo kama PARANEX hupatikana katika maduka yote ya kilimo na mifugo. Dawa nyingine nazo zinafaa kuogeshea kwa kufuata masharti ya mtengenezaji.

Friday, December 11, 2009

TANGAWIZI

1.0 UTANGULIZI:
Jina la kitaalamu ni Zingiber officinale
Tangawizi ni aina ya zao la kiungo ambalo sehemu inayotumika ni tunguu (rhizome) ambalo huonekana kama mizizi ya mmea. Asili ya zao hili ni maeneo ya kitropiki ya bara la Asia na hasa katika nchi za India na China. Zao hili linazalishwa kwa wingi kutoka katika nchi ya Jamaica. Hapa nchini zao hili hulimwa katika mikoa ya Kigoma, Tanga, Morogoro, Pwani, Mbeya na Kilimanjaro.



Tangawizi hutumika kama kiungo katika kuongeza ladha, harufu na kuchangamsha katika vinywaji (kama chai, soda, juisi, vilevi n.k) na vyakula mbalimbali kama mikate, biskuti, keki, nyama za kusaga, achari n.k. Hutumika pia katika viwanda vinavyotengeneza madawa ya tiba mbalimbali kama dawa za meno, kikohozi, tumbo na muwasho wa ngozi n.k. pia hutumika katika vipodozi kama poda n.k).

2.0 AINA ZA TANGAWIZI
Hakuna uthibitisho wa aina za tangawizi ambazo hulimwa hapa nchini ila kuna dalili ya kuwa na aina za White Africa (Jamaica) na Cochin (flint); hii huwa na tunguu ngumu zenye nyuzi.

3.0 TABIA YA MMEA
Tangawizi ni mmea unaotambaa chini ya ardhi, wakati wa masika hutoa majani juu ya ardhi. Jamaica ina rangi hafifu ya kahawia na tunguu fupi wakati Cochin ina tunguu fupi zaidi lenye ngozi ya rangi iliyo kati ya kijivu na nyekundu. Mmea una urefu wa futi mbili na majani yake ni membamba marefu ambayo hufa kila mwaka yakiacha tunguu ardhini likiwa hai. Maua ya mmea huu yana rangi nyeupe au manjano.

4.0 HALI YA HEWA NA UDONGO
Zao hili hustawi katika maeneo yenye hali ya kitropiki, kutoka usawa wa bahari hadi mwinuko wa mita 1,500 au zaidi. Huhitaji mvua kiasi cha mm.1,200-1,800 na joto la wastani wa nyuzi za sentigredi 20-25. Hustawi vema katika udongo tifutifu wenye rutuba na usiotuamisha maji.

MMEA WA TANGAWIZI


5.0 UPANDAJI
Zao la tangawizi hupandwa kwa kutumia vipande vya tunguu vyenye kichipukizi kizuri angalau kimoja na huweza kukatwa katika urefu wa sm.2.5-5. Wakati mwingine, vichipukizi vinavyopatikana katika kumenya tangawizi huweza kuhifadhiwa na kutumika kwa kupanda. Kiasi cha kilo 840-1700 cha vipande vya tunguu huweza kutumika kwa kupanda katika hekta moja. Nafasi inayotumika kupanda ni kati ya sentimita.23-30 kwa 15-23 na kina cha sentimita.5-10 na mara nyingi hupandwa katika matuta. Baadhi ya mazao huweza kupandwa katika shamba la tangawizi ili kuweka kivuli chepesi ingawa si lazima kivuli kiwepo. Inashauriwa kumwagilia maji endapo mvua inakosekana.

Wiki 1-2 kabla ya kupanda weka mbolea ya samadi au mboji kiasi cha tani 25-30 kwa hekta na kwa kukuzia weka kiasi cha NPK kwa uwiano wa kilo 36:36:80. Tandaza nyasi shambani kuhifadhi unyevunyevu hasa pale kivuli kinapokosekana. Palizi hufanywa mara magugu yanapoota, dawa ya kuua magugu, kama simazine au round up hutumika.

MKATE WA TANGAWIZI NA LIMAO


6.0 Magonjwa na wadudu:
• Madoa ya majani yanayosababishwa na viini vya magonjwa viitwavyo Colletotrichum zingiberis na Phyllosticta zingiberi.
• Kuoza kwa tunguu; kunasababishwa na viini viitwavyo Pithium spp
• Mizizi fundo; inasababishwa na Meloidegyne spp.

7.0 UVUNAJI
Tangawizi huweza kuwa tayari kwa kuvuna kati ya miezi 9-10 baada ya kupanda, wakati majani yake yanapogeuka rangi kuwa njano na mashina kusinyaa. Tangawizi inayohitajika kwa kuhifadhi kwenye kemikali (preserved ginger in brine) huvunwa kabla haijakomaa kabisa, wakati ile iliyokomaa kabisa huwa kali zaidi na huwa na nyuzi hivyo hufaa kwa kukausha na kusaga. Mavuno hutofautiana kulinganana na huduma ya zao, mavuno yanaweza kuwa kiasi cha tani 20-30 cha tangawizi mbichi huweza kupatikana.

8.0 USINDIKAJI
Tangawizi ikisindikwa utapata unga, mafuta maalum (essential oils) n.k. Tangawizi iliyovunwa huweza kumenywa, kukatwa na kukaushwa juani au mara nyingine huchovywa katika maji yaliyochemka kwanza na ndipo kukaushwa au hukamuliwa mafuta. Pia tangawizi husindikwa na kuhifadhiwa kwenye chupa zikiwa zimechanganywa na sukari na/au chumvi au bila kuweka kitu chochote. Hata hivyo tangawizi ina Kiasi cha mafuta cha 16.0-18.0%.



9.0 SOKO LA TANGAWIZI
Soko la tangawizi lipo ndani na nje ya nchi, kiasi kikubwa kinauzwa nchini. Bei yake ni kati sh. 300-1,500/- kutegemeana na msimu.

10.0 GHARAMA ZA UZALISHAJI NA MAPATO
GHARAMA YA HEKTA MOJA:
Mbegu Tshs. 240,000/-
Vibarua 250,000/-
Mbolea(mboji/samadi) 150,000/-
Jumla 640,000/-
MAPATO:
Kilo 20,000 X300 =6,000,000/-

Saturday, December 5, 2009

MIHOGO - NJIA BORA ZA UKAUSHAJI NA USINDIKAJI

1. Mambo Muhimu Ya Kuzingatia Katika Utayarishaji Wa Mihogo
Mibichi Na Ukaushaji


1.1 UTAYARISHAJI
Mihogo mibichi iliyovunwa huoshwa mara mbili. Uoshaji wa kwanza ni ule wa kuondoa udongo baada ya kuvuna, na uoshaji wa pili ni baada ya kumenya mihogo kabla ya kukausha.Baada ya kuoshwa mihogo humenywa kwa kutumia kisu kikali, na kutumbukizwa ndani ya maji safi. Baada ya kumenya kiasi kinachotakiwa mihogo huoshwa na maji safi hadi kuwa myeupe.

1.2 UTENGENEZAJI WA CHIPSI

Mihogo iliyo safi huwekwa ndani ya mashine ya kuzungushwa kwa mikono au mashine ya kuzungushwa kwa mota ya umeme, kisha huparuliwa na kutoka vipande vidogo vidogo ambavyo huanikwa katika makaushio bora.



1.3 KWA MIHOGO MICHUNGU
Baada ya kuparuwa mihogo kuwa chipsi, huwekwa katika mifuko safi (viroba) na kuwekwa mahali penye kivuli kwa muda usiopungua saa sita ili kuacha sumu iliyoko kwenye mihogo kupotea kabla ya kukausha.

1.4 UKAUSHAJI

Mihogo safi ambayo imeparuliwa au kukatwa vipande vidogo vidogo hukaushwa katika makaushio bora kwenye jua kali. Makaushio bora huwa ni yale ambayo yamejengewa kichanja kilichoinuliwa mita mbili kutoka ardhini, na kutandazwa chekeche ya plastiki juu yake, yenye matundu madogo yasiyoweza kupitisha chembechembe za mihogo mikavu Kitambaa safi cha kaniki au mikeka safi huweza kutumika pia kama tandiko la juu ya kichanja ambapo chipsi za mihogo huweza kukaushwa kwa hali ya usafi.

VICHANJA BORA VYA KUKAUSHIA MIHOGO


Epuka kukaushia chipsi za mihogo katika majamvi mabovu juu ya ardhi kwani uchafu utakaoingia ndani ya mihogo hautakuwa rahisi kuondoa tena na husababishsa bidhaa ya unga kutokuwa na ubora.Ukaushaji duni wa mihogo Uharibifu au upotevu unaosababishwa na ukaushaji duni husababisha muhogo kubadilika rangi na kupata ukungu.

UKAUSHAJI DUNI WA MIHOGO


1.5 NJIA BORA ZA KUKAUSHA MIHOGO

Mihogo iliyoparuliwa (chipsi) hukaushwa na baadaye kusindikwa ilikupata unga.
VIFAA NA MALIGHAFI
• Mihogo safi
• Kisu kikali kisichoshika kutu.
• Mashine ya kuparua (grater)
• Kaushio bora
• Kitambaa cheusi kikubwa cha kutosha na kilicho safi au majamvi safi
• Vifungashio.

MASHINE YA KUPARUA MIHOGO(grater)



UTENGENEZAJI WA MAKOPA YA MIHOGO

• Menya mihogo safi kuondoa maganda
• Parua kwa kutumia mashine kupata chipsi.
• Anika kwenye kichanja au kaushio bora lilotandikwa kitambaa cheusi kilicho safi au jamvi safi ili kuzuia uchafu kuingia ndani ya chipsi.
• Sambaza na geuzageuza vipande hivyo ili kuharakisha ukaukaji.
• Muda wa kukausha hutegemea hali ya jua na ukubwa wa vipande. Vipande vidogo hukauka upesi na huwa bora kwa mlaji. Vipande vikubwa huchelewa kukauka na hupoteza ubora
• Fungasha vipande vilivyokaushwa kwenye magunia safi, kasha hifadhi kwenye maghala bora.

1.6 KUHIFADHI MIHOGO MIKAVU (Chipsi Au Makopa)
Njia pekee ya kuhifadhi mihogo kwa muda mrefu ni kwa kuhifadhi mihogo iliyokaushwa. Muhogo uliokaushwa huweza kuhifadhiwa kwa muda wa miezi 6 hadi 12 bila kuharibika. Makopa yanashambuliwa na dumuzi zaidi kuliko chipsi, hivyo inashauriwa kuhifadhi mihogo iliyoparuliwa na kukaushwa (chipsi) ambayo inakuwa katika hali ya unga unga na kufanya mashambulizi ya dumuzi yapungue kabisa.
Chipsi za mihogo zinaweza kuhifadhiwa katika magunia safi ya juti na kupangwa ndani ya ghala juu ya chaga. Pia chipsi zinaweza kuhifadhiwa katika hali ya kichele ndani ya sailo au kihenge bora. Mihogo haihifadhiwi kwa kutumia madawa ya viwandani. Hifadhi kwa hali ya ukavu, usafi na kagua ghala mara kwa mara kuona kama kuna mashambulizi ya panya na chukua tahadhari kuepuka upotevu wa chakula hicho. Aidha hifadhi kwa muda ulioshauriwa ili kudumisha ubora wa bidhaa.

2 KUSINDIKA MIHOGO ILIYOKAUSHWA

2.1 Kusindika muhogo uliokaushwa kupata unga
VIFAA
• Mashine ya kusaga
• Mifuko ya kufungasha
• Mashine ya kufungia mifuko
• Chekeche
• Mizani
• Muhogo safi uliokaushwa vizuri.

MASHINE YA KUSAGIA MIHOGO



JINSI YA KUSINDIKA
• Saga muhogo uliokaushwa kwenye mashine ili kupata unga.
• Chekecha kwa kutumia chekeche laini. Ukubwa wa matundu ya chekechekeche hutegemea kiwango cha ubora wa unga kinachotakiwa na soko.
• Weka unga kwenye mifuko kutegemea matakwa ya soko (kilo 1,2,5,10, au 50)
• Funga vyema kwenye mifuko ya kufungashia ili hewa isiingie
• Hifadhi kwenye chaga au fremu zilizowekwa mahali pakavu na pasipokuwa na mwanga mkali.

2.2 Viwango vya ubora wa unga wa muhogo uliokaushwa Unga laini
• Unga huu unapochekechwa kwa kutumia chekeche yenye matundu madogo
(milimita 0.60) hupenya karibu wote (asilimia 90)

Unga wenye ulaini kati
• Unga huu unapochekechwa kwa kutumia chekeche yenye matundu makubwa (milimita) 1.20) hupenya karibu wote (asilimia 90).

2.3 MATUMIZI YA UNGA WA MIHOGO
Hutumika kupika ugali, uji na katika kutengeneza maandazi, tambi, keki, biskuti,kababu, donati, mkate, chapati na chapati maji.


Virutubisho vinavyopatikana kwenye gramu 100 za unga wa muhogo ni kama ifuatavyo
Maji asilimia 13
Nguvu kilokalori 320
Protini gramu 1.7
Vitamini C miligramu 4
Kalsiamu miligramu 4
Fosiforasi miligramu 135
Potasiamu miligramu 885
W anga gramu 84
Madini ya chuma miligramu 2