KURASA

Monday, December 19, 2011

MGOGORO WA KILIMO CHA MAHINDI MKOANI SINGIDA




Umeibuka mgogoro mkoani Singida mara baada ya mkuu wa mkoa Dr.Parseko Kone kupiga marufuku kilimo cha mahindi mkoani humo. Mmoja wa waliopinga mpango huo ni Mheshimiwa Salome Mwambu mbunge wa Iramba mashariki kwa tiketi ya CCM.

Akitetea kilimo cha mahindi MH Mwambu alisema kwamba hilo silo tamko la mkoa kwa sababu hakuna hata kiongozi mmoja wa mkoa au wilaya ambaye alijaribu kuwashirikisha wananchi kwenye mchakato huo

Pia alisema kwamba kilimo cha mahindi kilikuwepo kwa miaka mingi mkoani humo na zao hilo likiwa ni la biashara na chakula kwa wananchi wenyewe



MAONI YANGU

Viongozi wote wawili walikuwa na nia njema sana kwa wananchi wa Singida, mkuu wa mkoa alikuwa anajitahidi kukabiliana na njaa mkoani mwake na ndio maana akawa anasisitiza kilimo cha mazao ya kinga ya njaa,ambayo ni yale yanayohimili ukame na uhaba wa mvua kama mtama, ufuta na uwele n.k

Mh mbunge naye alikuwa akiwatetea wananchi wake kwa sababu ndio wapigakura wake na yeye ndiye mwakilishi wao, akiangalia anaona kwamba miaka mingi watu wamekuwa wakitegemea mahindi kama zao la chakula na biashara, ndio maana akashauri kwamba watu wasikatazwe kulima mahindi bali walazimishe kupanda na mazao ya kinga ya njaa

Kwa ujumla wote wamefanya maamuzi bila ya kuwashirikisha wataalamu wa kilimo na hali ya hewa, kila mtu alikuwa anatetea kibarua chake. kama wange washirikisha wataalamu basi nina imani kwamba mabo yangekuwa mazuri.

Mkoa wa Singida ni moja ya mikoa inayopata mvua moja kubwa kwa mwaka, na hali yake ni ya ukame kiasi ingawa mvua zinaweza kuwa kubwa zikiambatana na upepo ambao pia huleta madhara kama ya kuharibu mazao na makazi ya watu, mabadiliko tabia nchi yamesababisha kuwe na mvua zisizotabirika na tume shuhudia mara kadhaa zikiwa chini ya kiwango. mkoa huu pia umeathirika na ukataji miti kwa ajili ya kuni, mkaa na matumizi mengine, na pia ufugaji uliokithiri umesababisha uharibifu wa udongo na kusababisha mmong'onyoko wa udongo kwenye baadhi ya sehemu. kwa sababu hizi na nyinginezo zote kwa pamoja zimesababisha madhara kwenye mfumo wa kilimo uliozoeleka na wenyeji wa mkoa huu.



USHAURI
1 - Wakulima walime mahindi kwenye sehemu zilizo tambarare na kwenye mabonde ambako unyevu unachelewa kukauka na wasilime mahindi kwenye uwanda wa juu na milimani kwani sehemu hizo ndizo zinafaa kwa mazao ya kinga ya njaa

2 - Matumizi ya kanuni za kilimo kilimo bora yazingatiwe kama kutumia mbegu bora za mahindi zinazokomaa muda mfupi za zinazoendana na hali ya hewa ya Singida, matumizi ya mbolea za samadi, viuatilifu salama n.k

3 - Upandaji wa mbegu kwa wakati, na kwa kufuata majira ya hali ya hewa, hii ni baada ya kufuata ushauri wa watabiri wa hali ya hewa, hili la hali ya hewa lifanywe na Mbunge akishirikiana na Mkuu wa Mkoa, yaani wafuatilie na wawaeleze wakulima muda sahii wa kuandaa mashamba na kuanza kupanda (wasilete siasa hapa)

4 - Viongozi wa siasa wakae na wakulima/maafisa kilimo na kushauriana nao kuhusu kilimo kwa ujumla, ikiwezekana wasaidie kuanzia upatikanaji wa mbegu bora watakazozichagua kwa pamoja, madawa ya kuua wadudu na taarifa za wadudu au magonjwa ya mazao ili kuzuia kusambaa (wanasiasa wasikae maofisini sana ila watembee kwenye himaya zao kujua matatizo)

1 comment:

Anonymous said...

mbona umepotea ndugu? wapenzi wa blog hii tuna kiu ya kupata mambo mapya.