KURASA

Friday, March 26, 2010

KONDOO AKISAIDIWA KUZAA WATOTO MAPACHA

JINSI YA KUKATA MICHE YA MISOJI (MITIKI)

Kwa kawaida miche ya misoji mara baada ya kutolewa kwenye kitalu huitaji kukatwa, mjasiliamali aliyeko jijini Mwanza aitwae NAYMA aliniomba nimwelekeze kwa picha na mimi bila hiyana nilikwenda shamba na kung,oa mche mmoja na kuukata na kuupiga picha kabla ya kuukata na baada ya kuukata ili kupata kipandikizi

MCHE KABLA YA KUKATWA (angalia mishale kujua sehemu za kukata)


Mche wangu niliukata na kuacha kiasi cha nchi mbili au pingili mbili za vidole kwa sehemu ya juu ya mzizi na kwenye mzizi niliondoa ile sehemu nyembamba ya chini, kwa kawaida hii sehemu ya chini hufa mara baada ya kupandwa kwa sababu sehemu nene/kubwa ya mzizi inayoachwa ndiyo huifadhi maji na chakula cha mmea, nadhani hapa nitakuwa nimemsaidia kama bado nipigie kwenye ile namba niliyokupa

KIPANDIKIZI TAYARI KWA KUPANDWA


Kumbuka wakati wa kupandwa lazima uweke kisahani ili kiweze kukusanya maji kwa ajili ya ukuaji mzuri, kama ni udongo unaotuamisha maji usiweke kisahani bali wekea kama tuta au mwinuko

WEKA KISAHANI KAMA UDONGO HAUTUAMISHI MAJI


WEKA TUTA KAMA UDONGO UNATUAMISHA MAJI

Friday, March 19, 2010

MBWA WAKIPANDANA KWA NINI HUNASIANA AU KUNATANA?



Nadhani karibia kila mtu ameshawahi kuona mbwa wakipandana, kama bado basi maelezo haya yatakusaidia siku ukiwaona, mara baada ya mbwa dume kumpanda jike utaona dume anageuka na kupeana mgongo na jike kila mmoja akiangalia upande wake wakati huo huo, uume ukiwa bado ndani ya uke, wanakuwa kama wanavutana na wakati mwingine wanaweza kutoa milio kama wanalalamika, unaweza kuhisi wanaumia na ukataka kuwatenganisha ACHA na wala usijaribu kufanya hivyo utawaumiza.

Kwa kawaida mbwa dume anapoanza kumpanda jike uume unakuwa haujasimama bali husaidiwa na kiuongo kijulikanacho kama baculum, hii ni tishu kama mfupa na iko ndani ya uume wa mbwa. Wakati mbwa dume anapotaka kumwaga manii ndani ya uke ndipo damu hujaa kwenye uume na hapo uume hutanuka (kudinda) kwa hiyo akimaliza kutoa manii uume hunasa ndani ya uke kwa sababu ya kule kutanuka.



Mbwa dume anapogeuka anazipa muda Mbegu za kiume ziweze kuingia vizuri kwenye uke na hivyo kusababisha ujauzito, ukitumia nguvu kuwaachanisha, mbali na kuumia pia jike hataweza kupata ujauzito. Hiki ni kitu cha asili kwa hiyo husaidia pia kuzuia madume mengine yasiingilie tendo hili na kulikatisha wakati Mbegu bado zinaogelea na kuyafuata mayai kwenye mji wa mimba, kwa kawaida hata kama mbwa madume walikuwa wanapigana kila mmoja akitaka kumpanda jike, mara baada ya Yule aliyefanikiwa kupanda na kugeuka wale wengine huacha vurugu zote.

MBWA WALIONASIANA BAADA YA KUPANDANA


Tendo hili huchukua kati ya dakika 20 – 30 na mbwa hufanikiwa kunasuka mara baada ya damu kupungua kwenye uume na uume kusinyaa na kupungua ukubwa. Kwa mbwa dume ambaye ni mara yake ya kwanza kupanda basin a hata yeye huchanganyikiwa atakapoona amenasa, anaweza hata kujaribu kujinasua au kupiga kelele, unachotakiwa ni kumshika shika shika mbwa wako kichani huku ukimuongelesha kwa upole, yaani jaribu kumpunguza presha ili atulie

Monday, March 8, 2010

KILIMO CHA UYOGA

Miaka ya karibuni, utaalamu wa kuotesha uyoga umeanza hapa Tanzania baada ya watu kutilia maanani lishe bora ya protini na manufaa mengine ya zao hilo. Kwa kuwa uyoga upo wa aina mbalimbali, usitawishaji wake hutofautiana katika mahitaji yake, ikiwa ni pamoja na hali ya hewa, malighafi za kuoteshea, urahisi wa teknologia ya kuotesha katika mazingira ya Tanzania na soko lake kwa wananchi na katika hotel. Hata hivyo ni wananchi wachache tu wanaojua kilimo cha uyoga.



Uyoga unaozalishwa unafahamika. Aina zinazofaa kwa Tanzania ni zile ambazo hustawi vizuri, kwenye maeneo ya joto la wastani wa nyuzi joto 20C hadi 33C. Kwa mfano uyoga aina ya mamama n.k. Aina hizi za uyoga pia uhitaji hali ya unyevu hewani (moisture) wa kiasi cha asilimia 75%.

UOTESHAJI WA UYOGA
Kabla ya kuanza kuzalisha uyoga inabidi kuwa na chumba chenye paa ambalo litazuia jua, mvua, na vumbi. Chumba hiki kinatakiwa kiwe na sakafu inayohifadhi unyevunyevu pamoja na sehemu ya giza ambayo ni muhimu kwa kuotesha utando wa uyoga. Mkulima
wa kawaida anaweza kutumia kasha kama sehemu ya giza.

Mbegu za uyoga huzalishwa kwenye maabara zenye vifaa vinavyowezesha kuotesha mbegu hizo bila kuchafuliwa au kuchanganyika na vimelea kama bakteria, ukungu au jamii
nyingine za uyoga ambazo haziliwi. Hapa Tanzania hivi sasa maabara hizo zipo Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kituo cha utafiti wa kilimo-Uyole na taasisi ya utafiti wa kilimo cha bustani- Tengeru (HORTI
Tengeru, Arusha).


HATUA MUHIMU ZA KUOTESHA UYOGA
Hatua muhimu za kuotesha uyoga baada ya kupata mbegu ni kama ifuatavyo:
Kusanya masalia ya mazao kama vile mabua, majani ya mpunga, ngano, pumba za mpunga au mahindi, masalia ya miwa baada ya kukamua nk. Vitu hivi hutumika kama mali
ghafi kwa kuoteshea uyoga.
Mabua, majani ya mpunga au migomba yakatwe kwa urefu usiozidi sm 6, au urefu wa vidole kwa kutumia panga au kisu.
Loweka mali ghafi kwenye maji ya kawaida kwa muda wa siku nzima (masaa 24).
Kisha yachemshe kwa muda wa saa mbili ili kuua vijidudu pamoja na vimelea vilivyomo.
Ipua na umwage maji yote halafu tandaza kwenye kichanja kisafi ili yapoe bila kuchafuliwa na vumbi au vijidudu.
Kisha jaza mali ghafi hii katika mifuko ya nailoni tayari kwa
kupanda mbegu.

NAMNA YA KUPANDA
Kuna aina mbili za upandaji

AINA YA KWANZA


Chukua mfuko wa nailoni wenye upana wa cm 40 - 45 na kimo cm 75. Weka tabaka la mali ghafi ya kuoteshea yenye kina cha sm 10 katika mfuko halafu tawanya mbegu ya uyoga juu yake. Baada ya kuweka mbegu, weka tena tabaka nyingine ya vioteshea na kuweka
mbegu juu yake. Endelea kuongeza tabaka kwa namna hii mpaka ifike ujazo wa robo tatu ya mfuko.

AINA YA PILI

Changanya malighafi ya kuoteshea (baada ya kuchemshwa na kupoa) na mbegu ya uyoga katika uwiano wa 1: 25 (mbegu : malighafi ya kuoteshea) kwa uyoga aina ya mamama (Pleurotus spp.)Kisha mchanganyiko huo ujazwe katika mifuko ya nailoni mifuko hii
iwe na ukubwa wa cm 20 kwa cm 40 ambamo unaweza kujaza kilo 1 – 1.5 ya mali ghafi ya kuoteshea.

Funga mifuko na toboa matundu kwenye mifuko yenye kipenyo cha cm 1 kwa kila umbali wa cm 6 hadi 10 kwa kila mfuko.Matundu yawe mengi ili kuingiza hewa ya kutosha ndani ya mifuko. Kumbuka uyoga ni kiumbe hai hivyo unahitaji kupumua kama inavyoonekana kwenye picha hapo chini.



MATUNZO
Weka mifuko kwenye chumba cha giza. Kwa mkulima wa kawaida waweza kutumia kasha lisilopitisha mwanga kama chumba cha giza. Acha mifuko humo kwa muda wa siku 14 - 21 bila kufunua ili ukungu mweupe uweze kutanda vizuri.Utando wa uyoga ukishatanda vizuri kwenye mali ghafi ya kuoteshea, hamishia kwenye chumba chenye mwanga na hewa ya kutosha kisicho pigwa na jua. Katika chumba chenye mwanga, mifuko inaweza kuwekwa
kwenye, meza, chanja la waya au miti. Mifuko inaweza pia kuning’inizwa kwenye kamba toka kwenye boriti za paa la chumba hicho. Unatakiwa kudumisha hali ya unyevu kwenye chumba hicho cha mwanga kwa kumwaga maji sakafuni. Ukiona vipando vinakauka
unaweza kunyunyizia maji yaliyochemshwa na kupoa juu ya mifuko mara tatu au zaidi kwa siku. Tumia bomba la mkononi lenye ukubwa wa lita moja kunyunyizia maji.
Tafadhali: usizidishe maji kwani maji yakiwa mengi sana yaweza kuozesha uyoga uliyoanza kuota. Aina nyingi za uyoga huanza kutoa vichwa (pini) siku 2 - 3 baada
ya kuwekwa kwenye mwanga.

UVUNAJI
Uyoga huwa tayari kuchumwa siku tatu baada ya vichwa /pini kuonekana.
Uyoga uvunwe kwa mkono kwa kushika katikati ya shina la uyoga kisha zungusha hadi uyoga ung’oke. Usiondoe kichwa peke yake katika kuvuna uyoga kwani kubakiza shina huzuia uyoga mwingine kutokea. Mkulima anatakiwa ajue soko la uyoga kabla ya kuvuna ili kuepuka gharama za kuhifadhi. Kwani uyoga ukishavunwa unatakiwa uliwe
kabla haujaharibika.

JINSI YA KUHIFADHI
i) Unaweza ukauweka uyoga kwenye mifuko ya karatasi na kuhifadhi kwenye jokofu.
ii) Unaweza ukauanika juani hadi ukauke na kuweka kwenye mifuko ya nailoni liyofungwa vizuri ili isipitishe hewa na unyevu.

SOKO LA UYOGA
i) Watu wengi hupenda uyoga mbichi uliotoka shambani wakati huo huo kama kitoweo, kwa kutumia kama nyama, samaki, au kama kiungo.
ii) Unaweza kuuza uyoga mbichi kwa bei ya shilingi 3000/= hadi 5000/= kwa kilo kwa uyoga aina ya mamama.
Pia unaweza kuuza nje ya nchi ikiwa uyoga wako ni kiasi kikubwa na uko katika viwango vinavyo kubalika kimataifa.



MAMBO YA KUZINGATIA
Uzalishaji wa uyoga huzingatia sana hali ya hewa na vifaa ulivyonavyo, hivyo basi, kabla hujachagua aina ya uyoga unaotaka kupanda pata ushauri kwa wataalamu walio
karibu nawe.

Ukishanunua mbegu, kama hupandi kwa muda huo, hakikisha umehifadhi mbegu hiyo kwenye jokofu. Kama huna jokofu la kuhifadhia, nunua mbegu baada ya kuandaa kila kitu. Hata hivyo, uotaji wa mbegu huwa mzuri kama zitakaa nje ya jokofu kwa siku mbili.

Mbegu za uyoga huwekwa ndani ya chupa yenye ujazo wa mililita 300, waweza kutumia chupa moja katika kupanda kwenye kilo 15 ya mali ghafi ya kuoteshea. Hakikisha
unamaliza mbegu yote iliyo ndani ya chupa kwani ikibaki itapata maambukizo ya vimelea.
Hakikisha unaponunua mbegu iwe ni nyeupe. Mbegu ambayo siyo nyeupe ni dalili za maambukizo ya vimelea vingine na hivyo haifai kwa kupanda.

Hakikisha chumba cha kupandia ni kisafi na hakipati vumbi toka nje ili kuzuia maambukizo ya magonjwa ya uyoga.

Usimwagilie uyoga maji yasiyochemshwa kwani maji hayo mara nyingi si salama. Yaweza kusababisha vimelea vingine kuota, kwani uyoga ni dhaifu kuhimili ushindani wa
vimelea.

Pia waweza kusababisha magonjwa ya uyoga ambayo kutibu kwake kunahitaji kutumia dawa za viwandani ambazo ni sumu na hivyo kusababisha madhara kwa mlaji. Unaweza kupata faida nyingi kutokana na uzalishaji wa uyoga,

FAIDA ZA UYOGA:-
Lishe kama protini inayolingana na ile ipatikanayo kwenye maziwa, samaki na kunde. Pia utapata vitamini B, C, na D, na madini ya joto, phosphoras, chuma na potashi.

Uyoga husadikika kutibu maradhi kama kifua kikuu, kisukari, moyo, shinikizo la damu na figo.

Masalia ya mazao hutumika katika kuzalishia uyoga, na baada ya kilimo cha uyoga yanaweza kutumika kama mbolea asili kwa kilimo cha bustani. Masalia ya kilimo cha uyoga pia hutumika kama chakula cha mifugo kama ng’ombe.

Kilimo hiki huhitaji eneo dogo sana la ardhi na kiasi kidogo cha maji, hivyo hupunguza tatizo la ukosefu wa ardhi na ugomvi katika jamii ambao unatokana na tatizo hilo.

Kilimo hiki ni njia nyepesi ya kutoa ajira kwa familia kutokana na gharama ndogo, teknolojia rahisi inayotumika na pato lake kubwa.