KURASA

Friday, June 26, 2009

NAZI

MNAZI



Tumezoea kwamba siri ya umri mrefu ni maji, lakini si maji peke yake ila yaambatane na ulaji mzuri, leo nawaletea siri ya NAZI ambazo ni zao la mti wa mnazi (cocos nicifera) ambao uko katika jamii ya mipama (palms) inayojumuisha miti kama michikichi, mitende na mingineyo tuyoitumia kama mapambo

NAZI KABLA YA KUFULIWA MAGANDA


Mti wa mnazi au MTI WA UHAI kama ninavyouita ni mmea unaostawi na kupatikana kanda za pwani na sehemu zenye joto, mikoa kama Tanga, Dar, Pwani, Mtwara, Lindi, Mafia na Zanzibar hupatikana kwa wingi. Kila sehemu ya mti huu inatumika katika maisha ya kila siku ya mwanadamu, makuti kuezekea na kutengenezea mafagio, tunda lake ni chakula, maganda ya nazi kwa ajili ya kuzuia upotevu wa maji kwenye bustani/shambani (mulching) magogo hutoa mbao na hutumika kutengenezea mitumbwi, na sehemu yoyote ya mnazi huweza kutumika kwa ajili ya kupikia kuanzia makuti, mahanda, vifuuu n,k

NAZI BAADA YA KUFULIWA


Jamii za watu wanaotumia sana nazi huwa hazishambuliwi na magonjwa kama kisukari, presha ya kupanda na magonjwa mengine ya moyo na kiasi kikubwa cha lehemu (cholesterol) mwilini ukilinganisha na jamii zinazotumia vyakula vyenye kupikwa na mafuta yanayotokana na mimea mingine kama karanga, alizeti, ufuta, mahindi n.k. kwa mfano mikoa kama Tanga na Zanzibar ambako kwa wastani mtu hutumia kiasi cha nazi 120 kwa mwaka katika vifo 1000 vya watu wazima ni vifo 1 – 2 vinavyohusiana na magonjwa ya moyo wakati mikoa ambayo hawatumii nazi karibu robo ya vifo hutokana na magonjwa ya moyo.

MAHANDA YA NAZI



Kuna taarifa kwamba nazi huongeza kiasi cha lehemu mwilini je ni vipi? Ukweli ni kwamba nazi inayotumika moja kwa moja yaani inakunwa na kupikiwa hapo hapo haina madhara ya lehemu, ila nazi inayohifadhiwa ndio huwa na tatizo hili kwa sababu huchanganyika na hewa ya haidrojeni (hydrogenation) na kuwa sawa na yale mafuta mengine ya viwandani KWA HIYO nazi iliyohifadhiwa baada ya kukunwa au tui lililohifadhiwa huweza kusababisha kuongezeka lehemu mwilini

NAZI ILIYOVUNJWA


Moja kati ya vyakula vichache duniani ambavyo walaji hawana mzio (allergy) nacho ni nazi, pia inasifika kwa kupunguza kiasi cha sukari mwilini, maji ya dafu husafisha figo na kibofu

NAZI ILIYOKUNWA TAYARI KUTENGENEZEWA TUI


MAHANDA YA NAZI YAKIZUIA UPOTEVU WA MAJI KWENYE CHUNGU CHA MAUA

Saturday, June 20, 2009

MMBONO- JATROPHA (bio diesel)

1.0 UTANGULIZI
Mmbono kwa kitaalam Jatropha curcas ni mti jamii ya nyonyo wenye mbegu zitoazo mafuta yenye sifa kama nyonyo. Huota kwenye maeneo ya nyanda kame na yenye upungufu wa rutuba. Mmea hauliwi na mifugo wala wanyama pori na kufanya mmea ufae kulimwa kwenye maeneo ya wafugaji huria. Mmea hutoa mbegu zenye mafuta ambayo hayaliwi bali hutengenezea sabuni, kuendesha mitambo, gesi kama nishati. Kutokana na faida nyingi kwa binadamu kiafya, kiuchumi na mazingira, mmea unaweza kuzalishwa kama zao. Mmea huu umetokea Marekani ya Kati na kusambazwa hadi Afrika Mashariki na Wareno.

2.0 AINA
• Mmea ni wa jinsia moja (monoecious) na maua yake huwa ya jinsia moja.
• Mmea unaweza kudumu hata zaidi ya miaka 50.
• Kuna aina tatu za mmea ambapo aina moja iliyopo Mexico huliwa baada ya kukaangwa.
• Kwa sasa aina inayopo hapa Tanzania; Jatropha curcas haifai kuliwa bali kwa matumizi mengine.




3.0 MAZINGIRA:
Mmea huweza kustawi katika mvua za kuanzia 250mm hadi 2380, lakini uzalishaji mzuri huwa kwenye 625mm – 750mm. Kwenye sehemu zenye unyevu wa kutosha, mkulima atapata matunda wakati wote wa mwaka.Mmea hustawi kwenye nchi za Kitropiki na una tabia ya kustahimili ukame. Mmea hustawi kwenye udongo usiotuamisha maji, wenye tindikali kuanzia Ph 4.5. Mmea hupatikana kwenye mwinuko kuanzia mita 0 hadi mita 1600 juu ya usawa wa bahari ila hustawi vizuri kati ya mita 450-750 juu ya usawa wa bahari.

4.0 UTAYARISHAJI SHAMBA
Shamba litayarishwe mapema kwa kuchimba mashimo kabla ya mvua.

5.0 UTAYARISHAJI MBEGU/VIPANDIKIZI

Tumia mbegu zilizokomaa na kujaa vizuri. Mbegu zioteshwe katika vitalu ili kupata miche bora. Miche ikae kitaluni miezi 2 hadi 3. Kama utapanda moja kwa moja shambani, tumia kilo 5-6 kwa hekta. Au pandikiza vipandikizi vyenye urefu wa sm 45–100 katika shimo la sm 30. Mbegu huota kuanzia siku 9 na kutoa matunda baada ya miaka 3–4. Vipandikizi hutoa matunda kuanzia miezi 9 kutegemea na sehemu.

6.0 KUPANDA KWA NAFASI.

Panda mbegu 2 kwa shimo kwa kina cha sm 2 hadi sm3. Nafasi kati ya mche ni 2.5m x 2.5m.Nafasi kama hiyo hukupatia miti 1600 kwa hekta moja.Aidha nafasi ya 3mx3m itumiwe katika kilimo mchanganyiko wa mibono na mazao mengine.

7.0 PALIZI NA KUPUNGUZA MICHE
Punguzia miche baada ya wiki 4 na kubakiza mmoja, kutegemea na utayarishaji shamba. Palizi sio lazima ifanyike isipokuwa kama umefanya kilimo mchanganyiko palizi inaweza kufanyika kwa kuzunguka mmea au kufyeka magugu mara moja kwa mwaka. Kukata matawi kufanyike baada ya mwaka mmoja au miwili.

8.0 KUZUIA MAGONJWA NA WADUDU WAHARIBIFU
Hakikisha mimea haisongani na shamba ni safi. Mmea haushambuliwi na magonjwa ila wadudu jamii ya beetle, golden flea beetle wanashambulia majani. Athari ya mavuno hutokea endapo uharibifu katika majani utafikia zaidi ya asilimia 40. Mkulima afanye ukaguzi wa shamba lake mara kwa mara na kuwasiliana na wataalam wa kilimo kabla ya kupiga madawa.




9.0 UVUNAJI
Matunda yaliyokomaa tayari kwa kuvunwa huwa na rangi ya kahawia. Uvunaji hufanywa wa mikono au kwa kupiga kwa fimbo au kifaa maalum kilichotengenezwa kwa kutumia waya, mfuko wa pamba na fimbo ndefu, mbegu huguswa na kipande cha waya na kudondoka kwenye mfuko au kitambaa kilichowekwa chini ya mmea.Kiasi cha kuanzia gramu 300 hadi kilo 9 za mbegu zinaweza kuvunwa kwa mmea au tani 2 – 6 kwa mwaka kwa hekta. Mti unaweza kutoa mbegu mfululizo kwa mwaka kwa sehemu zenye unyevu au kuzaa mara mbili kwa msimu sehemu zenye ukame.

10.0 HIFADHI YA MAZAO
Baada ya kubangua mbegu kwenye matunda zikaushwe vizuri kabla ya kuhifadhiwa kwenye mifuko ya plastiki/magunia. Hifadhi mavuno kwenye sehemu kavu na dhibiti viumbe waharibifu kama panya.


11.0 MANUFAA YA MMEA

(1)Mbegu hutoa mafuta mengi yanayotengeneza sabuni na nishati ya kuwashia taa, jiko na gas, nchi nyingi hutumia mafuta haya kama diesel. Nishati hiyo mbadala hupunguza kasi ya matumizi ya kuni/mkaa na hivyo kuhifadhi mazingira.
• Zao linafaa katika maeneo ya nyanda kame yenye migogoro ya wafugaji na wakulima kwa vile mmea hauliwi na mifugo.
• Baada ya kusindika mbegu, mashudu hutoa mbolea ya komposti yenye ubora kama mbolea ya kuku.
• Uzalishaji wake una gharama ndogo ukilinganisha na mazao mengine
• Kama zao, wakulima wataongeza pato na kupunguza kasi ya magonjwa ya ngozi.
• Kuzuia mmomonyoko wa udongo kwa njia ya upepo na maji.





12.0 MASOKO
Mmea hutoa bidhaa kama mafuta, sabuni, gesis na mbolea zenye manufaa mengi kwa jamii. Hivyo wakulima wazalishe kwa wingi, wafanye mikataba na wasindikaji, wasafirishaji na wanunuzi wa mazao, kutumia mbinu za masoko na kupata mafunzo ya kutosha ili kutosheleza mahitaji ndani na nje ya maeneo ya uzalishaji

Kuna baadhi ya wanamapinduzi ya kilimo wanaupinga mmea huu, wakiamini kwamba kwa sababu mkulima anapata hela nyingi na kwa muda mfupi, basi wakulima wengi wataacha kupanda mazao ya chakula na badala yake watapanda mmea huu. matokeo yake ni kuwa uzalishaji wa chakula utapungua sana duniani na kusababisha njaa

Saturday, June 13, 2009

MAZIWA YA NGAMIA NA KISUKARI

AINA ZA KISUKARI
Aina ya kwanza ya kisukari ni pale mgonjwa anapohitaji kutumia insulin kila siku, aina hii huwa ni asilimia isiyozidi 10 ya wagonjwa wote wa kisukari, miili yao huzalisha insulin kidogo sana au haizalishi kabisa.Aina ya pili ni ile ambayo mwili mgonjwa wa mgonjwa huzalisha insulin lakini mwili unashindwa kuitumia na baada ya miaka kadhaa mwili hushindwa kuzalisha insulin na kusababisha aina ya kwanza ya kisukari


MDAU AKIMKAMUA NGAMIA


Maziwa ya ngamia yamekuwa yakisifika katika kuwasaidia wagonjwa wa kisukari aina ya kwanza kama watakunywa maziwa haya kiasi cha nusu lita kwa siku. Kwa kawaida mgonjwa wa kisukari aina ya kwanza huitaji kiasi cha ankara 20 za insulin kwa siku lakini akitumia maziwa haya huitaji kiasi cha ankara 6 – 7 za insulin kwa siku.



Huko india katika jimbo la Rajasthan kuna jamii/ kabila linayoitwa Raica ambalo husifika kwa ufugaji wa ngamia, jamii hii husifika kwa kutokuwa na wagonjwa wa kisukari isipokuwa kati ya wale wachache ambao huwa hawatumii kabisa maziwa ya ngamia




Maziwa ya ngamia pia husifika kwa kusaidia wagonjwa wa shinikizo la juu la moyo, pia husaidia katika kupambana na vimelea kama virusi na bakteria. Kwa mfano mgonjwa wa kifua kikuu anayaetumia dawa na maziwa ya ngamia hupata nafuu haraka zaidi ya yule asiyetumia maziwa ya ngamia

Sunday, June 7, 2009

UTUPA - DAWA YA KUULIA WADUDU

Huu ni mmea unaopatikana zaidi sehemu zenye baridi na nyanda za juu na unastawi sehemu zenye mvua za wastani na nyingi, huwa hauhimili ukame. Ni mmea unaokua haraka na kusambaa kama usipodhibitiwa, baadhi ya nchi umepigwa marufuku kupanda kwa sababu ya kutishia uoto wa asili



MATUMIZI
KUFUKUZA PANYA / MCHWA

Kama shamba lako limevamiwa na panya wanaochimba ardhini, panda huu mmea pamoja na mazao mengine kwa umbali wa mita 3 kila upande (3m * 3m) na mpakani mwa shamba lako, baada ya mwaka mmoja shaba halitakuwa na mashimo ya panya. kwa njia hii hii pia utafanikiwa kufukuza mchwa, kwenye majumba unaweza kuupanda kwenye kingo za nyumba na mpakani, kama kuna kichuguu cha mchwa panda miche hii na kichuguu kitakufa baada ya mchwa kuhama.

KUOGESHEA MIFUGO
Chukua kiasi cha kilo moja ya majani ya utupa na maji lita 25 loweka kwa masaa mawili (2) mpaka matatu (3) au chemsha kwa dakika 30 na lita 27 za maji, chuja kwa kitambaa kisha weka kwenye bomba lakuogeshea changanya na sabuni ya unga kidogo ili iweze kunata kwenye mwili wa mnyama wako na hapo inakuwa tayari kwa matumizi ONYO usitumie kuogeshea nguruwe hawana uwezo wa kuhimili dawa hii kwenye ngozi zao




KUNYUZIA SHAMBANI / BUSTANI
Chukua kiasi cha kilo moja ya majani ya utupa na maji lita 5 loweka kwa masaa mawili (2) mpaka matatu (3) au chemsha kwa dakika 30 na lita 6 za maji, chuja kwa kitambaa kisha weka kwenye bomba na uanze kunyunyuzia shambani au majumbani kwa minajili ya kuua wadudu kama mbu, mende, n.k

KUHIFADHI NAFAKA KWENYE GHALA
Chukua gram 100 za unga wa majani ya utupa changanya na mahindi au maharage kilo 100, funga vizuri gunia lako na hifadhi kwenye ghala. Dawa hii huwa na nguvu kwa muda wa mwaka mzima.

MBEGU ZA UTUPA



MATUMIZI MENGINE
Mmea huu ukipandwa mchanganyiko na mazao mengine huongeza rutuba ardhini kwa kuongeza kiasi na naitrojeni, mbegu zake hutumika kama chanzo cha protini kwenye ufugaji wa mbuzi ila zisiliwe nyingi kwani ni sumu, Unga wa mbegu zake unauwezo wa kusababisha samaki wapooze (paralyze)unga wa utupa gram 1 na maji lita 2.5 hutumika kama dawa ya minyoo kwenye ngombe na mbuzi kwa kiwango cha 1cc kwa kilo 10 za mnyama,

Wednesday, June 3, 2009

UJENZI WA BARABARA KISARAWE MPAKA KAZIMZUMBWI




Jumatatu nilikuwa nimeenda Kisarawe maeneo ya visegese (SHAMBA) ndio nikakutana na huu ujenzi wa barabara ambao uko katika hatua za matayarisho. Nilipoongea na wahusika wa kampuni ya ujenzi ya SKYLINK waliniambia barabara hiyo ya lami itakwenda mpaka maeneo ya kijiji cha Kazimzumbwi ambako kunatarajiwa kujengwa kiwanda kipya cha saruji.

UPIMAJI UNAENDELEA


Ujenzi huu utakuwa faraja kwa wakazi wa kazimzumbwi na sisi wakulima wenye mashamba maeneo karibu na hayo, kwa mfano mimi kutoka Kisarawe mjini ambapo lami ilikuwa ndio mwisho wake nilikuwa naendesha kilometa 8 kwenye barabara ya vumbi, kwa sasa nitabakiwa na kilometa zisizozidi 2 kutokea Mpuyani ambapo huwa nachepuka kwenda kwenye barabara inayoelekea Kilvya.


VIJIKO KAZINI






Kiwanda cha saruji pia ni faraja kwa taifa kwani bidhaa hiyo imekuwa ni muhimu sana katika maendeleo ya nchi kwa ujumla, wananchi wataajiriwa kama wafanyakazi na vibarua na hivyo kuongeza ajira, serekali kwa upande wake itanufaika na kodi ya mapato kutoka katika kiwanda hicho

KAMBI YA UJENZI