KURASA

Wednesday, August 22, 2012

NG'OMBE ALIYE KWENYE JOTO - JINSI YA KUMTAMBUA

Kwa kawaida ng'ombe jike aliyebalehe huingia kwenye joto kila baada ya siku 14 - 24 au wastani wa siku 21 kama hatapandwa na kushika mimba, hii hutegemea na aina ya ng'ombe, mazingira, lishe na hali ya hewa. kuna masaa kati ya 6 - 10 kabla hajaingia vizuri kwenye joto (pre heat) na joto lenyewe huchukua kati ya masaa 4 - 30 pia kutegemeana na aina ya ng'ombe, mazingira, lishe na hali ya hewa na yai hupevuka kwa wastani wa masaa 10 - 12 baadae

Kama utataka kumpandisha ng'ombe jike wako kwa kutumia madume bora ya kuazima au kwa kutumia  kupandisha kwa njia ya chupa, basi ni muhimu kuzijua dalili kuu ambazo huonekana ng'ombe jike anapokuwa kwenye joto, dalili hizi zinaweza kuonekana kabla ya joto, wakati wa joto ana hata baada ja joto kupita kidogo, kwa hiyo ni muhimu kuzitambua mara zinapoanza ili usiweze kupitiliza na kulikosa joto halisi

DALILI KUU

  1. Sehemu ya nje ya kizazi/uke huwa kubwa zaidi kama imeumuka na kutuna zaidi ya ile saizi yake ya kawaida.
  2. Sehemu ya nje ya kizazi/uke huwa na rangi nyekundu inayoelekea kukooza zaidi ya kawaida yake.
  3. Ute ute hutoka kwenye kizazi na huwa mzito wenye kunata nata.
  4. Ng'ombe huwa hatulii, mwenye kuzunguka zunguka na hata kulia lia zaidi ya kawaida yake.
  5. Ingawa ni jike lakini pia hujaribu kuyapanda majike mengine yaliyopo bandani, kana kuna mabanda mengine zaidi, ukimuhamisha hali hii ya kuwapanda wenzie hizi.
  6. Hunyanyua nyanyua mkia na kwenye ncha mkia huwa imevurugika (rough)
  7. Ukimgandamiza mgongoni kwa kutumia mikono sehemu ya nyuma kabisa karibu na mkia hutulia na kusikilizia kama anapandwa, mwanzo hatatulia ila ukifikia wakati sahihi atatulia na hapo ndipo unapoweza kumuwekea mbegu kwa njia ya chupa na kama unatumia dume lenyewe litatambua hali hii kwa hiyo ukiona dalili tu zinaanza mpeleke kwa dume na lenyewe litapanda kwa wakati sahihi.