KURASA

Tuesday, September 15, 2015

KILIMO BORA CHA MTAMA

Mtama ni kundi la mbegu ndogo aina ya mazao ya nafaka au nafaka ambayo kwa jina la kisayansi unajulikana kama (Sorghum bicolor), ni mazao yanayolimwa sana duniani kote kwa ajili ya chakula na lishe Mtama hutoa mazao mengi hata kwenye hali ambayo haifai kwa kilimo cha aina nyingine za mazao ya nafaka. Mtama una uwezo mkubwa wa kustahimili ukame.

Mtama unaweza kutumika kwa kuchemshwa na kuliwa kama ulivyo, kusagwa na kutumika kwa uji, kutengenezea vinywaji kama vile bia, kuoka mikate, na aina nyinginezo za vitafunwa. Mmea wa mtama pia hutumika kwa ajili ya malisho ya mifugo kama vile hay  na sileji. Mtama unastawis vizuri kwenye mazingira yenye wastani wa milimita 400 – 700 za mvua kwa mwaka. Pia mtama unavumilia sehemu zinazotuhamisha maji, na unaweza kulimwa sehemu zenye mvua nyingi.

Mtaama unafaa pia kwa sehemu kame zenye wastani wa joto la chini kiasi cha nyuzi joto 18°C, ili kuweza kuota vizuri, na kiasi cha nyuzi joto 25-30°C ili kukua vizuri. Mtama hauwezi kuvumilia barafu. Mtama unaweza kukua kwenye aina zote za udongo. Kwa kiasi kikubwa unafaa zaidi kwenye udongo wa mfinyanzi, lakini pia kwenye udongo ambao una kiasi kidogo cha mchanganyiko wa kichanga. Mtama unaweza kuvumilia uchachu kwenye udongo kuanzia pH 5.0-8.5, na inavumilia udongo wenye chumvi kuliko yalivyo mahindi.

Aina za mtama

Kwa jumla kuna aina zaidi ya 30 za mtama zinazolimwa kama chakula. Mtama hustawi vizuri kwenye joto ikivumilia pia ukame. Hivyo ni nafaka muhimi kwenye maeneo yabisi za Afrika. Katika miaka ya nyuma kilimo chake kiliachwa mara nyingi kwa ajili ya mahindi kwa sababu mahindi huleta mazao makubwa zaidi kwa ekari. Lakini wakati wa ukame mahindi ni hasara na watu hurudi-rudi kwenye kilimo cha mtama.

Aina za mtama zinatofautiana kulingana na rangi zake, kuna nyeupe, nyekundu, na kahawia. Mbegu za asili huwa zinachavushwa kwa urahisi zaidi lakini mavuno yake huwa ni hafifu ukilinganisha na mbegu za kisasa. Hata hivyo, aina za kisasa zinazalishwa kwa gharama nafuu zaidi zinapopandwa kwa kufuata kanuni za kilimo bora.

Serena:  Ina punje za kahawia. Aina hii hustawi kwenye eneo lenye mvua za wastani na hukomaa katika kipindi cha siku 110. Aina hii huwa na shina na mizizi imara, ambapo huweza kuzalisha kiasi cha kilo 3,000 kwa hekari moja. Ambapo zinahitajika kilo 5 za mbegu kwa hekari moja. Aina hii ina uwezo wa kukabiliana na ugonjwa milia, kutu, na madoa ya kahawia kwenye majani.

Seredo:  Hii ni aina nyingine yenye punje za kahawia, na inapendekezwa Kulimwa kwenye eneo lenye mwinuko wa mita 1,500 kutoka usawa wa bahari. Aina hii huchanua baada ya siku 71 na hukomaa katika kipindi cha siku 120. Aina hii huwa ni ndefu, na ina uwezo wa kuzalisha kilo 5000 kwa hekari moja. Ina uwezo wa kukabiliana na ugonjwa wa milia, kutu, mabaka kwenye majani, na madoa ya kahawia kwenye majani.

Gadam: Inafanya vizuri katika sehemu ambazo si kame sana. Katika nchi nyingi mfano Kenya, aina hii ya mtama hutumika kutengenezea bia na pia kwa chakula. Aina hii huvumilia bungo na ugonjwa wa majani.

Hakika na Wahi:  Hizi ni aina mbili za mtama ambazo zimezalishwa na kituo cha Utafiti wa Kilimo cha Ilonga kwa ajili ya kuoteshwa kwenye mashamba yalioathiriwa na viduha. Mbegu hizi zina rangi ya manjano iliyopauka. Unga wa aina zote mbili zinafaa sana kwa kupika ugali.

Utayarishaji wa shamba na kupanda

Kwa kawaida mtama hupandwa kwa kutumia mbegu. Mbegu hupandwa shambani moja kwa moja baada ya shamba kuandaliwa, lakini pia zinaweza kurushwa shambani, kasha zikavurugwa pamoja na udongo. Unapaswa kutayarisha shamba la kupanda mtama, iwe ni kwa ajili ya malisho au chakula kabla mvua za msimu hazijaanza. Zao hili hufanya vizuri zaidi kwenye udongo ulio laini. Linaweza pia kupandwa kwenye udongo ambao haukulimwa vizuri na bado ukaota vizuri.

Nafasi:  Mtama unaopandwa kwa ajili ya malisho, unaweza kupandwa kwa nafasi ya sentimita 75×10. Aina za mtama ambazo zinalengwa kwa ajili ya lishe kwa binadamu na wanyama, zinahitaji nafasi kiasi cha sentimita 60×20. Nafasi hutoa mwanya wa kuwa na kiwango kikubwa cha malisho. Mkulima anaweza kupanda mbegu za mtama kiasi cha kilo 2.4-3.3 kwa hekari moja. Ni mara chache sana mbegu hupandwa kwenye vitalu na kuhamishiwa shambani baadaye.

Kupanda:  Mtama hupandwa mvua zinapoanza kunyesha. Mbegu ni lazima zifukiwe ardhini usawa wa sentimita 3 kwenda chini, hii itasaidia kuepuka kuota wakati ambao si msimu kamili wa mvua. Pia zinaweza kufukiwa kiasi cha sentimita 2 wakati ardhi inapokuwa na unyevu. Mtama unahitaji rutuba ya hali ya juu wakati wa kupanda na wakati wa kuota. Ni vizuri kutumia samadi au mboji iliyooza vizuri wakati wa kuandaa shamba.

Mseto:  Unaweza kupanda mtama mseto na mazao jamii ya mikunde, na kuongeza mboji shambani mwako. Hii inaweza kuwa njia nzuri zaidi ya kupata virutubisho vinavyohitajika. Mseto wa mazao jamii ya mikunde inashauriwa iwe ni kama vile maharagwe, kunde, n.k

Uangalizi na utunzaji
Ni lazima kung’oa baadhi ya mimea inapokuwa na urefu wa sentimita 30, au siku 30 baada ya kupanda, ili kuwa na uhakika wa nafasi ya sentimita 10 kati ya mstari na mstari kwa mtama unaokusudiwa kwa ajili ya malisho, na nafasi ya sentimita 20 kati ya mstari kwa mtama uliokusudiwa kwa ajili ya chakula na lishe ya mifugo.

Palizi ya mkono ifanyike walau mara mbili. Shamba la mtama ni lazima liwekwe katika hali ya usafi na kutokuruhusu magugu wakati wote hasa katika kipindi cha mwanzoni.