KURASA

Tuesday, September 29, 2009

SEHEMU YA 4 - MATUNZO YA WATOTO WA NGURUWE




Kwa kawaida hunyonya kwa wiki 5 -8, na baada ya hapo hutengwa na mama yao na kuanza kupewa chakula chenye protini 25% kwa muda wa wiki 6 za mwanzo

KUKATA MENO
Mara baada ya kuzaliwa watoto wakatwe meno kwa kutumia mkasi mkubwa au kifaa cha kukatia waya (wire cutter) umuhimu wa zoezi hili ni kwa sababu nguruwe huzaliwa na meno na mara wanapoanza kunyonya huumiza chuchu za mama yao na kumsababishia ugonjwa wa chuchu (mastitis)

MADINI CHUMA
Wakizaliwa tu wanahitaji madini ya chuma kwa wingi, maziwa ya mama yanatoa kiasi cha 10% tu, huwa wanapigwa sindano (Iron Injection) kiasi cha 155mg kwa kitoto kimoja ili kuwaongezea madini ya chuma ya ziada, muone mtaalamu wa mifugo akusaidie kwa hili



KUHASI
Madume ambayo yatakuzwa kwa ajili ya nyama ni vizuri yakahasiwa, hii husaidia ukuaji wa haraka na pia huondoa harufu ya balehe, Zoezi hili lifanyike wakati wakiwa na wiki 2-3 inapofika wiki ya 5 zoezi huanza kuwa gumu kwa sababu watoto wanakuwa wakubwa na litahitaji sindano za ganzi, zoezi hili linahitaji mtaalamu wa mifugo.

MINYOO
Mzazi anapokaribia kujifungua wiki ya mwisho achomwe sindano ya kuondoa minyoo na magonjwa ya ngozi ijulikanayo kama IVOMEC SUPER au IVERMECTIN zinazopatikana kote nchini, dawa hii husaidia kuwalinda watoto na minyoo hadi wanapoacha kunyonya ndio na wao wapigwe sindano hii ambayo pia itasaidia kuua minyoo ya mapafu, minyoo ya macho, viroboto na kuondoa ukurutu.



CHAKULA
Baada ya wili chache vitoto vitaanza kula chakula kidogo kidogo kwa kuanzia na kile anachopewa mzazi, hakikisha mzazi anapewa chakula kingi na chakutosha kwa sababu atakuwa anakula yeye na watoto wake

KITIMOTO SEHEMU YA 3 - NGURUWE JIKE (MZAZI)

UCHAGUZI
Yawe na chuchu zisizopungua 18 na chuchu ziwe nene na ndefu, chuchu fupi na ndogo huleta matatizo wakati wa kunyonya , kumbuka mtoto wa nguruwe chuchu atakayo nyonya siku ya kwanza ndiyo hiyo hiyo atakayonyinya mpaka atakapoacha kunyonya
Awe na miguu ya wastani yenye nguvu na isiwe na kasoro kama matege au kukaa upande na kucheche mea, hii humsaidia kuhimili madume makubwa
Uke uwe na ukubwa wa kutosha na umbo la kawaida, pia upimwe na mtaalamu kwa kuingiza vidole na kuangalia kama wakati wa kuvitoa vina kwama kwama, hii huwa dalili ya majike dume (hermaphrodites)



CHAKULA
Maji yalishwe chakula cha kunenepesha mpaka yakifikisha uzito wa kilo 80, baada ya hapa yapewe chakula maalum cha wazazi ambacho kitasaidia wasinenepeane na kuwa na mafuta mengi kwenye njia ya uzazi

BANDA
Majike hukaa moja moja au mengi kwenye banda moja muda wote (kipimo ni 2.5m *1.5m ) kwa kila nguruwe kasoro tu yanapokaribia kuzaa ndio huhamishiwa kwenye banda la kuzalia

NGURUWE AKIWA KWENYE BANDA LA KUZALIA


UPANDISHAJI
Majike yapandishwe yakifikisha umri wa wiki 28 na uzito wa kati ya kilo 120 – 140, nguruwe aachwe mpaka aingie joto kwa mara ya 3 ndio apelekwe kwa dume ambapo kila baadda ya siku 21 nguruwe huingia kwenye joto

KUINGIA KWENYE JOTO
Dalili za joto ni guruwe kupiga kelele hovyona kuhangaika lakini ukimkandamiza kiunoni na mikono yako hutulia, uke huwa na rangi nyekundu na hutoa ute mweupe. Baada ya dalili za mwanzo nguruwe huwa tayari kupandwa baada ya masaa 38 – 42 na hudumu kwa masaa kama manne (4) inashauriwa ukiona tu dalili za mwanzo umpeleke jike kwenye banda la dume

MIMBA
Mimba huchukua siku 114 mpaka watoto kuzaliwa (miezi 3 wiki 3 siku 3) kipindi cha ujauzito nguruwe jike hula sana mpaka kiasi cha kilo 5 -7 kwa siku apewe mlo kamili lakini kuwe na umakini asinenepe sana na ikifika wiki ya mwisho ahamishiwe kwenye banda la kuzalia (furrowing pen)

BANDA LA KUZALIA


Liwe na ukubwa usiopungua 3m * 2m, liwe na sehemu ya watoto ambayo mama mtu hawezi kufika watoto waingie huko kwa kupenya, hii husaidia nguruwe asiweze kuwalalia watoto wake. Sehemu ya watoto iwe na chanzo cha joto kama vile jiko, hii husaidia kufundisha watoto wakimbilie kule muda wote

Friday, September 25, 2009

UFUGAJI WA NGURUWE - SEHEMU YA PILI

Sehemu ya pili ya maelezo kuhusu ufugaji wa nguruwe tuaangalia nguruwe dume ambaye ndiye atakuwa natumika kwa ajili ya kupandishia majike kwenye mradi wa nguruwe, wengine huwa wanatumia madume ya kukodi, lakini kama utakuwa na majike zaidi ya 10 utahitaji kuwa na dume kwenye mradi wako,

UCHAGUZI WA DUME
Dume litoke kwenye kizazi ambacho hakina historia ya magonjwa na wana historia ya kuzaa watoto wengi ,wenye afya bora, na ukuaji mzuri, angalia kizazi/ukoo wake uwe na chuchu nyingi zisizopungua 14 zikiwa 18 ni nzuri zaidi

BANDA LA DUME
Liwe na ukubwa usiopungua 3 m * 2.5m geti liwe lachuma na linafunguka kuelekea kwa ndani na nje pande zote mbili, siku zote majike ya pelekwe kwa dume na si kinyume chake.

CHAKULA
Dume alishwe kilo 2 – 3 za mlo kamili wenye kiasi cha wastani cha protini, epuka kumlisha mashudu mengi kwa sababu yana kuwa na kemikali inayojulikana kama omega 3 fatty acids ambayo hupunguza kiasi cha manii kwa nguruwe, tumia mimea kama lukina na desmodiam au dagaa kama chanzo cha protini

UPANDISHAJI
dume aina ya saddle back akimpanda jike aina ya landrace


Madume huanza kupanda yakifikisha umri wa miezi 12 – 14 hupanda jike moja mara 2 kwa siku na hupanda majike 6 kwa kila siku 8 na majike yasifululize kwa zaidi ya siku mbili zinazofuatana, majike yapelekwe asubuhi mapema kabla ya dume kula chakula
Dume linaweza kuendelea kutumika kwa upandishaji mpaka likifikisha miaka 3 – 4 ndipo unaweza kuanza kutumia dume lingine, uzoefu unaonyesha nguruwe chotara huwa na uwezo wa kupanda mara nyingi na kwa muda mrefu zaidi. Dume moja huweza kuhudumia majike 20 lakini kwa matokeo mazuri tumia dume moja kwa kila majike 15 – 18

UFUGAJI WA NGURUWE - SEHEMU YA KWANZA

Kutokana na maombi ya Bw John Mwaipopo kuhusu ufugaji wa Nguruwe na kuku, leo nimeamua kuanza kumuelezea njia bora na sahihi

AINA ZA NGURUWE (baadhi)
LARGE WHITE


-Hii ndiyo aina kubwa zaidi ya nguruwe wa kufugwa nyumbani
-Kama jina lake lilivyo ana rangi nyeupe mwili mzima
-masikio yake yamesimama wima
-Ana sura iliyobonyea kwa ndani (dish faced)

LANDRACE


-Weupe mwili mzima
-masikio yamelala kabisa
-Wana ukubwa wa wastani

SADDLEBACK


-Ni wakubwa
-Wana rangi nyeusi na mstari mweupe kuzunguka shingo na miguu ya mblele
-Masikio yamelala kiasi


DUROC

Asili yao inatoka tangu mwaka 1812 katika majimbo ya New York na New Jersey ambako ndio walizalishwa kwa mara ya kwanza ingawa pia kuna tetesi kwamba waliletwa toka Uingereza

Wana rangi ya kahawia iliyooza mpaka iliyopauka na kutaka kuwa kama njano, wana masikio yaliyolala kwa mbele na sura ndefu ilyonyooka, wana nyama tamu sana na isiyo na mafuta mengi, ni Mbegu inayotumika Zaidi kwenye kuchanganya na Mbegu nyingine ili kupata uzao wenye nyama tamu na yenye mafuta kidogo, Madume ndio hutumika kwenye kupanda majike ya Mbegu nyingine kama Large White na Lamd race sababu ni kwamba majike ya Duroc hayazai watoto wengi

CAMBOROUGH

Hii ni Mbegu mpya ambayo inatokana na Mbegu za Large white na Land race ambao walichanganywa kitaalam  ili kupata sifa za uzazi wa watoto wengi, ukuaji wa haraka, kutumia chakula vizuri, uzalishaji maziwa wengi kwa ajili ya watoto, sifa ya kipekee ni uwezo wa majike kuendelea kuzaa kwa miaka mingi zaidi ukilinganisha na wengine.


Wana rangi nyeupe tupu, masikio yamelala kidogo kwa mbele na wana uso mrefu ulioonyooka, wana uzazi wa wastani watoto 14 na majike huanza kupandwa wakiwa na miezi 8 tu

Tuesday, September 22, 2009

KILIMO KWANZA

AZIMIO LA KILIMO KWANZA


KWA KUWA Baraza la Taifa la Biashara (TNBC), chini ya Mwenyekiti wake Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lilifanya mkutano tarehe 2 na 3 mwezi Juni 2009 jijini Dar es Salaam, kujadili sera na mikakati ya kuleta mapinduzi ya kilimo cha Tanzania pamoja na utekelezaji wake chini ya kaulimbiu ya “KILIMO KWANZA”;


NA KWA KUWA asilimia themanini ya Watanzania hutegemea kilimo kwa ajili ya kuendeleza maisha yao;


KWA KUTAMBUA KUWA changamoto kubwa kwa Tanzania ni kupambana na umaskini na kwamba hili litawezekana hasa kwa kuongeza tija katika kilimo;


KWA KUZINGATIA KUWA Tanzania imejaaliwa kuwa na rasilimali za kutosha kwa ajili mazao, mifugo na uvuvi, ambazo kwa sasa matumizi yake yapo chini;


KWA KUFAHAMU KUWA Tanzania ni nchi ya pili barani Afrika kuwa na kiasi kikubwa cha maji kinachoweza kutumika kwa kilimo cha umwagiliaji pamoja na ufugaji;


NA KWA KUTAMBUA KUWA jitihada za makusudi zimekuwa zikichukuliwa ili kuboresha kilimo bila mafanikio yakuridhisha;



HIVYO IMEAZIMIWA KWAMBA:

1.KILIMO KWANZA iwe ndiyo dhana ya kuleta mapinduzi ya kijani kwa lengo la kukifanya kilimo cha Tanzania kuwa cha kisasa na cha kibiashara;

2.Dhana ya KILIMO KWANZA ijumuishwe kwenye mipango mbalimbali ya Serikali ili kuhakikisha mafanikio ya utekelezaji wake;

3.Jitihada zifanyike katika kuongeza rasilimali mbalimbali ili kufanikisha utekelezaji wa KILIMO KWANZA;

4.Sekta binafsi ihamasishwe ili iongeze uwekezaji kulingana na wajibu wake katika utekelezaji wa KILIMO KWANZA; na

5.Utekelezaji wa KILIMO KWANZA utaongozwa na nguzo kumi zifuatazo:

I. Utashi wa kisiasa kutoa msukumo wa mapinduzi ya Kilimo.
II. Kugharamia mapinduzi ya Kilimo
III. Uboreshaji wa mfumo wa utawala wa kilimo.
IV. Mabadiliko ya mfumo mkakati katika kilimo.
V. Upatikanaji wa ardhi kwa ajili ya kilimo.
VI. Vivutio vya kuchochea uwekezaji katika kilimo.
VII. Uendelezaji wa viwanda katika kuleta mapinduzi ya kilimo.
VIII. Sayansi, Teknolojia na Rasilimali Watu katika kuwezesha mapinduzi ya kilimo.
IX. Uendelezaji wa Miundombinu ili kuwezesha mapinduzi ya kilimo.
X. Uhamasishaji na ushirikishwaji wa Watanzania kuunga mkono na kutekeleza KILIMO KWANZA.

Friday, September 18, 2009

NYUNGUNYUNGU JINSI YA KUWAKUZA KWA AJILI YA CHAKULA CHA SAMAKI

Kuna msomaji mmoja wa Zanzibar Bwana Ali Makame Juma (POLO) wa mahinda kaskazini B, ambaye alifurahishwa na maelezo ya ufugaji wa samaki na akaniomba nimwelekeze pia uzalishaji wa nyungunyungu



MAHITAJI
Nyungunyungu
Chombo cha kufugia
Udongo wa juu (top soil)
Mahindi (dona)
Majani makavu

JINSI YA KUFANYA

(A) Andaa chombo chako ambacho hakivuji mfano sinki la bafu, pipa la plastiki (likatwe nusu)
(B) Jaza udongo kiasi cha inchi 4 – 8 kwenye chombo
(C) Weka inchi moja ya majani makavu
(D) Weka mchanganyiko wa dona na vegetable shortenings
(E) Weka nyungunyungu
(F) Funika juu
(G) Ongeza mchanganyiko wa dona na vegetable shortenings baada ya mwezi mmoja na kila baada ya wiki mbili weka 1qt ya maji kila unapoongeza mchanganyiko huu
(H) Weka chombo chako pasipo na mwanga wa jua



KUKUZA NYUNGUNYUNGU KWA AJILI YA CHAKULA CHA SAMAKI NA MBOLEA
MAHITAJI

(a) nyungunyungu
(b) Mabaki ya jikoni/chakula
(c) Kinyesi cha mnyama ambaye hajatoka kupewa dawa za minyoo
(d) Ndoo 3 zenye matobo nusu sentimeta

JINSI YA KUFANYA
(a) Tafuta minyoo kutoka eneo ulilopo, chimba chini au kwenye vinyesi vya wanyama vilivyo lundikana, usi chukue minyoo wa sehemu nyingine kuzuia kuvamia mazingira mapya na kubadili mfumo wa maisha ya viumbe (biodiversity)
(b) Ndoo moja weka minyoo, ya pili weka mabaki ya jikoni nay a tatu iwe tupu
(c) Zipange kwa mpangilio huu ya chini iwe tupu, ya kati iwe na minyoo na ya juu iwe na mabaki ya chakula
(d) Ndoo ya juu ijazwe mabaki ya chakula mpaka juu, na inyunyuziwe maji kidogo kufanya mabaki yawe na unyevu, maji mengi yataua minyoo.
(e) Baada ya muda minyoo itapanda kwenye ndoo ya juu na kuanza kula chakula, chakula kikipungua na kubakia theluthi mbili, toa ndoo ya chini utakachokikuta ni mbolea uiweke bustanini/shambani na uiweke juu
(f) Ndoo yenye minyoo ambayo sasa iko chini itabaki na chakula kidogo na baadhi ya minyoo, minyoo irudishe ndoo ya kati ambayo mwanzo ilikuwa na chakula sababu minyoo mingi itakuwa huko
(g) Ndoo ya juu ijazwe na mabaki ya jikoni tena na endelea na mzunguko huu kwa muda wa miezi 3 minyoo itakuwa mingi tayari kwa ajili ya kulisha samaki
(h) Katikati ya zoezi hili unaweza kutumia baadhi ya minyoo kwa ajili ya kupandishia zamaki (breeding) kumbuka kuweka ndoo hizi kwenye kivuli wakati wote



NJIA NYINGINE RAHISI
Chukua kiroba cha katani na weka pumba za mahindi kama kilo 5 ziloweshe na maji kodogo, tafuta kwenye shina lamigomba mikubwa, chimba pembeni yake na uzike gunia lako, hakikisha mgomba wako haumwagiliwi na maji ya sabuni hata kidogo na wala hauwekewi kemikali yoyote. Acha gunia lako kwa muda wa mwezi mmoja nenda kachimbe ukiwa umevaa gloves za shamba pekua pekua na utakuta nyungunyungu kibao wamezaana, hamisha na ulishe samaki wako, endelea kuvuna kila baada ya mwezi mmoja na kuongeza pumba nyingine kiasi
Hii njia inafaa zaidi kwa ajili ya wale wanaohitaji nyungunyungu kidogo tu kwa ajili ya kulisha samaki wanaopandishwa (breeding stock)

Wednesday, September 16, 2009

HOLSTEIN FRIESIAN - kinara wa utoaji maziwa duniani



ASILI YAKE

Uholanzi katika jimbo la friesland

UZALISHAJI KWA MWAKA
10,158 kg za maziwa
3.64% mafuta
3.05% protini

RANGI
nyeupe na nyeusi, mkia huwa na rangi nyeupe na kwenye paji la uso huwa na rangi nyeupe yenye umbo kama la pembe tatu ,mara chache (1/1000) huzaliwa ndama mwenye rangi nyekundu na nyeupe

UZITO
kilo 1200 majike
kilo 1400 madume



Huyu ndiye aina ya ng'ombe anayeshikilia rekodi ya uzalishaji maziwa kwa kiwango cha juu, maziwa yake hayana mafuta mengi. Nimeshuhudia akitoa maziwa zaidi ya lita 70 kwa siku kwa mikamuo mitatu lita 30 / 20 / 25 Madume yanatumika kwa kulimia na kukokota mikokoteni, Ni mkubwa kushinda nyati ambaye ana uzito wa kilo 800-1000, kama wanavyoonekana kwenye picha urefu wao ni sawa na kimo cha mtu mwenye urefu wa wastani. Kwa Tanzania wanapatikana zaidi Kitulo mkoani Iringa na Uyole (kituo cha utafiti wa kilimo) Mkoani Mbeya, aina hii ya ng'ombe hustawi zaidi katika mazingira yenye baridi kali.

Kama unataka mbegu hii wasiliana na maafisa ugani wa mifugo ili waje kupandisha ng'ombe wako kwa njia ya chupa, mbegu zinazotumika kwa njia hii hutoka kwa madume PURE BREED CLASS A na matokeo yake ni kupata ndama bora

Saturday, September 12, 2009

MAZIWA - Jinsi ya kufahamu kama yameongezewa maji

Ubora wa maziwa hupimwa kwa njia nyingi, kwa mfano harufu ilikugundua kama ng’ombe alitumia dawa yoyote, pia kwa kuangalia unaweza kujua kama maziwa hayana rangi ya kawaida, na kwa vipimo maalum zikiwemo kemikali ili kujua kama maziwa yana ubora usio faa (maziwa hayapimwi kwa kuonja)



Mara kadhaa wafugaji wamekuwa wakiongeza maji kwenye maziwa ili kuweza kujipatia kipato zaidi na hii huwa ni hasara kwa mlaji. Kwa kawaida kuna kipimo kinachojulikana kama LACTOMETER, hiki ni kipimo ambacho kinaweza kutambua kama maziwa yameongezwa maji. Lactometer hutumiwa kwa kuweka maziwa kwenye chombo maalum cha maabara kama test tube na beaker , koroga ili kuyeyusha mafuta ya kwenye maziwa na kisha lactometer hutumbukizwa kwenye maziwa, maziwa mazuri lactometer itasoma kati ya 1.026 – 1.036 tofauti na hapo maziwa yatakuwa yameongezwa maji au kitu kingine, kwa kawaida kwenye maziwa huwa kuna protini, mafuta, maji , chumvi chumvi na sukari (lactose)

Kifaa hiki kinaweza kudanganywa kwa kuongeza sukari, ngano au maziwa ya kopo na kikasoma kwamba maziwa hayajatiwa maji, kwa sababu jinsi lactometer inavyoelea zaidi ndivyo maziwa yanaonekana bora zaidi (hayaongezewa maji)
Kama huna kipimo cha lactometer wala usiwe na wasiwasi wa kuyapima maziwa maana kuna njia za kienyeji ambazo zitakupa matokeo mazuri tu kama au zaidi ya lactometer

NJIA YA KWANZA


Chukua kibiriti toa njiti moja na uichovye kwenye maziwa (haraka) na kisha kuiwasha haraka haraka, kama maziwa hayajaongezwa maji njiti itawaka kama kawaida na kama kuna maji njiti haitawaka au itawaka kidogo na kuzimika hapo hapo kutegemeana na kiasi cha maji yaliyongezwa.


NJIA YA PILI



Mwaga tole la maziwa kwenye mkono wako kasha liache lile tone litirike na kumwagika chini, ukiangalia mule yalikotiririka maziwa utoana yameacha njia yenye rangi nyeupe, hii ni kwa maziwa halisi, na maziwa yaliyoongezwa maji yataacha njia nyeupe ambayo imepauka. Njia hii inahitaji uzoefu kidogo na unaweza kujizoesha kwa kununua maziwa ukayagawanya sehemu mbili na kisha sehem u moja kuyachanganya kiasi na maji, halafu mimina maziwa kutoka sehemu zote mbili na uangalie tofauti yake



TAHADHARI

Kwa wale wanaofuga ng'ombe aina ya Friesian (pure breed) wakati wa mvua nyingi kama ngombe wako utamlisha majani machanga tu bila ya majani makavu na pumba zenye virutubisho, basi maziwa atakayotoa yakipimwa kwa kutumia vipimo hivi yataonekana kama yameongezwa maji, ingawa ki ukweli ni kwamba hayaongezwa kitu chochote

Sunday, September 6, 2009

HOMA YA BONDE LA UFA- tishio kwa wanyama na binadamu

1.UTANGULIZI

Ugonjwa wa Homa ya Bonde la Ufa (Rift Valley Fever) kupitia vyombo vya habari na kupitia Shirika la Afya ya Wanyama Duniani (OIE) umeripotiwa kulipuka mara kwa mara katika eneo letu la Afrika ya Mashariki hasa katika nchi jirani ya Kenya. Ugonjwa huu, kama jina lake linavyoonyesha hutokea kwenye nchi zenye bonde la ufa na Tanzania ni mojawapo ya nchi hizo. Ugonjwa hutokea baada ya mvua nyingi na mafuriko yanayofuatia kuwepo kwa ukame wa muda mrefu.

Uchunguzi wa “remote sensing” uliofanywa na Shirika la Kilimo na Chakula Duniani (FAO) unaonyesha kuwa maeneo yaliyo na hatari zaidi ya kuambukizwa na ugonjwa ni pamoja na Kenya, Kusini mwa Somalia, Kusini na Kusini Mashariki mwa Ethiopia, Kusini mwa Sudan na Kaskazini mwa Tanzania.



2.HISTORIA YA UGONJWA

Ugonjwa wa Homa ya Bonde la Ufa (Rift Valley Fever) katika nchi ya Kenya umefahamika kwa zaidi ya miaka 60 iliyopita. Ugonjwa unaofanana na Homa ya Bonde la Ufa ulionekana mara ya kwanza nchini Kenya mwaka 1913. Tangu wakati huo matukio makubwa ya ugonjwa yameonekana katika nchi nyingi za Bara la Afrika ikiwa ni pamoja na Misri, Sudan, Somalia, Kenya, Msumbiji, Nigeria, Senegal, Tanzania, Uganda, Zambia, Zimbabwe, Namibia na Afrika ya Kusini.
Nchi ya Misri ilikumbwa na ugonjwa huu mwaka 1977 na 1978 ambapo watu wapatao 18,000 waliugua na 598 walikufa. Nchi ambazo taarifa zilitolewa za matukio ya ugonjwa huu nje ya Bara la Afrika ni pamoja na Yemen na Saudi Arabia. Kwa hapa Tanzania ugonjwa huu ulionekana mwaka 1979 na 1998 katika mikoa ya Mara, Arusha na Kilimanjaro ambapo ng’ombe, Mbuzi, kondoo na ngamia waliathirika.

3.VISABABISHI VYA UGONJWA NA JINSI UNAVYOENEA


Ugonjwa wa Homa ya Bonde la Ufa (Rift Valley Fever) unasababishwa na virusi viitwavyo Phlebovirus na ambavyo kitaalam vimewekwa katika familia ya Bunyaviridae. Virusi hivi huweza kuishi kwenye mayai ya mbu aina ya aedes, ambayo yana tabia ya kuishi kwenye vumbi kwa muda mrefu na kuanguliwa wakati wa mafuriko. Baada ya kuanguliwa mbu hawa husambaza ugonjwa kwenye mifugo na kwa watu wakati wanapofyonza damu. Mbu aina nyingine kama vile Culex, Mansonia, Anopheles, na Eretmapodites wanaweza kusambaza virusi vya ugonjwa kati ya wanyama na wanyama na kati ya wanyama na binadamu.



Lakini zaidi ya kupata ugonjwa moja kwa moja toka kwenye mbu binadamu wanaweza kupata ugonjwa kupitia kugusa damu au majimaji ya aina nyingine ya wanyama wakati wa kuchinja, kuzalisha wanyama wagonjwa, kushika vitoto vya mbuzi au kondoo vilivyokufa.

Aidha binadamu wanaweza kupata ugonjwa kutokana na kula vyakula visivyopikwa vizuri vitokanavyo na wanyama wagonjwa au wenye virusi.


4.DALILI ZA UGONJWA

4.1.Dalili kwa mifugo
Ugonjwa huu huwapata ng’ombe, mbogo, kondoo, Mbuzi, ngamia na binadamu. Ugonjwa huonekana zaidi kwenye maeneo ya watu wenye mifugo mingi. Dalili za kwanza katika wanyama ni kutupa mimba kwa wingi hususan katika kondoo na ngamia na vifo vingi vya ghafla kwa karibu asilimia 90 ya mbuzi na kondoo wachanga. Kwenye mbuzi na kondoo wakubwa dalili za ugonjwa ni pamoja na kutapika, kutokwa makamasi yenye damu na kuharisha, rangi ya njano kwenye ngozi ya ndani inayofunika macho, midomo na sehemu za uzazi na vifo katika asilimia 10 hadi 20 ya wanyama hawa. Ng’ombe hawaugui sana kama ilivyo kwa mbuzi na kondoo.

4.2.Dalili kwa binadamu
Dalili za ugonjwa kwa binadamu ni pamoja na kuumwa kichwa, kuumia macho wakati yanapoangalia mwanga mkali, mafua, homa kali, tumbo kuuma, kutapika na wakati mwingine kutapika damu. Virusi huchukua muda wa siku mbili hadi sita tangu kuingia mwilini hadi kuanza kuonyesha dalili na ugonjwa unaweza kusumbua kwa muda wa siku tatu hadi saba au zaidi. Vifo kwa binadamu vinaweza kutokea baada ya virusi vya ugonjwa huu kushambulia ubongo na viungo vingine vya mwili ambapo husababisha kuvuja damu.




5.KINGA NA NAMNA YA KUUEPUKA

Kama ilivyokwishaelezwa Ugonjwa wa Homa ya Bonde la Ufa unasababishwa na virusi na unaenezwa na mbu. Kwa hiyo njia mojawapo ya kuzuia mifugo isipate ugonjwa ni kuiogesha au kuinyunyizia dawa aina ya pyrethroids ambazo ni pamoja na Flumethrin, Deltamethrin na Alphacypermethrin. Dawa hizi tayari ziko nchini na zinatumika kuogeshea mifugo ili kuikinga isishambuliwe na kupe au mbung’o na zinaweza kutumika pia ili mifugo isishambuliwe na mbu.

Njia ya kuzuia binadamu wasipate ugojwa huu ni kutumia vyandarua. Pia wananchi wanaweza kuepuka ugonjwa huu kwa kupika vizuri vyakula vitokanavyo na mifugo. Wizara inashauri wananchi wachukue tahadhari hizi hata kama ugonjwa haujaonekana popote nchini kwa sababu kinga ni bora kuliko tiba.

Sunday, August 30, 2009

MIKARATUSI NA UKWAJU - TIBA YA KIFUA

Mikaratusi na ukwaju ni tiba yenye nguvu dhidi ya kifua na kukohoa, tiba hii ni rahisi kuandaa na haina gharama.



UAANDAAJI
Chukua jani moja au zaidi ya mkaratusi lililokomaa kutoka katika matawi machanga/mapya ya mti, ponda ponda na uchuje kwenye maji kiasi cha mililita 100-200, unaweza kutumia blender pia kusagia dawa hii, kisha changanya na juisi ya ukwaju, pia unaweza kuongezea tangawizi kidogo ukipenda.


MATUMIZI
Kunywa mchanganyiko huu mara 3 kwa siku kwa siku 3-5
Ukitumia mchanganyiko huu mara moja kwa wiki ni kinga tosha kwa magonjwa ya njia ya hewa



MUHIMU Ukichemsha majani ya mkaratusi chumbani na kuacha mvuke usambae chumbani ni kinga tosha juu ya mafua, pia huleta harufu nzuri chumbani (air freshener)

Monday, August 17, 2009

MBAAZI- cajanus cajan

Pamoja na kuwa ni chakula tulichokizoea sana, lakini mmea huu pia ni dawa ya magonjwa mbali mbali

MAANDALIZI

Chukua majani, maua au mizizi kiasi cha nusu kilo (ni vizuri kama utachanganya vyote) pondaponda na uloweke kwenye maji safi kiasi cha lita 2 kwa muda wa masaa 24.


Chuja na uweke dawa hii mbali na jua/joto, ni vizuri kama ataweka kwenye friji, kunywa kikombe kimoja kutwa mara 3 kwa siku 3




TIBA

Dawa hii inaweza kutibu magonjwa yafuatayo

1-Inauwezo mkubwa wa kushusha homa

2-Husaidia kuponesha vidonda.

3-Husaidia kurekebisha mzunguko wa hedhi kwa wanawake.

4-Husaidia kupunguza uvimbe

5-Huponyesha kifua na kukohoa.

6-Husafisha kibofu/njia ya mkojo.

7- Huongeza kinga ya mwili dhidi ya magonjwa mbali mbali

Tuesday, August 11, 2009

TANZANIANS BLOGGERS SUMMIT



Je wewe ni mwanablogu (Blogger) au mdau wa habari na mawasiliano kwa umma kwa kutumia mtandao? Kama jibu ni ndio, tafadhali unaombwa kujiorodhesha kwa ajili ya maandalizi ya Kongamano Maalumu la Kitaifa kwa ajili Wanablogu (Bloggers) na wadau wa habari na mawasiliano wa Tanzania (Tanzanians Bloggers Summit) linalotarajiwa kufanyika Desemba mwaka huu jijini Dar-es-salaam,Tanzania.

Dhumuni la kongamano hili ni Kuelimishana, Kufahamiana, Kuamsha Utambuzi Rasmi Kuhusu Tekinolojia ya Blogu na Mawasiliano ya Umma kwa Kutumia Mitandao, Kusaidia Utambuzi Rasmi juu ya mchango wa blogu nchini Tanzania kama chombo muhimu cha habari na mawasiliano, Kuelimishana jinsi gani blogu zinaweza kutumika katika kuleta maendeleo katika nyanja za kijamii, kisiasa na kiuchumi, kuburudisha, kukuza utamaduni nk.

Wataalamu mbalimbali kutoka ndani na nje ya nchi wataalikwa kutoa mada na mafunzo mbalimbali kuhusiana na tekinolojia ya kublogu, zana nyinginezo za mawasiliano mtandaoni kama vile mitandao jamii(social networking), online forums nk.Kutakuwa na vipindi vya maswali na majibu.
Ili kufanikisha maandalizi ya Kongamano hili la kihistoria, kujiorodhesha kwako ni muhimu sana. Muda wa kujiodhoresha ni kuanzia tarehe 12/8/2009 (Jumatano) mpaka 12/9/2009 (Jumamosi) tu.

Kinachohitajika ili kujiandikisha ni :
Jina Lako, Anuani yako ya barua pepe (E-mail), Mahali Ulipo au unapoishi (Nchi,mji nk),Namba ya Simu (sio lazima) na Anuani au URL(Universal Resource Locator) ya blogu yako (mfano www.kongamano.blogspot.com/wordpress.com/.com/typepad nk). Vyeti vya Ushiriki vitatolewa kulingana na habari utakazoziorodhesha hapa.
Unaweza kujiorodhesha kwa kutuma ombi lako kwa barua pepe kwenda; summit@bongocelebrity.com.

Zingatia tarehe za kujiandikisha.
Ni mwezi mmoja tu! Asante kwa ushirikiano. UMOJA NI NGUVU!

TEAK FOR SALE - MITIKI INAUZWA

SPECIE - tectona grandis (seed planted not cloned)

AGE - 18 years old

QUANTITY - 50 standing trees

LOCATION - Mahenge, Morogoro

CONTACT - mitiki1000@gmail.com

For serious buyer send your price offer & further negotiation will be made at the site

Monday, August 10, 2009

KICHAA CHA MBWA

KUSAMBAA

Kichaa cha mbwa kinaweza kusambazwa na mate ya wanyama, wengi tumezoea kwamba mbwa ndiye anasambaza kichaa, lakini wanyama wengine kama paka, popo, ng'ombe, mbweha, fisi na wengine wanaweza kukisambaza




DALILI ZA MBWA MWENYE KICHAA

siku 1-3 mbwa hubadilika zile tabia ulizozizoea hapa ni ngumu kidogo kugundua

siku 3-4 mbwa huwa na aibu na pia huwa anakwepa mwanga (photophorbia), anajifichaficha na kung'ata kila kitu kinachopita karibu yake hata kama karatasi limepeperushwa na upepo

siku 5 mbwa huanza kulemaa akianzia miguu ya nyuma (hind quarter paralysis) kisha kufuatia miguu ya mbele, baada ya siku saba mbwa hufariki




CHANJO
Mbwa wachanjwe dhidi ya kichaa angalau mara moja kwa mwaka, watoto wanaozaliwa na mama aliyechanjwa wachanjwe baada ya miezi mitatu baada ya kuzaliwa, unaweza kuwachanja kabla kama kuna mlipuko wa kichaa cha mbwa

Sunday, July 19, 2009

MBEGU BORA ZA MAHARAGE

Aina mbili ya mbegu bora za maharage zimeendelezwa/zimezalishwa katika kituo cha utafiti wa kilimo kilichopo Uyole mkoani mbeya. Mbegu hizo ni BILFA 16 na UYOLE 04. Kuzalishwa kwa mbegu hizi bora ni juhudi za muda mrefu za mpango wa kuzalisha mbegu bora za maharage lengo likiwa ni kuongeza uzalishaji na maharage yakiwa katika sifa na ubora unapendekezwa na wakulima pamoja na walaji, wakulima hupendelea mbegu zinazohimili magonjwa, zinazohimili ukame na zenye mazao mengi wakati walaji hupendelea maharage yenye ladha nzuri na yanayoiva kwa urahisi yakiwa katika bei yenye unafuu.

Mbegu ya UYOLE 04 hutambaa, huzaa maharage yenye ukubwa wa wastani mpaka kubwa kabisa zikiwa na rangi ya maziwa, zinahimili magonjwa sugu kama kutu ya maharage na anthracnose, huiva haraka yakipikwa na huwa na ladha nzuri sana

Wakati wa kupanda mbegu hii hutegemea msimu wa kuanza na kuisha kwa mvua, kwa mfano sehemu ambazo mvua huisha mwisho wa mwezi wa 4 au mwanzo wa mwezi wa 5 basi upandaji uanze mwezi wa 3 kwa sababu ukuaji wa mbegu hizi mpaka kukomaa huchukua wastani wa siku 105. Kiasi cha mbegu zinazohitajika kupanda ni kilo 70 – 80 kwa hekta ambapo miche 200,000 huota na huweza kuzalisha kiasi cha tani 1.5 – 1.8 kwa kila hecta, mbegu hii hufaa sana kupandwa nyanda za juu kaskazini (mikoa ya Mbeya, Iringa, Songea na Rukwa) ambako ardhi imeinuka wastani wa mita 800 – 2000 kutoka usawa wa bahari na kuna baridi.


BILFA 16


Mbegu ya BILFA 16 huwa na rangi nyekundu mchanganyiko na maziwa kama nguo ya jeshi, mbegu ni za ukubwa wa wastani, huweza kuhimili sana magonjwa, mimea ni ya kijani kibichi yenye majani madogo madogo huwa na matawi 4 – 5 maua huwa na rangi ya pinki na vishubaka vya maharage huwa vyeupe na vikikomaa huwa rangi ya maziwa

. Kiasi cha mbegu zinazohitajika kupanda ni kilo 70 – 80 kwa hekta ambapo miche 200,000 huota na huweza kuzalisha kiasi cha tani 1.2 – 1.5 kwa kila hecta, ambacho ni kidogo ukilinganisha na UYOLE 04, mbegu hii hufaa sana kupandwa nyanda za juu kaskazini (mikoa ya Mbeya, Iringa, Songea na Rukwa) ambako ardhi imeinuka wastani wa mita 800 – 2000 kutoka usawa wa bahari na kuna baridi. Na mbegu hii hukoma baada ya siku 80 – 84 tangu kupandwa kwa hiyo hufaa kwenye maeneo yenye mvua za muda mfupi.

Saturday, July 11, 2009

MIGOMBA - KANUNI ZA KILIMO BORA

Hapa Tanzania kilimo cha migomba kimekuwepo Kwa miaka mingi. Kilimo hiki ni maarufu sana kwa sababu zao la ndizi limekuwa likitumika kama chakula kikuu kwa baadhi ya mikoa kama vile Kagera, Kilimanjaro na Mbeya na hivyo kulifanya muhimu, kufuatia mazao ya mahindi, mpunga, mtama, muhogo,viazi na mazao ya jamii ya kunde kama vile maharage.
Zao la ndizi linaweza kuwa moja kati ya mazao ya biashara iwapo litazalishwa kwa kufuata kanuni bora za uzalishaji wa zao hilo, ikwa ni pamoja na kupanda aina bora ya migomba inayozaa ndizi zinazotambulika katika masoko ya kimataifa.

ASILI YA MIGOMBA
Asili ya migomba ni nchi za Malaysia na India ambazo ziko Kusini Mashariki mwa Asia. Migomba inayolimwa sasa imetokana na migomba ijulikanayo kama Musa balbisiana ambayo asili yake ni India, na Musa acuminata ambayo asili yake ni Malaysia. Kutoka Malaysia na India migomba ilifika Afrika Mashariki katika karne ya tano

MAENEO YANAYOLIMWA MIGOMBA NCHINI

Nchini Tanzania mikoa inayoshughulika na kilimo cha migomba na kuzalisha zao la ndizi kwa wingi ni pamoja na Kagera, Kilimanjaro, Mbeya, Arusha, Manyara, Mara, Tanga, Morogoro, Kigoma, na Pwani. Hata hivyo zao hili linaendelea kuenea katika mkoa mingine nchini ikiwa ni pamoja na Dar es salaam,, Mwanza, Ruvuma, Shinyanga na Lindi. Pia Dodoma na Singida.
Kilimo cha migomba kinaweza kufanyika katika kipindi chote cha mwaka kulingana na kiasi na mtawanyiko wa mvua hasa mabondeni au kwa umwagiliaji.



MATUMIZI
Kilimo cha migomba kina faida nyingi, baadhi ya faida za migomba na
zao la ndizi ni: -
1Zao la chakula
2Zao la Biashara
3Kutengenezea pombe
4Kulisha mifugo
5Kutengenezea mbolea (mboji)
6Matandazwa shambani (mulch)
7Kutoa kivuli
8Kutoa nyuzi
9Kutengenezea vitu vya sanaa
10Kamba
11Malighafi ya kutengeneza vyakula na vinywaji mbalimbali.
12Dawa
13Majani kama miamvuli, sahani, vikombe na kata
14Kuezekea.

Ndizi kwa ajili ya chakula hutumika kwa kutengeneza vitu mbalimbali-:
1Makangale (Banana figs)
2Poda (Powder)
3Chenge (chips)
4Jeya (flakes),
5Juisi,
6Lahamu (jam)
7Vinywaji baridi, kama soda
8Mvinyo (Wine)
9Pombe kali
10Hamira

UZALISHAJI
Zao la ndizi likizalishwa kwa utaalamu unaokubalika huweza kutoa mazao yenye ubora wa hali ya juu na kuongeza uzalishaji kwa eneo. Mambo yafuatayo yafaa kuzingatiwa katika uzalishaji wa zao hili.

(a) Hali ya hewa
Kiasi cha chini cha mvua kifaacho ni 100mm kwa mwezi au 1200mm kwa mwaka. Mwinuko ni kutoka usawa wa bahari hadi mita 1800 juu ya usawa wa bahari. Zaidi ya mwinuko huo migomba haikui vizuri. Kiasi cha joto kinachofaa ni nyuzi joto za sentigredi 25 hadi 30 chini ya nyuzi joto 16 migomba haikui vizuri. Migomba hustawi vizuri kwenye udongo wenye rutuba ya kutosha, kina kirefu, usiotuamisha maji na pia usiwe na chumvi. Chachu ya udongo inafaa iwe kati ya pH 5 hadi 8.

(b) Aina za ndizi
Kuna aina nyigi sana za ndizi. Nchini Tanzania ndizi zinazozalishwa, zipo za aina nyingi ambazo hutofautiana kwa majina kutokana na eneo au mkoa unaozalisha. Hata hivyo zinaweza kugawanywa katika makundi mawili. Aina ambayo huliwa kwa kuzichoma, kukaanga au kupikwa zikichanganywa na vyakula vingine kama vile nyama. Aina za ndizi hizo ni pamoja na Mzuzu, Mshale, Matoke, Bokoboko na Mkono wa Tembo.
Aina nyingine ni zile ambazo huliwa kama matunda, aina hizo ni kama vile Kisukari, Kimalindi, Mzungu na Mtwike.

Kuna aina nyingine za ndizi ambazo kwa sasa huzalishwa hapa nchini ambazo zina fahamika kwa ubora wake katika masoko ya ndizi ya kimataifa. Aina hizi ni pamoja na Williams, Grand Naine, Pazz, Jamaica, Gold Finger, Nyingine ni Uganda green, Embwailuma Giant na Chinese Cavendish.



(c) Utayarishaji wa shamba
1Safisha sehemu inayohusika kwa kutumia zana ulizonazo.
2Ng’oa visiki vyote na mizizi yake yote
3Lima sehemu hiyo kwa kutumia jembe la mkono, rato, au trekta ili kuwezesha mizizi laini ya migomba kupenya ardhini kwa urahisi.
4Baada ya visiki na magugu yote kuondolewa na hivyo ardhi kuwa wazi, uchimbaji wa mashimo ya kupandikiza machipukizi au miche ya migomba unaweza kufanyika.

(d) Nafasi ya kuchimba mashimo
Mashimo yatachimbwa kwa nafasi inayokusudiwa kutumika kati ya
mashina ya migomba na kati ya mistari kama ifuatavyo:-
1Migomba inaweza kupandwa kwa nafasi ya Umbali wa meta
2.75 kwa 2.75 kwa migomba mifupi kama Kimalindi na
Kisukari. (Mashina 1,331 kwa hekta )
2Umbali wa meta 3 kwa meta 3 kwa migomba ya urefu wa kati
kama Jamaica na Mshale (Mashina 1,110 kwa hekta)
3Umbali wa meta 3.6 kwa meta 3.6 kwa migomba mirefu zaidi kama
Uganda green Mashina 760 kwa hekta).

(e) Uchimbaji mashimo.
Uchimbaji mashimo inafaa ufanywe mapema kiasi cha juma moja hadi mwezi kabla ya muda wa kupanda. Shimo lichimbwe kwa kutenganisha udongo wa juu na wa chini.

Vipimo vya shimo ni vyema vikazingatiwa. Iwapo utachimba shimo la mviringo litafaa liwe na kipenyo cha sentimeta 60 hadi 90 na kina cha sentimeta 60 hadi 90. Iwapo utachimba shimo la mstatili au mraba litakuwa na urefu, upana na kina cha sentimeta 60 hadi 90, kutegemea kiasi cha mbolea kilichopo na kiasi cha kvua kinachonyesha sehemu hiyo. Uwekaji wa mbolea hufuatia mara baada ya mashimo kuwa tayari. Kiasi cha madebe 5 ya mbolea ya samadi iliyooza vizuri au mboji iwekwe kwenye lundo la udongo wa juu kando ya kila shimo na ichanganywe kisha mchanganyiko wa mbolea na udongo urudishiwe katika shimo kisha kijiti kichomekwe katikati ya shimo hilo, ilikuonyesha sehemu ambapo mche au chipukizi litapandwa.

(f) Kuchagua machipukizi bora
Machipukizi mazuri yanayofaa kwa mbegu ni yale yenye sifa hizi hapa chini: -
Sifa za chipukizi bora
1Liwe chipukizi sime, yaani lenye majani membamba na siyo
chipukizi maji yaani lisiwe lenye majani mapana.
2Litoke kwenye mgomba (shina) wenye afya nzuri, usiokuwa na
magonjwa, minyoo ya mizizi, wala vifukusi vya migomba.
3Litoke kwenye mgomba wenye sifa ya kuzaa mikungu
mikubwa.
4Liwe na afya nzuri na lisiwe na dalili za ugonjwa, wadudu, au
mayai ya vifukusi.
5Urefu uwe kati ya meta 1 na meta 2
6Kipenyo cha sehemu ya chini ya shina la chipukizi (tunguu) kiwe ni kati ya sentimeta 15 hadi 25.

(g) Upandaji wa machipukizi
Wakati unaofaa kupanda machipukizi ni mwanzoni mwa msimu wa mvua. Chomoa kile kijiti na chimba shimo la kiasi cha sentimeta 30x30 katikati ya shimo lililojazwa mchanganyiko wa udongo na samadi kisha panda chipukizi hilo.

Rudishia udongo na hakikisha tunguu lote limefunikwa vizuri. Shindilia udongo ili chipukizi lisimame wima imara. Machipukizi yanayo tarajiwa kupandwa yanatakiwa kuondolewa mizizi yote ili kudhibiti minyoofundo na fukuzi wa migomba. Pia maji ya moto au dawa kama vile furadani inaweza kutumika kuulia wadudu kwenye mizizi ya migomba.

UTUNZAJI WA SHAMBA NA MIMEA.
(a) Uwekaji wa matandazwa (mulching
)
Kazi hii ni vyema ikafanywa mara baada ya kupanda kama inawezekana. Matandazo yawe ni makavu na unene wa sentimeta 15 ili kuhifadhi unyevu, kuzuia magugu na yakioza yataongeza mbolea.

(b) Uongezaji wa mbolea
Baada kupanda ni vyema kuongeza mbolea madebe 2 kuzunguuka shina la migomba kila baada ya miaka miwili au mitatu. Mbolea hii inatakiwa kuchanganywa na udongo na kufunikwa kwa matandazwa.

(c) Umwagiliaji maji shambani
Migomba huhitaji maji mengi. Wakati wa kiangazi. Inafaa kumwagilia ili kuto kupunguza sana ukubwa na wingi wa ndizi zinazotarajiwa kuvunwa kwa mwaka. Kiasi cha maji kinachotakiwa kwa wiki ni milimita 25, yaani eneo linalo zunguka shina la migomba lilowe kabisa.

(d) Kupunguzia machipukizi
Inatakiwa kupunguza mimea ya migomba kwa kila shina na kubaki mimea mitatu tu, yaani Mgomba wenye ndizi (Mama), Mgomba mkubwa ambao bado haujazaa lakini unakaribia kuchanua (Mtoto), Mgomba mchanga uliochipua hivi karibuni ( Mjukuu)

(e) Uondoaji wa Majani Makavu
Mimea ya migomba inafaa iondolewe majani yote makavu ili kuondoa uwezekano wa kuwepo mazalia ya wadudu na magonjwa, kuruhusu mionzi ya jua na kufanya urahisi wa kuhudumia shamba .Pia hufanya shamba kuonekana safi.

(f) Uondoaji wa ncha mwishoni mwa matunda
Baada ya mkungu kutoa ndizi, ua hunyauka na kubakiza ncha mwishoni mwa matunda. Ncha hizo hupaswa kuondolewa .Huduma hii husaidia kupunguza uwezekano wa kujeruhi matunda wakati wa kusafirisha jambo ambalo kupunguza ubora wa tunda.

(g) Kuweka Miega
Miega ni nguzo au kamba ambazo hutumika kuzuia migomba iliyobeba mikungu mikubwa isianguke kutokana na uzito mkubwa. Miega ni ya lazima katika sehemu zenye upepo mkali. Kazi hii inatakiwa kufanywa kwa uangalifu ili isijeruhi ndizi na mgomba wenyewe.




(h) Uondoaji wa kichombezo cha ua la kiume (Shumba)
Uondoaji wa shumba huwezesha matunda kukua vizuri, kuongezeka uzito wa mkungu pia huzuia magonjwa kama vile ugonjwa wa mnyauko wa migomba (Banana Baterial Wilt), ugonjwa wa Majivu nchani mwa matunda (Cigar end rot). Ukataji hufanyika juu ya kovu la pili baada ya kichana cha mwisho, kwa kutumia kisu kikali.

UVUNAJI
Zao la ndizi huweza kuanza kuvunwa katika kipindi cha miezi 9 hadi miezi 15 tangu kupandwa kwa chipukizi. Muda wa kuvunwa hutegemea hali ya hewa. Katika sehemu za joto ndizi huvunwa mapema zaidi kuliko sehemu za baridi. Pia migomba iliyopandwa kwa kutumia machipukizi huzaa mapema kuliko iliyopandwa miche iliyozalishwa kwa chupa (tissue culture)

MATUMIZI YA RIBONI

Riboni za rangi moja (au alama ya kamba) hufungwa kwenye migomba ya umri mmoja mara tu inapoanza kuchanua, na riboni ya rangi nyingine hufungwa kwenye migomba itakayoanza kuchanua wiki mbili hivi zinazofuata na kuendelea hivyo ili kurahisisha kuitambulisha mikungu ambayo itavunwa kwa wakati mmoja. Pia matumizi ya riboni hurahisiha utunzaji wa kumbukumbu ili kujua ni lini na ni mikungu mingapi itavunwa.

WAKATI UNAOFAA KUVUNA
Mkungu wa ndizi huweza kuvunwa katika hatua tofauti kulingana na matumizi, aina na mahitaji ya soko. Mkungu huachwa kwenye mgomba mpaka vidole (matunda ) vimejaa. Uzito wa mkungu hongezeka haraka katika wiki mbili za mwisho, ambapo migongo ya ndizi hutoweka.
Ndizi zinaweza kuvunwa zikiwa zimekomaa na zimeiva kwa kiasi cha asilimia 75 kwa ajili ya kusafirishwa mbali, pia zinaweza kuvunwa zikiwa kukomaa na zimeanza kuiva kwa ajili ya soko la karibu, au zikiwa zimekomaa na kuiva kabisa kwa ajili ya soko na matumizi ya nyumbani Njia bora ya kukata mkungu, ni ile inayohakikisha kuwa mkungu wa ndizi hauanguki chini na kuvunja, kuchubuan au kuharibu ndizi, jambo ambalo litapunguza ubora. Ukichelewa kuvuna ndizi zinaweza kuharibiwa na ndege, wanyama, wadudu au kuibiwa.

MKUNGU WA NDIZI AMBAO UMEONDOLEWA SHUMBA


UBORA WA NDIZI
Ndizi zenye sifa nzuri sokoni ni zile ambazo zimekomaa kwa kiasi kinachotakiwa na zenye vidole vyenye urefu mzuri na visivyo na michubuko. Pia ziwe hazijashambuliwa na magonjwa wala wadudu waharibifu.

KIASI CHA MAVUNO
Mavuno ya ndizi hutegemea zaidi aina ya migomba, hali ya hewa, utunzaji wa mimea shambani. Mavuno huweza kufikia hadi tani 60 au zaidi kwa hekta kwa mwaka. Hata hivyo mavuno mazuri kwa mkulima wa kawaida yasipungue kati ya tani 20 hadi 30 kwa hekta kwa mwaka.

MAGONJWA
Ugonjwa wa hatari sana ulioingia hivi karibuni katika wilaya ya Muleba na maeneo mengine mkoani Kagera kutoka nchi jirani ya Uganda ni wa Mnyauko wa migomba unaosababishwa na bakteria (Banana Bacterial Wilt). Magonjwa mengine yanayosumbua zao hili ni Kuoza tunguu, Ugonjwa wa panama, Ugonjwa wa majivu nchani mwa tunda, Sigatoka, na Moko.

WADUDU WAHARIBIFU
Wadudu wanaosumbua zaidi hili ni Minyoo fundo (Banana nematodes), na Vifukuzi (Banana weevils).

UDHIBITI WA MAGONJWA NA WADUDU WAHARIBIFU
Magonjwa na wadudu hawa huweza kuepukwa kwa kufuata kanuni bora za uzalishaji wa zao hili. kama usafi wa shamba na kuchagua chipukizi bora. Au kupanda miche iliyozalishwa kwa chupa (Tissue culture banana seedlings) Hata hivyo mara mataizo haya yakitokea muone mtaalam wa kilimo aliye karibu ili aweze kukupa ushauri wa dalili za ugonjwa wa mnyauko wa migomba unaosababishwa na bakteria

Friday, July 3, 2009

MAJI MOTO-RAFIKI WA MKULIMA




1.0 Utangulizi
Majimoto (Oecophylla longinoda) ni wadudu maarufu sana katika Kanda ya Kusini mwa Tanzania. Wanaitwa Majimoto kwa sababu wanapouma,, huleta maumivu kama ya maji ya kukandia jeraha!. Kwa msingi huo huo, wayao huwaita “malumila” wasambaa huwaita “madadada” na Wamwera nao huwaita “ mangongongo”. Majimoto ni maarufu sana kwa uhodari wao wa kujenga viota kwa kufuma majani mabichi .
Ukubwa wa kiota hutegemea ukubwa wa ukoo, aina ya mti na majani yatumikayo na ulaini wa majani yenyewe. Kuna aina ya miti zaidi ya 75 ambayo Majimoto wameonekana kujenga viota vyao, ikiwa ni pamoja na mikorosho, michungwa, miembe na mengineyo.



Utafiti wa awali uliofanyika kwa mahojiano na wakulima mbalimbali, umeonyesha kwamba wengi hawajui faida yoyote toka kwa wadudu hawa, zaidi sana walisimulia athari zao kwamba ni wadudu wanaouma sana na kuleta maumivu makali. Nimeandaa makala hii ili kuhamasisha na kufundisha watu kwamba Majimoto ni rafiki wa mkulima.

2.0 Maisha ya Majimoto
Ukoo wa Majimoto una malkia mmoja tu ambaye analishwa na watenda kazi wakuu, ambapo yeye kazi yake ni kutaga mayai. Akitaga mayai watenda kazi wadogo (minor workers) ndio huchukua na kuatamia na hatimaye kuwatunza wachanga wanapototolewa.

Watenda kazi wakuu ndio hufanya mawindo na mashambulizi makali katika mti hadi ardhini, nao hukamata wadudu aina nyingi tu ambao wanakutana nao. Mmoja akimshika mdudu, hutoa harufu ya tahadhari na kufumba na kufumbua Majimoto wengi hujikusanya na kusaidia mashambulizi hadi kuua na hatimaye kupeleka chakula katika viota vyao.




Majimoto hupenda kuishi na kuwalinda wadudu wengine aina ya “Homoptera” katika namna ya ushirika. “Homoptera” hao, kama vile Hilda spp, Coccos spp n.k., hutoa aina ya majimaji mwilini mwao (honey dew) ambayo hutumika kama chakula kikuu kwa Majimoto; wakati huo huo, wadudu hao hunufaika kwa ulinzi toka kwa Majimoto dhidi ya adui wa kila namna. Uhusiano huu hauleti madhara yoyote kwa wakulima wa korosho.

3.0 Matumizi ya Majimoto katika kuthibiti wadudu waharibifu
Tangu miaka ya nyuma (AD 304), Majimoto walitumika huko China kuthibiti wadudu waharibifu katika mazao kama vile michungwa. Katika nchi ya Tanzania, matokeo ya majaribio yameonyesha kwamba Majimoto ni wadudu mashuhuri sana katika kuthibiti mbu wa mikorosho na minazi. Mikorosho yenye Majimoto wengi haishambuliwi na mbu kulinganisha na ile isiyo nao. Majimoto wakitanda kwenye machipukizi, maua au tegu, hufanya ulinzi mzuri sana dhidi ya mashambulizi ya mbu waharibifu. Asilimia 65 ya mashamba ya korosho Kusini mwa Tanzania, tayari kuna makoloni ya wadudu hawa, lakini siyo mikorosho yote katika shamba ina Majimoto na asilimia 85 ya michungwa yote Tanga ina makoloni ya majimoto Hivyo, kuna haja kubwa ya kuwaneemesha Majimoto

:
3.1 Jinsi ya kuwaneemesha Majimoto.
Majimoto kama rafiki wa mkulima wanahitajika waneemeshwe ili waongezeke na wawe wengi katika mikorosho ili kufanya ulinzi thabiti dhidi ya wadudu waharibifu. Mbinu ambazo hutumika kuwaneemesha Majimoto ni pamoja na:
• Kuhamisha na kupandikiza Majimoto

Majimoto wanaweza kuhamishwa toka mti mmoja na kupandikizwa katika mti mwingine. Viota vya Majimoto vinaweza kukatwa toka mti mwingine na kufungiwa katika matawi ya mti mwingine, hasa karibu na eneo lenye machipukizi mapya. Majimoto hawa wanaweza kujijenga, kuzaliana na kuanzisha makoloni mengine mapya katika miti waliohamishiwa. Hii inadhihirika kwa ongezeko la idadi ya viota vinavyojengwa wiki moja hadi nyingine.
Angalia: Majimoto wa koo/familia mbili tofauti wanaweza kudhuriana. Uangalifu ufanyike kiasi kwamba upandikizaji wa Majimoto ufanyike kwenye mti ambao hauna kundi lingine ili kuepuka ugomvi na mauaji baina yao.

• Kueneza kwa njia ya kamba


Majimoto wanaweza kuenezwa kwa kutumia kamba kutoka mti mmoja hadi mwingine, ili kuifanya kamba kama daraja la juu kwa juu. Kamba inapaswa kufungwa kwenye tawi karibu na kiota cha Majimoto nao wataweza kupita hadi mkorosho mwingine na kuanzisha makoloni mapya hatimae kuzidi kuongezeka.
Majimoto hupendelea kupita kwenye kamba za kienyeji na hasa kamba zitokanazo na ukindu au magome ya miti. Hawapendelei kupita kwenye kamba za viwandani, hivyo epuka kutumia kamba ya katani au nailoni kwa ajili ya kazi hii na pia usishike kamba ya kienyeji kama umeshika vitu vyenye harufu kali kama mafuta ya kujipaka.

• Kuthibiti adui wa Majimoto


Imefahamika kwamba jamii ya Sisimizi (Pheidole megacephala) pichani juu na Sangala ni maadui wa Majimoto. Miti ambayo imetawaliwa na wadudu hawa, ni vigumu kukuta Majimoto wakijitawala. Ili kuwaneemesha Majimoto, inatupasa kuwadhibiti wadudu hawa.
Dawa ya AMDRO ndiyo itumikayo kuangamiza sisimizi. Dawa hii iliyo kama sukari, hunyunyizwa kuzunguka shina la mti lenye sisimizi. Kiasi cha gramu 4 za dawa hii kwa mti, inatosha kuthibiti sisimizi. Dawa inarudiwa tena endapo dalili za sisimizi kujitokeza tena zitaonekana.

Jinsi ilivyotengenezwa dawa hii, sisimizi huonekana kuipenda sana; maana, mara tu baada ya kunyunyiza, huibeba na kumpelekea malkia wao, ambaye baada ya kula hufa akifuatiliwa na ukoo mzima wa sisimizi. Kwa hiyo baada ya siku mbili tatu hivi, sisimizi wote watakuwa wamekufa, hivyo kutoa nafasi kwa Majimoto kuweza kutawala eneo lote.



Sangala hawadhuriki na dawa hii ya Amdro, badala yake, utafiti unaendelea kufanyika ili kupata dawa ya kuwathibiti sangala. Hata hivyo, grisi ya miti na wakati mwingine oili chafu, hutumika kuzungushia kwenye mashina ya miti iliyoshambuliwa na sangala ili kuwadhibiti wasipande juu. Matumizi ya ile kamba ya kuhamishia Majimoto kama daraja la juu

Friday, June 26, 2009

NAZI

MNAZI



Tumezoea kwamba siri ya umri mrefu ni maji, lakini si maji peke yake ila yaambatane na ulaji mzuri, leo nawaletea siri ya NAZI ambazo ni zao la mti wa mnazi (cocos nicifera) ambao uko katika jamii ya mipama (palms) inayojumuisha miti kama michikichi, mitende na mingineyo tuyoitumia kama mapambo

NAZI KABLA YA KUFULIWA MAGANDA


Mti wa mnazi au MTI WA UHAI kama ninavyouita ni mmea unaostawi na kupatikana kanda za pwani na sehemu zenye joto, mikoa kama Tanga, Dar, Pwani, Mtwara, Lindi, Mafia na Zanzibar hupatikana kwa wingi. Kila sehemu ya mti huu inatumika katika maisha ya kila siku ya mwanadamu, makuti kuezekea na kutengenezea mafagio, tunda lake ni chakula, maganda ya nazi kwa ajili ya kuzuia upotevu wa maji kwenye bustani/shambani (mulching) magogo hutoa mbao na hutumika kutengenezea mitumbwi, na sehemu yoyote ya mnazi huweza kutumika kwa ajili ya kupikia kuanzia makuti, mahanda, vifuuu n,k

NAZI BAADA YA KUFULIWA


Jamii za watu wanaotumia sana nazi huwa hazishambuliwi na magonjwa kama kisukari, presha ya kupanda na magonjwa mengine ya moyo na kiasi kikubwa cha lehemu (cholesterol) mwilini ukilinganisha na jamii zinazotumia vyakula vyenye kupikwa na mafuta yanayotokana na mimea mingine kama karanga, alizeti, ufuta, mahindi n.k. kwa mfano mikoa kama Tanga na Zanzibar ambako kwa wastani mtu hutumia kiasi cha nazi 120 kwa mwaka katika vifo 1000 vya watu wazima ni vifo 1 – 2 vinavyohusiana na magonjwa ya moyo wakati mikoa ambayo hawatumii nazi karibu robo ya vifo hutokana na magonjwa ya moyo.

MAHANDA YA NAZI



Kuna taarifa kwamba nazi huongeza kiasi cha lehemu mwilini je ni vipi? Ukweli ni kwamba nazi inayotumika moja kwa moja yaani inakunwa na kupikiwa hapo hapo haina madhara ya lehemu, ila nazi inayohifadhiwa ndio huwa na tatizo hili kwa sababu huchanganyika na hewa ya haidrojeni (hydrogenation) na kuwa sawa na yale mafuta mengine ya viwandani KWA HIYO nazi iliyohifadhiwa baada ya kukunwa au tui lililohifadhiwa huweza kusababisha kuongezeka lehemu mwilini

NAZI ILIYOVUNJWA


Moja kati ya vyakula vichache duniani ambavyo walaji hawana mzio (allergy) nacho ni nazi, pia inasifika kwa kupunguza kiasi cha sukari mwilini, maji ya dafu husafisha figo na kibofu

NAZI ILIYOKUNWA TAYARI KUTENGENEZEWA TUI


MAHANDA YA NAZI YAKIZUIA UPOTEVU WA MAJI KWENYE CHUNGU CHA MAUA