KURASA

Tuesday, May 8, 2012

UUNGAJI WA MICHE YA MATUNDA


Kuchagua matunda ya mlimao kutoka kwenye mti mama
Chagua na kuvuna malimao yaliyoiva vizuri.Usitumie malimao yaliyooza.
Miche ya milimao ndiyo imekuwa ikitumika sana kama miche shina kwa ajili ya kuunganisha michungwa na miti ya matunda ya jamii yake kama vile michenza, midimu, madalanzi, mawashington nk. 
Aina nyingine ya mmea shina kwa ajili ya kuunganisha michungwa na miti ya matunda ya jamii yake ni Karizo na Volkameriana. Aina hizi bado ni ngeni kwa watu wengi.

Kukamua na kundaa mbegu za malimao.
Kata tunda kwa mzunguko bila kuingiza kisu hadi katikati ya tunda ili kuepuka kukata mbegu. • 
Kamua mbegu zote kutoka kwenye tunda na ziweke kwenye chombo kisafi.Safisha mbegu ili kutoa utelezi wote (utelezi unazuia uotaji mzuri wa mbegu). • 
Chagua nbegu zinazozama kwenye maji kwani mbegu zinazoelea juu ya maji hazioti. • 
Mbegu za malimao zipandwe mara tu baada ya kusafishwa kwani kwa kufanya hivyo mbegu zinaota vizuri zaidi kuliko mbegu zinazokaushwa kwanza kabla ya kupanda.

Kuandaa tuta na kupanda mbegu za malimao
Andaa tuta lenye kimo cha sentimeta 20. Tumia udongo unaopitisha maji kwa urahisi ( udongo wa kichanga au mchanga wenyewe ni bora zaidi). Sawazisha vizuri sehemu ya juu ya tuta.

Kupanda mbegu za malimao:
Weka alama za mistari kwenye tuta kwa nafasi ya sentimeta kumi (10) mstari hadi msitari (alama hizo ziwe na kina cha sentimeta moja na nusu (1.5) hivi. Panda mbegu kwa kuzidondosha moja moja kwenye mstari kwa nafasi ya sentimeta moja (1). Fukia mbegu kwa kurudishia udongo wa pembeni ya mstari. Mbegu za limao zinaota siku ishirini na nane au zaidi toka siku ya kupandwa.


Kupandikiza miche shina ya milimao
Miche ya milimao ina pandikizwa ikiwa na majani mawili yaliyokomaa. Jaza udongo kwenye kiriba ukiacha nafasi ya sentimeta mbili juu kwa ajili ya kumwagilia maji. Ng'oa miche bila kuharibu mizizi. 
Pandikiza miche iliyo bora tu. Tumia kijiti au kifaa maalumu kuweka shimo katikati ya kiriba. • 
Weka mche kwenye shimo na shindilia udongo vizuri. 
Zingatia kwamba mmea unaweza kuathirika endapo udongo utafukiwa juu sana ya sehemu linalotenganisha mizizi na shina.

Kutunza miche shina ya mlimao
Ondoa matawi ya pembeni kila mara yanapojitokeza.Dhibiti wadudu na magonjwa kila vinapojitokeza. 
Miche wa mlimao inakuwa tayari kwa kuunganishwa inapofikia umri wa miezi sita (6) hadi miezi tisa (9) (hutegemea matunzo). Mche unakuwa kwenye hatua nzuri ya kuunganishwa unapofikia unene wa penseli.

NAMNA  YA UUNGANISHAJI MICHE JAMII YA MICHUNGWA
KWA KUTUMIA MKATO WA HERUFI T





KWA KUTUMIA KIPANDE




Kutunza miche iliounganishwa
Mwagilia maji mara kwa mara kuhakikisha kuna unyevu wa kutosha wakati wote.
Ondolea machipukizi chini ya sehemu iliyounganishwa ili chakula cha mmea kitumike kwenye sehemu ya juu
iliyounganishwa tu
Baada ya siku 14 hadi 21 mmea huwa tayari umesha ungana na mara nyingine vitawi kuchipua.
Kwa miche ya jamii ya michungwa huu ni wakati wa kufungua utepe/plastiki.
Kwa miche ya miembe baada ya kitawi kuchipua na kufikia majani manne yaliyokomaa ondoa utepe /plastiki kwa kuifungua polepole (utepe unaweza kufunguliwa mapema endapo utakuwa unaonekana kuuzuia mche kukua).
Tangu kubebesha hadi kupandikiza huchukua wastani wa miezi 3 hadi 6.
Ni vema kupandikiza mwanzo wa majira ya masika.
Mti uliobebeshwa unauwezo wa kutoa maua wakati wowote baada ya kuunga. Lakini si vema kuuruhusu uzae mapema kwani utadumaa.
Mti uruhusiwe kuzaa baada ya kupata ukubwa wa kutosha Kwa hali ya kawaida hii ni baada ya miaka mitatu.

Wadudu na magonjwa ya miche ya mitunda kitaluni
Wadudu na viumbe wengine jamii ya buibui, jamii ya minyoo wadogo wadogo na magonjwa vinavyoweza kuleta madhara kwa miche kwenye kitalu.

Wadudu waharibifu
i. Chawa mfuta
Hushambulia miche ya milimao, miembe na mchungwa kitaluni na bustanini.
Hufyonza utomvu kutoka sehemu changa za mmea na majani.
Wadudu hawa hutoa maji maji yenye sukari ambayo huvutia vimelea vya ukungu mweusi kutokea kwenye
majani na hivyo kuathiri shughuli za utengenezaji wa chakula cha mmea.

Kuzuia
Kuna wadudu wadogo wadogo wenye umbo la kobe wanaokula chawa mafuta. Jamii hii ya wadudu huonekana pia kwenye maboga.
Kama wadudu hawa wanaleta madhara unaweza kutumia dawa za kuulia wadudu kama vile Endosulfan (Thiodan), Diaziozon, Fenitrothion, Karate na Decis.
Pia tumia mbegu za mwarobaini zilizosagwa na kuchangaywa ndani ya maji pamoja na sabuni ya unga.
Matunda ya mti huu yameonyesha kupunguza kwa kiasi kikubwa wadudu wa aina hii.

ii. Viwavi wa majani ya mitunda jamii ya michungwa
Mama wa kiwavi huyu ni kiepeo mkubwa mwenye rangi nyeusi pamoja na mabaka meupe. Kipepeo jike hutaga
mayai kwenye majani na baada ya mayai kutotolewa viwavi hutokea. Huwa ni wadogo wenye rangi ya udongo ama kijani na alama nyeupe mgongoni. Viwavi hawa hutoa vitu kama pembe mbili kichwani za kutishia maadui na hutoa harufu mbali wanapobugudhiwa

Madhara
Viwavi hawa hula majani machanga kwenye miche. Huweza kusababisha miche kunyauka kwa kukosa majani hasa kwa miche midogo ya michungwa.

Kuzuia
Kagua miche mara kwa mara na kuwaondoa kwa mkono na kuwauwa au tumia dawa za kuulia wadudu kama vile Endosulfan, Diazonon na Fenitrothion.

iii. Viwavi waharibifu wa majani
Hawa ni viwavi wanao kula majani na kuweka alama zinazofanana na mifereji au mistari ndani ya jani. Jani lililo shambuliwa na mdudu huyu huonyesha michoro ya njia ndani ya jani alimo pita mdudu. Mama wa viwavi hawa ni nondo. Viwavi hawa ni wadogo na wembamba kiasi kuwa hula sehemu ya katikati ya jani na huacha
ngozi yenye rangi ya fedha. Jani linaonyesha alama kama michoro ya vinjia vingi alimo pita funza. ushambulia majani machanga na husababisha jani kujikunja na kuathiri kazi ya utengenezaji chakula cha mmea.

Kuzuia
Dawa - diazinon, fenitrothion, thionex, karate, decis, n.k.

iv. Mdudu anayefyonza majani machanga ya miembe.
Mdudu mkubwa ana rangi nyeusi kwenye mabawa na mwili wake una rangi nyekundu. Ana pembe ndefu kuzidi urefu wa mwili wake. Wadudu wakubwa na wadogo hushambulia mimea kwa kufyonza na hivyo kuingiza/kueneza sumu inayosababisha sehemu zilizofyonzwa kufa.

v. Wadudu wanaofyonza maji maji kwenye matawi na majani ya miche
Wadudu hawa hufunikwa na utando mweupe kama nta. Wadudu wakubwa na wadogo hufyonza chakula cha mmea kwenye mashina, matawi na majani ya miche na hata miti mikubwa ya matunda jamii ya michungwa. Wadudu hawa hufuatwa sana na sisimizi kwa vile wanatoa maji yenye sukari ambayo husababisha ukungu mweusi ambao hufanya matawi na majani kuonekana kama yamepakwa masizi.

Kuzuia
Zuia sisimizi ambao huwafuata wadudu hawa, kwani sisismizi huzuia maadui asili wa hawa wadudu wasiweze kuwashambulia.
Tumia dawa za aina ya – Diazinon au Endosulfan ili kuwaua.

vi) Panzi (Mburumundu)
Panzi hawa wanaweza kuleta madhara makubwa pindi wanapokuwa wengi katika kitalu. Kwani aina hii ya panzi hula majani ya miche na miti midogo iliyopandikizwa shambani hasa wakati wa kiangazi.
Kuzuia
Kuwatoa kwa mkono au fimbo na kuwauwa.
Nyunyizia Mafuta ya taa;
Dawa:- Fenitrothion

vii) Nyenyere
Ni vidudu vidogo jamii ya buibui.Viumbe hawa hushambulia majani ya miche na miti mikubwa
na matunda.Nyenyere hushambulia sana miche hasa wakati wa kiangazi na kipindi chenye joto kali

Kuzuia
Kama mshambulizi ni makubwa tumia dawa - Malathion, dicofol.

Minyoo wadogo wadogo
Minyoo hawa hushambulia mizizi ya miche na miti mikubwa ya mitunda jamii ya michungwa.
Ni vizuri kubadilisha mchanga/udongo au kikuzia mimea mara kwa mara kwenye kitalu cha kuoteshea miche.
Endapo si rahisi kufanya hivyo tumia dawa kama vile furadan au unga wa matunda ya mwarobaini kabla ya kuotesha tena miche sehemu hiyo hiyo.

Magonjwa ya Mitunda jamii ya michungwa shambani
i) Vidonda katika shina
Huletwa na aina fulani ya ukungu. Dalili za ugonjwa huu ni kutokea sehemu ya shina ambayo hubadilika rangi.
Huongezeka ukubwa na baadaye kutoa utomvu. Ugonjwa huu hutokea sana kwenye sehemu iliyo na udongo ambao hutuamisha maji.

ii) Ugonjwa wa kukauka miti
Husababishwa na virusi ambavyo husambazwa na chawa weusi. Ugonjwa huu hujionyesha kwa dalili zifuatazo:-
Kwa mitunda kama dalansi na ndimu sehemu ya shina, ganda hunyauka na ndani yake hutokea mipasuko pasuko. Kisha mmea hudhoofika pole pole na hutoa matunda madogo madogo. Majani ya mitunda hubadilika ghafla na kuwa njano. Dalili hizi hutokea kutegemea aina ya mche-shina na kikonyo vilivyotumika. Mche shina unaoweza kustahimili ugonjwa huu ni limao, mchungwa na michenza aina ya cleoptra.

iii) Ugonjwa wa kutobadilika rangi kwa machungwa
yanapokomaa
Ugonjwa huu hutokea hasa katika sehemu za miinuko ya kati na husambazwa na vidudu viitwavyo psyllids, na vile vile kwa kuchukua vikonyo vya kubebeshea kutoka kwenye miti inayoonyesha dalili za ugonjwa.
Ugonjwa huu sio tishio sehemu za joto za nyanda za chini. Dalili za ugonjwa huu ni kama zifuatavyo: Kwenye majani hutokea mabaka ya rangi ya njano dalili kama vile mti uliokosa madini ya Zinc. Vile vile hutokea machipukizi ya kusimama yasiyo ya kawaida, matunda huwa ya ukali na hayabadiliki rangi kuwa njano yanapoiva.

Kuzuia
Sehemu ambazo ugonjwa unaweza kutokea angalia wadudu kama chawa. Hakikisha wadudu hawa hawashambulii miche kwenye kitalu. Wakiwepo, majani huonyesha kujikunja kwa kuweka mafundo sehemu ya juu. Vile vile epuka kuchukua vikonyo kutoka kwenye miti yenye dalili za ugonjwa huu.

iv)Nzi weupe wa kwenye mimea jamii ya michungwa
Hawa ni wadudu ambao hukaa kwenye  majani ya mimiea wakizaliana na kufyonza virutubisho vya mmea, na hii husababisha mmea kudumaa na kutoa mazao duni





Kuzuia
Nja ya kiusalama zaidi ni kwa kupandisha shambani wadudu aina ya Cales noacki ambao huwala hawa nzi weupe na kuzuia kusambaa kwao




 Magonjwa ya matunda ya miembe shambani
Ukungu wa majani Husababishwa na ukungu ambao kwenye majani hutokea alama enye rangi ya kahawia na halafu jani hujikunja na baadaye kudondoka.

Kuzuia
Tumia dawa ya ukungu - kama vile Benomyl.
Pulizia maji ya yaliyo changanywa na unga wa mbegu za muarobaini

5 comments:

Unknown said...

Hii blog ina elimu nzuri sana
Gingers sana kwa kazi nzuri

Unknown said...

Space ya michungwa na milimao ikoje

Unknown said...

Mlimao na ndimu huchukua muda gani kuanza kuzaa

Unknown said...

Nataka kufahamu namna ya kubebesha mchungwa

said...

Kwa zaidi ya miaka 13 ya ndoa sikuweza kuzaa, naendelea kuharibika hata nikipata mimba, madaktari wote hawakuweza kunisaidia, hadi dada yangu akanielekeza kwa Dr DAWN, ambaye alinisaidia nikapata ujauzito na sasa hivi kuwa na mtoto mzuri wa kike,
Anasaidia pia marafiki zangu wengi niliowaelekeza, Dr DAWN ni baraka kwa kila mtu anayewasiliana naye,
*Kama unataka kupata mimba.
*Ukitaka kuacha kuharibika kwa mimba.
*Ukitaka kumrudisha mpenzi wako.
*Kama unataka mume/mkeo arudishwe.
*Kama unataka kurejesha mali yako iliyoibiwa au Pesa.
*Ukitaka kutibu aina yoyote ya ugonjwa,
Wasiliana naye kwa WhatsApp: +2349046229159