KURASA

Monday, December 19, 2011

MGOGORO WA KILIMO CHA MAHINDI MKOANI SINGIDA




Umeibuka mgogoro mkoani Singida mara baada ya mkuu wa mkoa Dr.Parseko Kone kupiga marufuku kilimo cha mahindi mkoani humo. Mmoja wa waliopinga mpango huo ni Mheshimiwa Salome Mwambu mbunge wa Iramba mashariki kwa tiketi ya CCM.

Akitetea kilimo cha mahindi MH Mwambu alisema kwamba hilo silo tamko la mkoa kwa sababu hakuna hata kiongozi mmoja wa mkoa au wilaya ambaye alijaribu kuwashirikisha wananchi kwenye mchakato huo

Pia alisema kwamba kilimo cha mahindi kilikuwepo kwa miaka mingi mkoani humo na zao hilo likiwa ni la biashara na chakula kwa wananchi wenyewe



MAONI YANGU

Viongozi wote wawili walikuwa na nia njema sana kwa wananchi wa Singida, mkuu wa mkoa alikuwa anajitahidi kukabiliana na njaa mkoani mwake na ndio maana akawa anasisitiza kilimo cha mazao ya kinga ya njaa,ambayo ni yale yanayohimili ukame na uhaba wa mvua kama mtama, ufuta na uwele n.k

Mh mbunge naye alikuwa akiwatetea wananchi wake kwa sababu ndio wapigakura wake na yeye ndiye mwakilishi wao, akiangalia anaona kwamba miaka mingi watu wamekuwa wakitegemea mahindi kama zao la chakula na biashara, ndio maana akashauri kwamba watu wasikatazwe kulima mahindi bali walazimishe kupanda na mazao ya kinga ya njaa

Kwa ujumla wote wamefanya maamuzi bila ya kuwashirikisha wataalamu wa kilimo na hali ya hewa, kila mtu alikuwa anatetea kibarua chake. kama wange washirikisha wataalamu basi nina imani kwamba mabo yangekuwa mazuri.

Mkoa wa Singida ni moja ya mikoa inayopata mvua moja kubwa kwa mwaka, na hali yake ni ya ukame kiasi ingawa mvua zinaweza kuwa kubwa zikiambatana na upepo ambao pia huleta madhara kama ya kuharibu mazao na makazi ya watu, mabadiliko tabia nchi yamesababisha kuwe na mvua zisizotabirika na tume shuhudia mara kadhaa zikiwa chini ya kiwango. mkoa huu pia umeathirika na ukataji miti kwa ajili ya kuni, mkaa na matumizi mengine, na pia ufugaji uliokithiri umesababisha uharibifu wa udongo na kusababisha mmong'onyoko wa udongo kwenye baadhi ya sehemu. kwa sababu hizi na nyinginezo zote kwa pamoja zimesababisha madhara kwenye mfumo wa kilimo uliozoeleka na wenyeji wa mkoa huu.



USHAURI
1 - Wakulima walime mahindi kwenye sehemu zilizo tambarare na kwenye mabonde ambako unyevu unachelewa kukauka na wasilime mahindi kwenye uwanda wa juu na milimani kwani sehemu hizo ndizo zinafaa kwa mazao ya kinga ya njaa

2 - Matumizi ya kanuni za kilimo kilimo bora yazingatiwe kama kutumia mbegu bora za mahindi zinazokomaa muda mfupi za zinazoendana na hali ya hewa ya Singida, matumizi ya mbolea za samadi, viuatilifu salama n.k

3 - Upandaji wa mbegu kwa wakati, na kwa kufuata majira ya hali ya hewa, hii ni baada ya kufuata ushauri wa watabiri wa hali ya hewa, hili la hali ya hewa lifanywe na Mbunge akishirikiana na Mkuu wa Mkoa, yaani wafuatilie na wawaeleze wakulima muda sahii wa kuandaa mashamba na kuanza kupanda (wasilete siasa hapa)

4 - Viongozi wa siasa wakae na wakulima/maafisa kilimo na kushauriana nao kuhusu kilimo kwa ujumla, ikiwezekana wasaidie kuanzia upatikanaji wa mbegu bora watakazozichagua kwa pamoja, madawa ya kuua wadudu na taarifa za wadudu au magonjwa ya mazao ili kuzuia kusambaa (wanasiasa wasikae maofisini sana ila watembee kwenye himaya zao kujua matatizo)

Saturday, December 17, 2011

SAMAKI WA MAPAMBO TOKA TANZANIA - (Ornamental Fish From Tanzania)

Tanzania imejaliwa kuwa na aina mbalimbali za samaki wa mapambo wanaopatikana katika maji baridi na maji chumvi. Samaki hawa hupatikana kwa wingi katika maji ya asili na baadhi yao hupatikana humu nchini tu. Kuna samaki wa mapambo ambao wapo katika hatari ya kutoweka. Kwa kiasi kikubwa samaki wa mapambo, wamekuwa wakivuliwa na kupelekwa nje ya nchi na wafanyabiashara.

HALI YA BIASHARA YA SAMAKI WA MAPAMBO
Samaki wengi wa mapambo kwenye maji baridi ni jamii ya Cichlids. Ziwa
Tanganyika lina spishi zaidi ya 200 lakini wanaosafirishwa nje ya nchi kwa ajili ya mapambo ni wastani wa spishi 30 Ziwa Nyasa lina spishi zaidi ya 750 lakini wanaosafirishwa nje ya nchi kama samaki wa mapambo ni takriban spishi 5 ambazo ni Aulo mamelela, A. blue neon, A. hongi, Proto steven na Tropheus ndole. Ziwa Victoria lilikuwa na spishi zaidi ya 300 katika miaka ya 1970 kabla samaki aina ya Sangara aliyepandikizwa hajasambaa na kula jamii ya Cichlid. Hivi sasa baadhi ya spishi zimetoweka na biashara ya samaki wa mapambo haipo Ziwa Victoria.

CICHLIDS TOKA ZIWA TANGANYIKA


Kwa upande wa samaki wa maji chumvi wanaoishi kwenye matumbawe (coral fish species), spishi zilizopo Tanzania ni nyingi lakini idadi kamili haijulikani. Hata hivyo, kati ya spishi takriban 4,000 zilizopo duniani ni spishi 200 – 300 ndio wanaotumika kwa mapambo.
Samaki aina ya “Cichilid” hutumika sana kwa mapambo duniani kote kwa kuwa wana uwezo wa kuzoea mazingira mapya kwa haraka kuliko samaki wengine (Koning, 1995). Hii inatokana na tabia yao ya kuwa na uwezo mkubwa wa kuvumilia hali tofauti ya mazingira ya maji ikiwemo pH na uchumvi chumvi (salinity). Pia, wana tabia ya kula aina mbalimbali za vyakula kutokana na mpangilio wa midomo, meno na taya (Pharyngeal jaws). Kuna wanaokula mwani (algae), mimea (plants), samaki, konokono n.k. Pia, aina hizi za samaki wanaweza kuishi na kusafirishwa kwa muda wa siku tano (5) bila kula alimradi mazingira ya maji yanaruhusu na vifo vinaweza kuwa chini ya asilimia 2 tu wakati wa kuwasafirisha.




Takwimu za biashara ya samaki wa mapambo duniani sio sahihi sehemu nyingi. Hata hivyo takwimu zilizopo zinaonyesha kuwa Uingereza mwaka 1987 waliuza samaki wa kiasi cha Paundi za Uingereza milioni 17 na Marekani waliuza samaki wa thamani ya Dola za Kimarekani milioni 739 mwaka 1988. Hata hivyo taarifa zilizopo zinaonyesha kuwa tabia ya kupenda (hobby) kufuga samaki wa mapambo inaongezeka kwenye nchi mbalimbali zikijumuisha, Japan, China, Australia, Afrika ya Kusini, Korea, Ujerumani na Malaysia. Mara nyingi ufugaji hufanyika kwenye mabwawa na matanki (aquarium).

Kwa upande wa Tanzania, takwimu za biashara ya samaki wa mapambo kutoka kwenye maji baridi kuanzia mwaka 2006 mpaka mwaka 2009 ni kama ifuatavyo: Kwa ujumla biashara ya samaki hawa huingizia Serikali pesa kidogo sana. Samaki wengi waliosafirishwa nje ya nchi katika mwaka 2006 walitoka Ziwa Nyasa. Jumla ya samaki 12,661 ambao walikuwa na thamani ya shilingi 100 87,143,451.25 waliingizia Serikali ushuru wa shilingi 6,541,825.56 tu. Jumla ya samaki 9,080 kutoka Ziwa Tanganyika waliokuwa na thamani ya shilingi 58,770,742.7 waliingizia Serikali kiasi cha shilingi 4,292,456.39. Mwaka
2009 samaki wengi walitoka Ziwa Tanganyika jumla ya samaki 23,500 wenye thamani ya shilingi 131, 356,148.5 waliingizia Serikali jumla ya shilingi 13,018,338.19 kama ushuru. Samaki kutoka Ziwa Victoria walisafirishwa wachache tu mwaka 2007, walikuwa 12 tu. Samaki wa mapambo kutoka Ziwa Victoria wako hatarini kutoweka kutokana na kuliwa na Sangara kwa hiyo wameingizwa kwenye “Red list” chini ya CITES,
hawasafirishwi tena. Kinachohimizwa ni ufugaji wa hao samaki.




FURSA YA UWEKEZAJI KATIKA SAMAKI WA MAPAMBO

i) Kuna fursa kubwa ya uwekezaji katika samaki wa mapambo wa Ziwa Tanganyika kwa kuwa samaki hao wapo wengi (Watson, 2000) na baharini kwenye matumbawe (Coral reef fish species)

ii) Kuwepo kwa masoko ya uhakika na mazingira mazuri ya kuvutia biashara Ili uendeleza na kuimarisha uwekezaji katika eneo hili ni muhimu kuhamasisha wananchi na wawekezaji kutoka nje katika kuwekeza kwenye biashara ya samaki wa mapambo. Pia, ni lazima kufanya utafiti wa kufahamu spishi zilizopo na wingi wa samaki wa mapambo ili kuepuka kumaliza baadhi ya samaki hao.

UMUHIMU WA BIASHARA YA SAMAKI WA MAPAMBO KATIKA KUONDOA UMASIKINI

Takwimu zilizopo zinaonyesha kuwa mapato ya biashara ya samaki wa mapambo kwenye nchi mbalimbali duniani ina thamani ya takriban Dola za Marekani milioni 186 na samaki wengi wanatoka nchi zinazoendelea (Watson, 2000). Kati ya hizi fedha Zinazobaki kwa jamii wanaokusanya samaki hao ni kidogo sana. Hata hivyo, kama jamii itawezeshwa kupata mtaji na teknolojia sahihi itaweza kujiongezea kipato na kupunguza umaskini. Asilimia 90 ya samaki wa mapambo duniani huzalishwa kwenye mabwawa hasa kwenye nchi zilizoendelea na samaki hao wametolewa kutoka kwenye nchi zinazoendelea ikiwemo Tanzania. Ili mwananchi aweze kunufaika na biashara ya samaki wa mapambo kuna umuhimu wa kuwaelimishwa kuhusu njia bora za kuwavua, kuwahifadhi na kuwasafirisha kwa ajili ya kuongeza kipato chao na taifa kwa ujumla.

SAMAKI WA UREMBO TOKA ZIWA NYASA

ATHARI ZITOKANAZO NA BIASHARA YA SAMAKI WA MAPAMBO

Shirika la Kimataifa la Hifadhi ya Viumbe na Mazingira kupitia kitabu cha “Red List’’ (IUCN, 1988) kimeainisha aina za samaki wa mapambo ambao wapo hatarini Kutoweka. Samaki hao ni pamoja na aina ya furu (Haplochromine). Athari za biashara hiyo ni kama ifuatavyo:

i) Kupungua wingi na makazi ya samaki waliopo kwenye maeneo ya asili ikiwa ni pamoja na maziwa, mito na bahari kwa njia mbalimbali. Hali ya aina hii imekwishatokea kwenye nchi ambazo biashara ya samaki wa mapambo ni kubwa kama vile Sri Lanka na Malaysia (Banister, 1989). Kwa upande wa Tanzania tathmini ya athari za biashara ya mapambo bado haijafanyika.

ii) Kuharibika kwa mfumo mzima wa ikolojia na kuharibu makazi ya samaki asilia (indigenous species). Hali hii hutokana na samaki wa mapambo kupelekwa kwenye maeneo ambayo sio ya asili yao kama vile mabwawa. Wakati mwingine samaki hawa huingia kwenye mito iliyo karibu na mabwawa wanayofugiwa na kwenda kwenye maziwa ambako
huchanganyika na samaki ambao ni wa asili kwenye maeneo hayo. Pia, biashara hii inaweza kuhatarisha ikolojia ya maji ya nchi waliyopelekwa.

CHANGAMOTO
i) Kuimarisha na kuendeleza miundombinu kwenye maeneo yenye vivutio kwa ajili ya utalii ikolojia ikiwa ni pamoja na barabara, umeme na maji safi;

ii) Upatikanaji wa mitaji na uwekezaji katika utalii ikolojia na biashara ya samaki wa mapambo;

iii) Kuweka bayana umiliki wa fukwe za bahari ambazo ziko nje ya Hifadhi za Bahari na Maeneo Tengefu ili kuharakisha uwekezaji wa maeneo haya kwa nia ya kukuza utalii ikolojia;

iv) Kufanya utafiti wa kufahamu ikolojia, aina, wingi wa samaki wa mapambo n.k.;

v) Kuboresha mazingira ya utalii ikolojia na biashara ya samaki wa mapambo.

MAPENDEKEZO YANGU
i) Kufanya utafiti wa kufahamu wingi wa spishi mbalimbali za samaki wa mapambo ili uvunaji uwe endelevu;

ii) Kuhamasisha wananchi na wadau wengine kuwekeza katika biashara ya samaki wa mapambo na utalii ikolojia;

iii) Kuhamasisha wananchi kutembelea Hifadhi za Bahari na Maeneo Tengefu ili kukuza utalii wa ndani; na

iv) Kufanya jitihada za kuhifadhi spishi za viumbe wa kwenye maji zilizo hatarini kutoweka.

Wednesday, November 23, 2011

MAGONJWA MAKUU YA NDEGE

Magonjwa huainishwa kulingana na baiolojia yao,kama Virusi,Bakteria,Kupe,ukungu,na chanzo chao,kwa mfano magonjwa ya lishe yaliyoangaliwa hapo juu.Hata hivyo,magonjwa makuu katika ndege yamegawanywa katika makundi matatu kulingana na makali yao na umuhimu katika mfumo wa uzalishhaji mdogo katika vijiji.Vitu muhimu kama tabia zao wakati wa mlipuko(dalili),na matibabu yanayowezekana(kuzuia ama kudhibiti)vile vile wakati wa kutokea magonjwa hayo.Umuhimu wa ugonjwa huthaminiwa na idadi ya vifo na athari kwa uzalishaji,na itatofautiana kutoka eneo hadi eneo na msimu hadi msimu.

MCHANGANYIKO WA MAGONJWA

Magonjwa kadhaa yasiyo maku yanaweza kukutana na magonjwa mengine na kusababisha madhara makali kwa ndege.Hii ndio hali kwa mfano maambukizo ya E.coli, utapiamlo na kupe wa ndani.Magonjwa kama haya ni vigumu kuua ndege lakini huwa na madhara makubwa kwa kinga ya ndege dhidi ya magonjwa,na kujenga msingi wa maambukizo rahisi ya magonjwa mengine baada ya kuwafanya ndege kuwa dhaifu kiafya.

Umuhimu mkubwa huashiria ugonjwa wa kawaida wenye vifo vingi(zaidi ya asilimia 30 ya kundi),husambaa kwa urahisi na ni vigumu kutibu au hautibiki kabisa.Umuhimu wa wastaani kawaida ,vifo vya wastani(10-30%) kwa kundi na /ama vigumu kutibu.Ugonjwa usio mkuu huashiria wa kawaida, vifo vichache na /ama rahisi kutibu.

UGONJWA WA KUAMBUKIZANA WA KUKU UNAOSHAMBULIA MAPAFU NA MFUMO WA NEVA - NEWCASTLE DISEASE (NCD)
Ugonjwa huu huua, ni wa kawaida katika msimu wa mvua,na hutokea mara kwa mara katika vifaranga wachanga,lakini pia katika kuku waliokomaa.Vifo vya juu katika kundi,mara kwa mara baina ya aslimia 30 na asilimia 80 ya ndege hufa,ugonjwa unapowakumbaKuku hupoteza hamu ya kula na usagaji mbaya wa chakula tumboni.Unaweza kuonyesha upumuaji mzito,kinyesi cha kijani na wakati mwingine kuhara damu. Unaweza kuonyesha dalili za kuchanganyikiwa,kiharusi na hufa ghafla.Dalili zinaweza kutokea zote wakati mmoja.Ugonjwa huu ni wa virusi (virus)kwa hivyo hauna tiba,lakini unaweza kuzuiwa kwa kuwachanja ndege wote ukijumuisha vifaranga wa kutoka wiki mbili.

HOMA YA NDEGE - AVIAN INFLUENZA(AI)

Ugonjwa huu hubebwa na bata na bata maji,na unaweza kusambaa kwa urahisi na ni hatari sana kwa kuku.Vifo vya juu katika kundi,ndevu na panga za jogoo huvimba na kuwa na rangi ya kibuluu (samawati).Husambaa kupitia chakula na maji yaliyochafuliwa katika madimbwi na vyombo vya maji/chakula.Ugonjwa huu husababishwa na virusi (virus),kwa hivyo hauna tiba.

Ili kujikinga na ugonjwa huu zingatia usafi kwenye banda lako na vyombo vya kuku, ukiona dalili za ugonjwa huu waondoe kuku wagonjwa, wachinjwe na kuchomwa moto. Kabla ya kuingiza kundi lingine la kuku kwenye banda lenye ugonjwa hakikisha unapulizia dawa za kuua virusi ka a VIRU KILL. Mara uonapo dalili za ugonjwa huu muite afisa ugani wa mifugo (Veterinarian)

NDUI YA KUKU - FOWL POX

Huonekana mara kwa mara katika vifaranga wadogo,lakini pia kwenye kuku waliokomaa na huonekana uvimbe mdogo mdogo kwenye ndevu,panga na uso wa kuku.joto la kuku hupanda,uchovu unaoambatana na vifo vya ghafla.Ugonjwa huu ni wa kawaida wakati wa msimu wa kiangazi,lakini pia unaweza kutokea mwaka mzima.Ugonjwa huu ni virusi kwa hivyo hauna tiba.Chanjo inapatikana kwenye maduka ya pembejeo za kilimo.

UGONJWA WA MAREK - MAREK DISEASE

Huonekana tu katika ndege walio na zaidi ya wiki 16 kwa hiyo hauwapati kuku wa nyama labda kama umewafuga kwa ajili ya uzalishaji (parent stock).Mwanzoni ndege wanaweza kuonyesha bawa moja kushuka au yote mawili.Ama mguu mmoja ama yote inaweza kupooza.Ugonjwa huu ni virusi,kwa hivyo hauna tiba,lakini Chanjo inapatikana kwenye maduka ya pembejeo za kilimo

MAAMBUKIZO YA BAKTERIA WA E.coli

Hutokea sana sana katika vifaranga walioanguliwa (Day old chicks),na husababisha maambukizo katika tumbo.Dalili katika ndege wakubwa:kupumua kwa tabu au maambukizo katika mayai na kupungua au kuacha kabisa kwa utagaji kwa kuku wa mayai, kinga bora ni usafi katika mayai kwa ajili ya .Tiba kwa vifaranga wagonjwa inawezekana ukiwa na kiua vijisumu (antibiotics) kama OTC 10%, 20%, 30%.

KIPINDUPINDU CHA KUKU - pasteurellosis

Unaweza kutokea wakati wowote na kwa rika zote.Dalili ni kuharisha sana kwa kuku,kupumua kwa tabu,kukosa hamu ya kula,ndevu na panga za jogoo huwa na rangi ya kibuluu(samawati).Unaweza kutokea kama ugonjwa sugu na kuku kufariki ghafla .Mambukizo kupitia chakula na maji yaliyochafuliwa.Hauna tiba.kinga ni usafi wa hali ya juu na chanjo.Ua na uchome moto kuku wote walioathirika.Chanjo inapatikana kwenye maduka ya pembejeo za kilimo.

UGONJWA WA KUHARA VIFARANGA

Ugonjwa huu unasababishwa na bacteria aina ya salmonella pullorum(Bacillary white bacteria)

Hutokea sana sana katika vifaranga wadogo.Vifaranga hutembea kwa tabu sana,tumbo huvimba na hukokota mbawa zao.Kinyesi chao huwa maji maji na hugeuka cheupe.Hauna tiba.Kuzuia ni kutilia usafi maanani.Ikiwa ugonjwa utatokea,tenga ama ua na uchome ndege.Ugonjwa huu husambazwa kwa kifaranga kutoka kwa mayai ya kuku aliyeathirika,ambaye haonyeshi daalili zozote za kuwa mgonjwa.

HOMA YA MATUMBO YA KUKU - TYPHOID

Huonekana zaidi kwenye kuku wakubwa.Dalili:joto huwa kali,uchovu,panga na ndevu za kuku huwa za kibuluu (samawati).Hauna tiba.Kinga ni kutilia usafi maanani na kuua kuku wagonjwa.Usinunue vifaranga kutoka kwenye vyanzo ambavyo hauvijui,na usitumie mayai kwa ajili ya kuanguliwa kutoka kwenye kuku wagonjwa.

GUMBORO - Infectious Bursal Disease(IBD)

Huonekana tu katika vifaranga walio chini ya wiki 6,na ni wa kawaida katika makundi makubwa ambayo yamefugwa katika sehemu zilizofungwa (indoor).Sio wa kawaida katika mfumo mdogo wa ufugaji vijijini.Dalili za kawaida: kuharisha.Ugonjwa huu ni virusi ,kwa hivyo hauna tiba.Chanjo inapatikana kwenye maduka ya pembejeo za kilimo.

UGONJWA WA KUPUMUA

Dalili:Pua inayotoka makamasi,uvimbe chini ya macho,macho yaliyojifunga,upungufu katika utagaji wa mayai.Tiba ni kuongeza kiua vijisumu (antibotics) katika maji ya kunywa.

UGONJWA SUGU WA KUPUMUA - Mycoplsmosis

Dalili:Pua inayotoka makamasi ama iliyoziba,uso uliovimba,macho yaliyojifunga,upungufu katika utagaji wa mayai,vifo visivyo vya kawaida.Tiba ni kuongeza kiua vijasumu (antibotics)katika maji ya kunywa.

COCCIDIOSIS

Ugonjwa huu unaweza kutokea wakati wowote na katika rika zote,lakini unaweza kuzuiwa kwa kusafisha kwa makini nyumba za ndege.Dalili:hali dhoofu ya kuku,kuchoka,kutembea kichwa chini ,manyoya yaliyotimka,kuhara damu.Vifo katika vifaranga wachanga.Ikiwa vifaranga wataendelea kuishi watabakia kuwa wembamba na watachelewa kutaga.Tiba:Weka dawa ya Coccidiostatics katika maji ya kunywa au chakula.Kuzuia:Usiweke ndege wengi pamoja.Epuka kuweka ndege wa rika mbalimbali katika nyumba moja kwani ugonjwa unaweza kusambaa kutoka kwenye kuku wakubwa hadi kwa vifaranga.

MINYOO

Minyoo ni vimelea vya ndani na ni vya kawaida katika umri wote katika mfumo wa uzalishaji vijijini na mjini.Vimelea hivi husababisha afya mbovu,kupoteza uzito,kupungua kwa uzalishaji wa mayai.Tiba bora ni kuongeza dawa ya minyoo kama piperazine katika maji ya kunywa mara moja ama mbili kwa mwaka,ikiwezekana wiki mbili kabla ya chanjo yoyote.

CHAWA, KUPE, VIROBOTO NA UTITIRI

Huvamia rika zote wakati wowote,lakini hutokea mara kwa mara katika nyumba za kuku zenye unyevunyevu na uchafu.Ndege waliokomaa husumbuliwa na hutumia wakati mwingi wakidonoa na kujikuna.Vifaranga wachanga wanaweza kufa kwa sababu ya upungufu wa damu (anaemia).Kama hautatibiwa utitiri,chawa,viroboto,kupe watasababisha kuku kupungua uzito na pia kuna uwezekano wa kupoteza manyoya kwa sababu ya kunyonywa damu na vimelea na kuwashwa na ngozi.Chawa wanaweza kuonekana karibu na macho na pua.Viroboto vinaweza kuonekana kwenye tumbo.Tiba:Nyunyiza dawa ya kuua vimelea kama Akheri powder,jivu na mafuta.Jivu na poda ya salfa inaweza kutumiwa mahali ambapo kuku huoga na mchanga.Viota vinaweza kulindwa kwa kuwekewa majani kadhaa ya tumbaku yaliyochanganywa na jivu katika viota.

MAGAMBA KWENYE MIGUU

Miguu yenye magamba husababishwa na vimelea vya nje vinavyowasha ngozi kwenye miguu ya ndege.Dalili:Miguu ina magamba yanayoonekana na majeraha na anaweza kulemazwa katika kutembea.Tiba:Weka miguu kila siku kwenye mafuta taa,ama katika dawa kuogeshea mifugo hadi magamba yatoweke.

LISHE DUNI

Ndege wanaoathirika zaidi ni wale wanaofugwa ndani kuliko wale wanaojtafutia chakulaDalili:mifupa kukua vibaya na kunyonyoka manyoya.Ndege hutembea kwa tabu;huchopea .Tiba,ukigundua mapema wape ndege wako vitamini na kalsiam ya ziada kwenye chakula, pia wape majani, mabaki ya mboga za majani au kinyesi cha ng'ombe

Thursday, November 10, 2011

KILIMO BORA CHA MINAZI




UPANDAJI
Uko wa ina mbili kuna wa vibox na wa pembetatu lakini kwa aina zote mbili umbali wa kupanda ni mita 7.6 kutoka shimo hadi shimo la mnazi, kiasi cha mashimo 175 kwa hecta huingia na kama utatumia mtindo wa pembetatu basi mashimo 13 zaidi yataingia kwa hecta.



Ukubwa wa shimo uwe futi tatu kwa kina, upana na urefu hi kwa maeneo yenye udongo mzuri na wakaida lakini maeneo yenye changarawe, mawe mawe na miamba ukubwa uongezeke hadi futi4 kwa mapana , urefu na kina, Shimo lijazwe majani kiasi cha kilo 15 – 20 unaweza kukisia kama theluthi moja ya shimo au futi moja baada ya kushindilia majani, weka juu yake kama, weka udongo wa juu (top soil) kiasi cha futi moja tena ongezea kiasi cha kilo 10 – 20 cha mbolea ya samadi.

Hakikisha haijai na kufunika shimo lote, pia kama utapata ule udongo mwekundu ambao wengi hupenda kuutumia kwenye bustani zao, pia weka humu kiasi kama utaukosa basi acha vivo hivyo, anza kumwagilia maji wiki moja kabla ya kupanda mbegu yako, kama shimo litatitia ongezea udongo wenye rutuba ya kutosha, kumbuka kuacha kisahani kwa ajili ya kukusanyia maji, ila kama ni sehemu ambazo hufurika kipindi cha mvua jaza udongo hadi kuweka tuta ili maji yasituame.

UPANDAJI
Ni vizuri kutumia mbegu ya nazi moja kwa moja kuliko kutumia miche, hii ni kwa sababu mbili kubwa, kwanza ukinunua mche unakuwa hujui imetoka mnazi gani, wenye ubora gani na hata uzaaji wake huujui, lakini inashauriwa kununua nazi kutoka kwenye mnazi moja kwa moja kwa kuchagua mnazi bora na unaozaa nazi nyingi na kubwa, chagua nazi kubwa zaidi kutoka katika kila mnzi bora.

Nazi ambayo haijafuliwa inakuwa na pembe tatu, moja ya pembe hizi huwa kubwa zaidi na mbili zilizobaki hufanan ukubwa, ule upande mkubwa ulazwe chini wakati wa kupandwa, na upande ule wenye kikonyo ambako nazi hujishika katika matawi ya mnazi (mahanda) ndipo ambapo huota, utatakiwa upatate au upapunguze kwa kisu ili kurahisisha kuota, wakati wa kupanda hakikisha nazi ina maji, ikiwa na maji kidogo sana usiipande, panda miezi miwili au mitatu kabla ya mvua kuanza, nazi inauwezo wa kuota yenyewe bila mvua kwa sababu ina maji ndani yake, ila baada ya kuanza kuota kama hakuna mvua ni muhimu kumwagilia ama sivyo mbegu yako itakufa.

Pia ni muhimu kutumia dawa za kuua mchwa au oil chafu wakati wa kupanda, pia kunadaadhi ya mimea ambayo mizizi yake hufukuza mchwa inaweza kupandwa pamoja na nazi yako. Kama utaamua kutumia miche basi hakikisha miche yako haipungui umri wa miezi sita tangu mbegu kupandwa ili kuzuia miche mingi kufa.

MAGONJWA YA MINAZI

- KUOZA VIKONYO
Huanza kwa majani machanga mawili ya mwanzo kubadilika rangi na kuwa njano na baadae huwa na vidoti vyeusi hutokea kwenye ukingo, majani hunyauka na kukauka na kisha sehemu ya chini linapoanzia jani huoza na kutoa harufu mbaya ambapo baadae mnazi wote hufa.

Ili kuzuia ugonjwa huu mara tu unapoona dalili za mwanzo tengeneza mchanganyiko ufuatao (gramu 100 za copper sulphate changanya na nusu lita ya maji) + (Gramu 100 za chokaa changanya na nusu lita ya maji) kila moja itengenezwe peke yake halafu kisha vichanganywe pamoja baadae kisha pulizia kwenye minazi iliyoanza kushambuliwa, kama mnazi umeshambuliwa sana ukatwe na kuchomwa moto kuzuia maambukizi zaidi. Pia pulizia mchanganyiko huu msimu wa baridi kuanzi mwezi wa 5 hadi wa 9 kwenye shamba lako kama kinga.

- KUOZA MAJANI
Majani huwa meusi kwenye ukingo na kuti likiliwa zaidi kati kati, majani machanga yakichomoza huwa dhaifu na kisha huchanguka, mnazi haufi ila mazao huwa duni kama ni mnazi unaozaa

ili kuzuia tumia dawa yoyote ya kuzuia fangasi za mimea kama Hexaconazol, Mancozeb au Dithane - M5, muhimu ukufika duka la pembejeo ulizia dawa ya kuua fangasi wa mimea utapata dawa na maelekezo ya kuchanganya usikariri haya majina ya dawa nilizotaja

Monday, November 7, 2011

MPWAPWA BREED - Mbegu bora ya ng'ombe iliyosahaulika

ASILI
Mbegu hii inatokana na mchanganyiko wa mbegu ya ng’ombe jike aina ya Zebu toka Tanzania na Red madume ya Sindhi na Sahiwal wenye asili ya india na Pakistan lakini waliotolewa nchini Kenya hii ilikuwa ni mwaka 1940 ambapo uzalishaji wa mbegu hii ulifanyika kwa mara ya kwanza katika kituo cha utafiti wa mifugo Mpwapwa Dodoma nchini Tanzania

Mwaka 1958 uboreshaji wa mbegu hii ulifanyika kwa kuongezea damu za ng’ombe wa ulaya (Bos Taurus) aina ya Ayshire na Jersey na mpaka kufikia mwaka 1960 mbegu ya Mpwapwa ikawa na na uwiano wa 20% Tanganyika Zebu 10% Boran 5% Ankole 55% Red Sindhi na Sahiwal na 10% Ayshire na Jersey. Mpaka mwaka 1971 mbegu hii ikawa na mchanganyiko wa 32% Red Sindhi, 30% Sahiwal, 19% Tanganyika Zebu 10% Boran na 10% Ayshire na Shorthorn, utagundua kwamba mbegu ya Jersey iliondolewa na kuingizwa short horn

MWONEKANO
Wanaonekana zaidi kama Sahiwal wakiwa na rangi nyekundu iliyofubaa mpaka kukooza sana au Nyekundu na nyeupe, Wana nundu kama ng’ombe wetu wa kienyeji, ngozi ya chini yashingo ijulikanayo kama DEWLAP ni ndogo zaidi ya Zebu lakini kubwa zaidi ya Ng’ombe wa kigeni, wana kiwele kikubwa zaidi ya ngombe wa kienyeji chenye kukamilika kirahisi ANGALIZO nundu na dewlap huwasaidia kupambana na mazingira ya Afrika hasa joto kali

MBEGU YA MPWAPWA


Madume yana uzito kati ya kilo 450 – 600 na majike kilo 275 – 300 wakati wa uzazi wa kwanza na huongezeka hadi kufikia kilo 450 hapo baadae, mbegu hii inauezo wa kuzalisha maziwa mengi kuliko ng’ombe wa kienyeji na pia uhimili mazingira ya joto na magonjwa kuliko Tanganyika Zebu

Serekali imeshindwa kusambaza mbegu hii kwa wafugaji na inasemekena karibia itapotea kwa sababu ng’ombe wa Mpwapwa waliobakia ni wachache sana na wanapatikana kwenye baadhi ya vituo vya utafiki kama Mpwapwa kwenyewe. Pia kuna tetesi kwamba kwa sasa hakuna MBEGU HALISI (pure breed) ya ng’ombe hawa kutokana na kuachwa wakapandana ndugu kwa ndugu (Inbreeding)

Wednesday, September 28, 2011

LEO NI SIKU YA KICHAA CHA MBWA DUNIANI -

Wakati leo tunaazimisha siku ya kichaa cha mbwa duniani, ugonjwa huu hapa nchini kwetu bado umekuwa tatizo sugu. Katika wilaya ya Temeke pekee watu 202 waling'atwa na kati ya hao 19 waliugua kichaa cha mbwa. Wilaya hii inajumla ya mbwa 4500, paka 1500 ambapo kati ya hao 3418 walifanikiwa kuchanjwa.

CHANJO YA KICHAA CHA MBWA (RABIES) KWA AJILI YA WANYAMA


Ugonjwa huu huweza kumpata viumbe vingi ikiwemo binadamu, ng'ombe, mbuzi, kondoo na kadhalika, na wasmbazaji wakuu wakiwa mbwa na paka ingwa kuna baadhi ya poo (vampire bats) nao pia husambaza ugonjwa huu kwa kung'ata na kusambaza vimelea vya kichaa cha mbwa.

ugonjwa huu upo kila sehemu ya dunia ambapo kwa mwaka huua jumla ya watu 55,000 kote duniani ambapo Afrika watu 21,000 hufa kila mwana na wengine 34,000 hufa barani Asia na kwingineko

Kauli mbiu ya mwaka huu ni TUSHIRIKIANE KUFANYA KICHAA CHA MBWA KUWA HISTORIA na njia pekee ni kuwachanja wanyama wetu, na pia kuwazuia wasizurure hovyo mitaani, MUONE MTAALAM WA MIFUGO ALIYE KARIBU NAWE ILI MBWA NA PAKA WAKO WAPATE CHANJO KAMILI

WILAYA ZA NGORONGORO NA LONGIDO ZAKUMBWA NA UGONJWA HATARI WA HOMA YA MAPAFU YA NGOMBE



Wilaya za Ngorongoro na Longido ambazo zipo mpakani na Kenya zimekumbwa na ugonjwa wa mapafu wa ng'ombe, hali hii imefanya jumla ya ng'ombe milioni moja (1,000,000) kuwa katika hatari ya kukumbwa na ugonjwa huu.

Ugonjwa huu ulitangazwa kama janga la kitaifa mnamo mwaka 2001 kwa sababau ni hatari sana na unaua ng'ombe kwa kasi sana, na unaweza kudhibitiwa kwa kuchanja mifugo mara unapoonyesha dalili za mlipuko.

Kutokana na hilo serekali imechukua hatua za dharura za kuwachanja ng'ombe wote katika wilaya ya Ngorongoro, Longido na zile za jirani kama Karatu na nyinginezo.

Historia ya ugonjwa huu inaanzia enzi za ukoloni mnamo mwaka 1905 na uliweza kudhibitiwa, lakini mnamo mwaka 1964 mwaka ambao ndio wa muungano wa Tanganyika na Zanzibar ulitokea na Tanzania kuzaliwa, ugonjwa huu ulilipuka tena nchini mwetu. mnamo mwaka 1990 ugonjwa huu ulilipuka tena katika Wilaya ya Loliondo mpakani na Kenya.



Mwaka 1994 ugonjwa huu ulilipuka tena na kusambaa hadi mkoa wa Morogoro katika wilaya za kilosa na Mahenge. na mwaka 1998 ugonjwa huu ulisambaa katika mikoa 11 ya nchi yetu

Ugonjwa huu hujulikana kama contagious bovine pleural pneumonia au CBPP kwa kifupi na kama unataka mifugo yako ichanjwe wasiliana na maofisa ugani waliokaribu nawe au ofisi za wizara ya mifugo

Saturday, September 17, 2011

MBEGU BORA YA MIHOGO YAGUNDULIWA

SHAMBA DARASA LA MIHOGO




Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika ikishirikiana na taasisi ya kimataifa ya kilimo cha kitropiki (IITA) kwa pamoja zimezalisha aina mpya ya mbegu za mihogo zenye kustahimili magonjwa makubwa ya zao hilo. Mbegu hiyo mpya inayojulikana kama KIROBA inatoa wanga mzuri kwa ajili ya lishe na kuhimili magonjwa, pia inaweza kutoa mazao kufikia tani 35 kwa hecta.


MIHOGO BORA TAYARI KUVUNWA



Akiongea hayo Meneja wa mradi wa Shirika la chakula Duniani (FAO) BW. Raphael Laizer wakati anakagua mashamba darasa ya mihogo huko Mkuranga, alisistiza kutumia mashamba darasa ya zao la muhogo kwa ajili ya majaribio ili kupata mbegu bora ambazo zitalimwa karibu mikoa yote na ziwe zenye uwezo wa kuhumili ukame na magonjwa pia.

MIHOGO YA KUKAUSHA (makopa) KWA AJILI YA UNGA

Saturday, August 13, 2011

KILIMO CHA VITUNGUU TWAUMU - garlic





UDONGO
Vitunguu twaumu vinahimili aina nyingi za udongo, ila vinastawi zaidi katika udongo usiotuamisha maji kabisa na wenye mbolea asili, kama mbolea si ya kutosha kwenye udongo, tumia samadi iliyokwisha oza vizuri usitoe samadi bandani na kuipeleka shambani moja kwa moja kwenye shamba la vitunguu thwaumu, labda kama utaliacha shamba bila kulimwa kwa zaidi ya miezi 6, pia unaweza kutumia mbolea za viwandani kama ammonium nitrate, ammonium sulphate, urea n.k wakati wa kupanda na kila baada ya wiki 4 – 6 mara mbili zaidi

UPANDAJI
Kipindi kizuri kwa upandaji ni kipindi ambacho hakuna joto hasa miezi ya May mpaka August kwa Tanzania, Unachukua kitunguu twaumu na kutenganisha vitunguu kimoja kimoja (bulbs) na kuchagua vile vikubwa maana hivi ndivyo vitakavyo kupa mazao mengi na bora, nafasi kati ya kitunguu na kitunguu ni sentimeta 10 na kati ya mistari ni sentimeta 30. Baada ya kupanda pandishia udongo na uukandamize kuhakikisha kwamba kimekaa vizuri na hakiwezi kuathiriwa na mvua au maji wakati wa kumwagilia ili kisikae upande au kungolewa kabisa. Uotaji mzuri hutegemea pia namna vitunguu thwaumu vilivyo hifadhiwa kabla ya kupandwa, kama vilihifadhiwa sehemu zenye joto na hewa finyu uotaji wake utakuwa duni na dhaifu.


UMWAGILIAJI

Kama kuna upungufu wa mvua au ni kipindi cha kiangazi basi ni vizuri ukamwagilia shamba lako, wakati mzuri wa kumwagilia vitunguu twaumu ni asubuhi na sio jioni au mchana, hii inasaidia vitunguu twaumu kujijengea uwezo wa kupambana na magonjwa, baada ya mizi miwili unaweza kupunguza umwagiliajai huku ukiangalia kwa kuchimba kidogo kama vitunguu twaumu vimezaliana vya kutosha na kuanza kukomaa, ukiona vimekomaa acha kabisa kumwagilia ili visioze

UANGALIZI
Aina nyingi za vitunguu twaumu vitakuwa kama vinatoa mbegu kwenye mmea (angalia picha chini), ingawa kuna nadharia nyingi lakini inashauriwa kukata hizi mbegu chini kabisa kwa kisu kikali na kisafi, usikate mapema mara baada ya kutokeza bali subiri mpaka mmea unapoanza kama kujikunja ndipo ukate, kwa wale wanaoacha mbegu hizi ukiamua kuzipanda kwa msimu wa kwanza zitazaa kitunguu kimoja tu cha duara lakini chenyewe ukikipanda tena kwenye mzunguko wa pili kitazaa vitunguu vingi kama kawaida



Ungoleaji wa magugu na majani ni muhimu muda wote ili kuondoa kugombea rutuba, hewa na maji shambani, kwa wenye mashamba makubwa wanaweza kutumia dawa za kemikali kama ROUNDUP na nyinginezo ili kudhibiti magugu, ingawa mimi sishauri hivyo.

MAGONJWA
Magonjwa kama botrytis (kuoza shingo) blue mould na fusarium (kuoza kwa vitunguu) husababisha hasara kubwa kama hayatadhibitiwa kwa kutumia viuatilifu mara unapoona dalili, pia magonjwa kama white rot huchukua zaidi ya miaka 20 kuondoka kama yatavamia shamba lako, inashauriwa kufanya mabadiliko ya zao kila baada ya miaka mitano kwa kupanda mazao mengine yasiyo jamii moja kama vitunguu maji, unaweza kupanda maharage, mahindi, karoti na kabichi katika mzunguko huo. Pia magonjwa kama kutu ya majani husababisha na unyevu mwingi hasa kama mimea itakuwa kwenye udongo unaotuamisha maji au mimea kumwagiliwa jioni au usiku, kumbuka kumwagilia asubuhi tu Ili kudhibiti ugonjwa huu wa kutu mimea ingolewe na ichomwe au utumie viuatilifu vya kuulia fangasi wa mimea.

Monday, August 8, 2011

NANE NANE NA MELTON KALINGA

Leo ni siku ya wakulima yaani nane nane na maadhimisho kitaifa yanafanyika Dodoma, mimi niko na mtaalam wa Samaka Bw Melton Kalinga kwenye kituo cha Kingolwira nje kidogo ya Morogoro mjini kama km12. Kinachofanyika kwa leo ni upandishaji wa Samaki aina ya kambale

Unaanza kwa kutafuta majike makubwa yenye mayai tumboni, kisha unatafuta na Madume yaliyokomaa, ili kupandisha kwa njia ya kimaabara kambale dume inabidi umuue kisha unachukua pituitari gland na kumwingizia jike mwenye mayai aliye hai, baada ya masaa 24 mayai yanakuwa yame komaa, unayakamua toka kwa jike kisha unachanganya na mbegu za kiume toka kwa samaki uliyemuua jana yake, kwa kutumia mtambo wa maabara wenye maji ya vuguvugu unatotolesha mayai hayo kwa njia ya kitaalam.

Vifaranga wa samaki aina ya sato wanapatikana pia kwa shilingi 50 tu, kwa mawasiliano zaidi mpigie Bw Kalinga 0757891761 au 787596798

KAMBALE WAKIVULIWA KWENYE BWAWA






UKAGUZI NA UCHAMBUZI KUJUA MADUME NA MAJIKE WANAOFAA





SAMAKI JIKE MWENYE MAYAI

SAMAKI DUME



UTOAJI WA MBEGU TOKA KWA DUME

MTAMBO WA KUTOTOLESHEA MAYAI YA KAMBALE

Thursday, July 7, 2011

MATIKITI MAJI - water melon




Ili kulima matikiti maji, inakubidi uwe na sehemu ya kutosha, yenye jua la kutosha, maji mengi na ardhi yenye rutuba ya kutosha, matikiti maji hukua haraka kama mimea mimgine ya jamii yake itambaayo mfano Matango, maboga na maskwash.
Kwa mtu ambaye anaanza kilimo yatampa tabu kidogo tofauti na Yule ambaye ana ujuzi kidogo na mambo ya kilimo kwa sababu yanahitaji umakini kiasi.

HALI YA HEWA
Mimea hii haihimili hali ya joto kali sana, mvua nyingi na udongo unaotuamisha maji, magonjwa ya fangasi na wadudu waharibifu, inastawi vizuri kwenye kuanda wa pwani na miinuko kidogo kama DSM,Tanga, Morogoro, Mtwara, lindi na Pwani ambapo kuna jua la kutosha. Muda mzuri wa kupanda ni kipindi cha kipupwe mwezi wa machi mpaka wa septemba .

UPANDAJI
Panda kwa kutumia Mbegu zinazouzwa madukani, ukitumia Mbegu kutoka kwenye tikiti ulilonunua linaweza likawa ni hybrid na matokeo yake matikiti yatakayozaliwa hayatakuwa bora kwa sababu yatakuwa ni kizazi cha pili (F2)
Panda Mbegu yako moja kwa moja kwenye shamba, usinunue miche au kupanda Mbegu kwenyemifuko ya plastiki halafu ndi uhamishie shambani, panda Mbegu mbili sentimeta 2 chini ya udongo kwa umbali wa sentimeta 30 kutoka shina hadi shina na mita 2 - 3 kutoka mstari hadi mstari, baada ya siku chache Mbegu zitaanza kuota, baada ya kama wiki 2 katika Mbegu mbili ulizopanda kata moja na uache ule mche wenye afya zaidi, angalizo using’oe mche bali ukate ili kuzuia kusumbua mizizi ya mche uliobaki.
Unaweza kupandishia udongo kwenye mashina na hii itasaidia kupunguza maji yasituame kwenye mimea yako, pia unaweza kuweka samadi badala ya kupandishia udongo ukiwa na nia ileile ya kuzuia maji yasituame na kuongeza rutuba.
Kama una sehemu ndogo ya shamba unaweza kuyawekea matikiti waya wa kutambalia, ila inabidi uwe imara kwa sababu ya kuhimili uzito wa matunda yenye, na wakati wa kuanza kutambaa kwenye waya ni lazima uifundishe mimea kwa kuielekezea kwenye waya na kufungia

MCHE ULIOCHIPUA


UANGALIZI
Miche ikiwa imetambaa kiasi unaweza kuweka matandazo kwenye udongo ili kuzuia upotevu wa unyevu, unaweza kuweka samadi au mbolea za viwandani, mimea ikiwa midogo tumia zaidi mbolea zenye nitrojen na utumie zaidi mbolea za potasiam mara baada ya maua kutokeza hadi matunda kukomaa, matawi yakifikia urefu wa mita 2 kata mbele ilikuruhusu kutoa matawi na hivyo kupata maua mengi zaidi hatimaye mavuno zaidi

MAUA NA MATUNDA
Matikiti hutoa maua dume na jike kwenye tawi moja, maua dume ambayo ni madogo zadi hutoka kwanza yakifuatiwa na maua jike ambayo ni makubwa zaidi, usipoona maua dume na jike kuna tatizo mfano maji kidogo yalimwagiliwa, upungufu wa viritubisho kwenye udongo, hali ya hewa ni joto/baridi sana n.k
Uchavushaji kwenye matikiti hufanyika na wadudu, kama huwaoni wakifanya kazi yao unaweza kufanya mwenyewe, muda mzuri ni wa asubuhi, unakata maua dume kwa kisu na kufanya uchavushaji kwenye maua jike, maua jike ya mwanzo kwenye tawi ndiyo yenye ukuaji bora zaidi, unaweza kukata tawi lisiendelee kukua baada ya matunda kutokeza hii husababisha kuwa na matunda makubwa zaidi

UCHAVUSHAJI KWA MKONO


UVUNAJI MATIKITI
Ili kujua matikiti yamekomaa inahitaji ujuzi kidogo, upande wa chini wa tunda huanza kuwa na rangi ya njano, pia kikonyo juu ya tunda hukauka kabisa na kuwa kijivu, ila njia nzuri ni kuyapiga kwa kiganja na kusikiliza mlio wake kama tunavyofanya kwenye mafenesi, hii nayo ni shule nyingine. Tumia kisu wakati wa kuvuna matikiti, yabebwe na kuhifadhiwa vizuri kwenye makasha tayari kuuzwa au kwa matumizi binafsi

MAGONJWA NA WADUDU
Wadudu wa matikiti wako wanaoshambulia majani na maua, na wengine hushambulia matunda , pia kuna magonjwa ya fangasi ambayo hushambulia mimea, ili kujua dawa za magonjwa ni vizuri kuchukua sampuli na kwenda nayo kwenye duka la dawa na pembejeo za kilimo ili kjupata dawa sahii, dawa aina ya KARATE itasaidia kuua wadudu wa majani, maua na matunda na FUNGICIDE itasaidia kwa mashambulizi ya fangasi

Sunday, June 26, 2011

LINDI - MTWARA

NYAMWAGE - MUHORO


MIKINDANI


MABIRIKA YA KUTENGENEZEA CHUMVI - LINDI


BEACH MTWARA


HIKI NDIO KIPANDE AMBACHO HAKINA LAMI KAMA KILOMETA 60

Thursday, June 16, 2011

NDANI YA RUFIJI

CHOMBO KINAKUJA



Wadau samahanini sana kwa kupotea humu kijiweni, ilikuwa ni lazima nipotee ili vitu vingine viende, lakini sasa nimerudi rasmi kwenye kijiwe changu

Wiki hii nilikuwa wilayani Rufiji nilifika sehemu kama Kibiti, Utete, Ikwiriri, Mkongwa na Nyamwage. Nililala Utete, ni sehemu tulivu na watu wake ni wakarimu kama tulivyo waTanzania wote.

Hali ya utete kwa wakati huu ni joto limepungua sana wala uhitaji kulala na feni kama DSM, kuna mbu wengi sana ni lazima ulalae na chandarua, mji hii uko pembeni ya mto Rufiji




Wakati wa kwenda tulitumia barabara ya Kilwa hadi Kibiti tukakata kulia kama unaelekea hifadhi ya Selous na kufika kijiji cha Mkongwa tukakata kulia na kuelekea kwenye kivuko cha Utete, tukasubiri pantoni baaddae tukavuka na kuingia Utete kama saa 3 asubuhi kwa kupitia njia hii ya mkato tuliokoa mwendo wa kilometa kama 40.

Utete tuliona vitu vingi maana kwanza kuna mto huu wa Rufiji, lakini bado hawajaanza kuutumia kiukamilifu, ila nina imani mambo yatakuwa mazuri maana kuna RUBADA ambayo mamlaka hii imepewa jukumu la kuendeleza bonde la Rufiji.

NAHODHA WA MV UTETE - BWANA ALLI


Wakazi wa Utete ni wakulima wa mazao kama Mpunga, mahindi na shughuli za uvuvi, pia kuna baadhi wanafuga samaki katika mabwawa binafesi ingawa ufugaji wao si mkubwa na si wakitaalam zaidi

TAA ZA BARABARANI - uswazi kwetu hamna hizi


Mji wa Utete una huduma za simu mitandao ya Voda, tigo , Airtel na Zantel, pia kuna umeme na taa mpaka za barabarani ingawa barabara hazina lami, mji una maji ya bomba lakini cha kuchekesha chanzo ni kisima waka mji unapitiwa na mto hapo hapo, maji ni ya chumvi

URITHI WETU



Usafiri ni wa mabasi mawili kwa siku moja saa 12 asubuhi na lapili kwenye saa 6 mchana ukiyakosa hayo, omba lifti kwenye magari madogo madogo ya Serekali au Binafsi au sivyo utalala.

WATAALAMU WA USHAURI KWENYE NYANJA ZOTE


Huduma nyingine ni Hospitali ndogo, pia kuna Magereza, kuna BOma lililojengwa na mkoloni linalotumika kama Ofisi ya Wilaya, Kuna posta, Nyumba za kulala wageni, sehemu za vinywaji, soko, na maduka ya bidhaa mbali mbali.

CHEMCHEM YA MAJI MOTO


Ukifika Utete ulizia wakulete huku, kwa pikipiki ni buku tu unalipia, wenyeji wanaamini maji haya ni yamaajabu na yanaweza kuytibu magonjwa, niliogopa kuwaambia hii ni volcanic feature

USAFIRI TOKA VIJIJI VINGINE KUJA UTETE


MAPATO NI MUHIMU


EWURA WAKIJA HUKU NI BALAA- PETROL INAUZWA KWENYE HIVYO VIDUMU



NILIUKUTA MTIKI IKABIDI NIUHUG



MKONGWA





KILMO KWANZA